Habari za Punde

Makamu Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein Apiga Kura ya Maoni Kumchagua Mbunge na Mwakilishi wa Jimbo la Tunguu Zanzibar.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi pia Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk.Ali Mohamed Shein akitia kura yake kumchagua Mbunge na Mwakilishi wa Jimbo la Tunguu Wilaya ya Kati  Unguja hafla hiyo imefanyika katika ukumbi wa Dk. Ali Mohamed Shein Tunguu SUZA leo, wakati wa Mkutano Mkuu wa Jimbo la Tunguu wa Kura za Maoni.


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, ambaye pia ni Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar leo alikuwa ni miongoni mwa Wajumbe wa Mkutano Mkuu waliopiga Kura ya Maoni kumchagua Mbunge na Mwakilishi wa Jimbo la Tunguu.

Zoezi hilo limefanyika leo huko katika ukumbi wa Dk. Ali Mohamed Shein uliopo Kampasi ya Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA), huko Tunguu Wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja.

Makamo Mwenyekiti huyo wa CCM Zanzibar akiwa miongoni mwa Wajumbe hao alishiriki kikamilifu katika zoezi hilo la kuwachagua viongozi hao wa Jimbo la Tunguu akiwa ni miongoni mwa Wajumbe 160 waliohudhuria kati ya Wajumbe wote 176 wa Jimbo hilo.

Zoezi hilo lilikuwa na jumla ya wagombea wa nafasi ya Ubunge ambao jumla yao walikuwa kumi na wagombea nafasi ya Uwakilishi jumla yao walikuwa ni 14 ambao mapema walipata fursa ya kujielezea na kunadi sera zao mbele ya Wajumbe hao wa Mkutano Mkuu wa Jimbo hilo.

Mapema Mwenyekiti wa CCM Jimbo la Tunguu Ramadhan Khatib Ramadhan aliwasihi Wajumbe wa Mkutano Mkuu huo kuwa zoezi hilo ni utaratimu maalum uliowekwa na Chama Cha Mapinduzi kwa kila ifikapo miaka mitano ya uchaguzi.

Alisema kuwa utaratibu huo ni kwa mujibu wa sheria na Katiba ya CCM ambao unakiongoza chama hicho.

Aidha, aliwataka wagombea wote wa nafasi hizo kukubali na kuridhika na matokeo watakayoyapata kwani waliogombea nafasi hizo ni wengi lakini wanaohitajika ni mmoja kwa nafasi ya Uwakilishi na mmoja kwa nafasi ya Ubunge wa Jimbo hilo.

Mwenyekiti huyo wa CCM Jimbo alisisitiza haja ya kuwachagua viongozi wenye sifa na walio na uwezo wa kukitetea chama hicho na kukitumikia kwa moyo wao wote kutokana na chama hicho kuimarika kwa muda mrefu na kuweza kuasisiwa tokea Mapinduzi matukufu ya Januari 12, 1964.

Pamoja na hayo, kiongozi huyo aliwaeleza Wajumbe na wagombea nafasi hizo kwamba uchaguzi huo utakuwa wa huru na haki kwa kufuata miongozo yote ya Chama hicho cha CCM sambamba na Katiba, sheria na kanuni zake.

Hapo jana wakati akimtambulisha Mgombea nafasi ya Urais kwa tiketi ya CCM Dk. Hussein Ali Hassan Mwinyi kwa wanaCCM na wananchi  wa mikoa miwili ya Pemba, hafla iliyofanyika katika uwanja wa kufurahishia watoto Tibirinzi Chake Chake Mkoa wa kusini Pemba, Rais Dk. Shein aliwataka viongozi katika Majimbo yote nchini kuwachagua viongozi makini, wenye uwezo na tena bila ya kufanya upendeleo.

Rais Dk. Shein aliwataka viongozi hao katika uchaguzi unaofanyika hivi leo kutowachagua wababaishaji wenye tamaa na badala yake wawachague viongozi watakaokiimarisha chama hicho.

Makamo Mwenyekiti huyo alieleza kuwa CCM ni chama kikubwa sana kina viongozi mbali mbali wenye sifa hivyo wasing’ang’aniwe viongozi waliokuwa hawana sifa hao kwa hao kila siku na kusisitiza kuwa ni vyema wakawachagua viongozi wenye sifa ambao wakisimama wanasikilizwa na wanamvuto kwa wapiga kura.

Alisisistiza kuwa viongozi wanatakiwa wawe na sifa nzuri ambazo wataweza kufanya kazi na Dk. Hussein Ali Hassan Mwinyi “Wajadilini kama tulivyowajadili wale 31 waliogombania nafasi ya Urais kupitia chama chetu, wajadilini nje ndani ndani nje”, alisisitiza Makamo huyo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.