Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, Amewakaribisha Wawekezaji na Wafanyabiashara Kutoka Nchini Nigeria Kuwekeza Zanzibar.

 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Balozi wa Nigeria Nchini Tanzania Mhe.Dk. Sahabi Isa Gada,(kulia kwa Rais) akiwa na Ujumbe wa Wafanyabiashara kutoka Nchini Nigeria, wakiwa katika mazungumzo hayo yaliofanyika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar.  

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amewakaribisha wawekezaji na wafanyabiashara kutoka Nigeria kuja kuekeza Zanzibar katika sekta yoyote wanayoitaka.

Hayo aliyasema leo wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Nigeria katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Sahabi Isa Gada Ikulu Jijini Zanzibar akiwa amefuatana na ujumbe wa wafanyabiashara na wawekezaji wa  Kampuni ya IBRU kutoka nchini Nigeria.

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein alisema kuwa Zanzibar ina rasilimali nyingi za uwekezaji hivyo ni vyema wafanyabiashara na wawekezaji hao wakaangalia sekta wanayoitaka na baadae kutumia fursa hiyo ya kuekeza.

Rais Dk. Shein alisema kuwa licha ya Kampuni hiyo kuwa na uzoefu katika uwekezaji wa sekta mbali mbali ikiwemo sekta ya uvuvi ambapo imeweza kuekeza ndani na nje ya Nigeria pia, ni vyema wakaangali uwezekano wa kuja kuekeza Zanzibar katika sekta nyengine zilizopo.

Alieleza kuwa mbali ya juhudi kubwa zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha sekta ya uvuvi ikiwa ni pamoja na kuifufua Kampuni yake ya uvuvi iliyoanzishwa miaka ya 70 na kuianzisha tena upya miaka mitatu iliyopita bado kunahitajika mashirikiano ya pamoja na Kampuni zenye uzoefu katika sekta hiyo.

Aidha, Rais Dk. Shein alimueleza Balozi huyo na ujumbe wake kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeweka milango wazi kwa wawekezaji wanaotaka kuja kuekeza Zanzibar ikiwa ni pamoja na kuwawekea mazingira mazuri kupitia Mamlaka ya Uwekezaji Vitega Uchumi Zanzibar (ZIPA).

Rais Dk. Shein alieleza kuwa Zanzibar inahitaji viwanda vya uvuvi hasa ikizingatiwa kuwa imezungukwa na bahari ambayo ina rasilimali nyingi wakiwemo samaki wenye sifa duniani lakini bado uvuvi wa bahari kuu haujafanyiwa kazi ipasavyo kutokana na ukosefu wa vifaa, viwanda vya kuchakata samani na hata utaalamu wa uvuvi wa kisasa.

Alisema kuwa uvuvi ni sehemu ya uchumi wa buluu ambapo Zanzibar haiko tayari kuachwa nyuma na ndio maana juhudi za makusudi zimekuwa zikichukuliwa na Serikali anayoiongoza katika kuhakikisha inatekeleza vyema mchakato huo.

Rais Dk. Shein alieleza imani yake kwa Kampuni hiyo ya IBRU na kuutaka ujumbe huo kuzitumia fursa hizo zilizopo Zanzibar hasa ikizingatiwa kuwa Zanzibar na Nigeria zina uhusiano na ushirikiano wa kihistoria.

Aliongeza kuwa imefika wakati kwa nchi za bara la Afrika kuzidisha ushirikiano wa pamoja katika sekta za maendeleo na uchumi hasa ikizingatiwa kuwa Afrika ina utajiri mkubwa wa rasilimali.

Hivyo, Rais Dk. Shein alisisitiza haja kwa nchi za Bara la Afrika kufanya kazi kwa pamoja na mashirikiano ili zipate maendeleo endelevu kwa manufaa ya Mataifa ya bara hilo pamoja na watu wake.

Aidha, Rais Dk. Shein aliipongeza Serikali ya Nigeria kwa kuendelea kushirikiana na Zanzibar katika kuimarisha sekta ya elimu hapa nchini ambapo nchi hiyo imeendelea na utamaduni wake wa kuwaleta waalimu wa Sekondari wa masomo ya Sayansi kuja kusomesha Zanzibar.

Rais Dk. Shein alisema kuwa hatua hiyo ni ya kihistoria kwani Nigeria pamoja na Ghana ni nchi za mwanzo katika Bara la Afrika zilizoiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta ya elimu mara tu baada ya Mapinduzi matukufu ya Januari 12, 1964.

Nae Balozi wa Nigeria katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Sahabi Isa Gada alimueleza  Rais Dk. Shein kuwa ujio wa wafanyabiashara na waekezaji hao kutoka Nigeria unatokana na mazungumzo aliyoyafanya kati yake na Dk. Shein wakati  alipokuja kujitambulisha mnamo Februari 28, mwaka 2018.

Balozi huyo akirejea mazungumzo aliyozungumza na Rais Dk. Shein na kusema kuwa miongoni mwa mambo matatu makubwa waliyozungumza ni pamoja nan chi yake kuleta wawekezaji kuja kuekeza hapa Zanzibar jambo ambalo amelifanyia kazi.

Balozi Gada alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa wafanyabiashara na wawekezaji aliokuja nao katika kutoka Kampuni ya IBRU ya Nigeria wana uzoefu mkubwa katika uwekezaji wa sekta mbali mbali na tayari wameshaekeza nchi kadhaa katika bara la Afrika.

Alisema kuwa wawekezaji hao wanauzoefu na wameweza kuekeza ndani na nje ya Nigeria zikiwemo sekta za uvuvi, mawasiliano, hoteli na utalii, kilimo, usafiri wa anga, mafuta na gesi asilia, usafiri na usafirishaji wa baharini pamoja na sekta ya habari.

Aidha, Balozi Gada alimueleza Dk. Shein kuwa Kampuni hiyo iliyoanzishwa mwaka 1956 imejikita sana katika sekta ya uvuvi kwa nchi ya Nigeria na tayari ina mtandao mkubwa katika kufanya shughuli zake za uvuvi kwa nchi za Magharibi mwa Afrika kama vile Togo, Cameroun, Benin, Mauritania, Gambia, Angola, Namibia pamoja na bahari ya Irish.
 Dk. Shein 
Sambamba na hayo, Balozi Gada alimueleza Rais Dk. Shein hatua zinazochukuliwa na Serikali yake kwa mashirikiano ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali katika kuongeza idadi ya walimu wa masomo ya Sayansi pamoja na mashirikiano kwa vyuo vikuu kikiwepo Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA).

Nao wawekezaji na wafanyabiashara hao walimueleza Rais Dk. Shein jinsi walivyovutiwa na mazingira ya Zanzibar sambamba na rasilimali na ukaribu wa watu wake na kuahidi kuja kuekeza.

Walieleza kuwa kutokana na fursa zilizopo hapa Zanzibar wako tayari kuja kuekeza na kuahidi kuendelea na mchakato kwa kukutana na taasisi husika zikiwemo Wizara na Mamlaka ya Uwekezaji na Vitega Uchumi Zanzibar (ZIPA) na Wizara ya Kilimo.

Sambamba na hayo, wafanyabiashara na wawekezaji hao walieleza uwezo walionao wa kuekeza kutokana na Kampuni yao ya IBRU jinsi ilivyojiimarisha  huku wakisisitiza namna ya sekta ya elimu ilivyoimarika nchini Nigeria na kueleza haja ya kushirikiana na Zanzibar katika kuimarisha sekta hiyo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.