KIFO cha
Marehemu Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Bejamin William Mkapa kimeacha pengo kubwa katika uongozi na maendeleo ya
Tanzania, Afrika na duniani kote kwa mchango wake uliooendelea kuhitajika ndani
na nje ya mipaka yaTanzania.
Rais wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, aliyasema hayo leo katika risala aliyoitoa kupitia vyombo vya
habari kufuatia kifo cha Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Bejamin William Mkapa, kilichotoke usiku wa
kuamkia Ijumaa ya tarehe 24 Julai, 2020.
Katika
risala yake hiyo Rais Dk. Shein alisema kuwa Marehemu Mzee Mkapa alikuwa na
uwezo mkubwa wa kubuni mambo mapya ya maendeleo ambapo miongoni mwa mambo
makubwa ambayo aliyaanzisha katika kipindi chake cha uongozi ni kuunda Mamlaka
ya Kodi ya Mapato Tanzania (TRA).
Alisema
kuwa aliunda (TRA) ili kuimarisha ukuaji wa uchumi, kuongeza ukusanyaji wa
mapato na kuiwezesha Tanzania kujitegemea ambapo jitihada zake hizo zilipelekea
Tanzania kukua kwa uchumi wake.
“Tulianza
kulipa madeni ambapo baadae nchi yetu ilisamehewa madeni yake, tulianza
kuaminiwa na tukawa tunakopesheka”, alisema Dk. Shein.
Aidha
alieleza kuwa katika kipindi chake cha miaka kumi uchumi ulikuwa kutoka
asilimia 3.6 hadi 6.7 sambamba na hatua hiyo, alichukua hatua za
kubinafsisha Mashirika ya Umaa ambayo
yalikuwa yakiendeshwa kwa hasara na kuuletea mzigo mkubwa kwa Taifa.
Akimuelezea
Marehemu Mkapa, Rais Dk. Shein alisema kuwa vilevile aliansha Mpango wa Kukuza
Uchumi na Kupinguza Umasikini( MKUKUTA),(MKURABITA) na (TASAF), pamoja na
kuanzisha Wakala kadhaa kama vile EWURA,SUMATRA kwa ajili ya kudhibiti na kutoa
huduma bora kwa jamii.
Alieleza
kuwa baada ya kustaafu kwake aliansiha Taasisi Isiyo ya Kiserikali ya Benjamin Mkapa, ambayo inayoshughulikia
masuala ya afya hasa mapambano dhidi ya UKIMWI.
Katika
masuala ya kupiga vita rushwa na ufisadi, kiongozi huyo alianzisha Tume Maalum
maaraufu kwa jina la Tume ya Warioba iliokuwa na lengo la kupendekeza njia bora
za kuzuia mianya na vitendo vya rushwa.
Alisema
kuwa matokeo ya jitihada hizo ni kuanzisha kwa taasisi ya kudhibiti na kuzuia
rushwa Tanzania (TAKUKURU) na hatimae kupelekea kuundwa kwa Mahakama maalum ya
wahujumu uchumi katika Awamu ya Tano ya Jamhuri ya Mungano wa Tanzania.
Kutokana
na kauli mbiu yake ya “Uwazi na Ukweli”, Rais Mkapa alianzisha Wizara Maalum
inayoshughulikia Utawala Bora, kadhalika alianzisha vitengo vya habari na
Mawasiliano katika Wizara na Mashirika pamoja na kuanzisha utaratibu wa
kuwahutubia wananchi kila mwezi.
Alisema
kuwa hatua hizo zimewawezesha wananchi kuyafahamu matokeo muhimu ya Kitaifa na
Kimataifa ambapo pamoja na suala hilo Marehemu Mzee Mkapa alitambua mapenzi ya
Watanzania katika sekta ya michezo kwa hivyo, alihakikisha anawajengea wananchi
kiwanja cha michezo cha kisasa chenye kiwango cha kimataifa.
Katika
uwanja wa siasa, Rais Dk. Shein alisema kuwa Marehemu Mkapa alikuwa ni mfano wa
wanasiasa bora walioweka mbele maslahi ya Taifa na kuongoza kwa mifano.
Alisema
kwua kwa uhodari mkubwa aliokuwa nao Marehemu Rais Mkapa, aliweza kuendesha
siasa za vyama vingi kwa haki na demokrasia ambapo uongozi wake wa miaka kumi
akiwa Rais, uliipatia Tanzania heshima kubwa katika Jumuiya ya Kimataifa na
ndani ya Taifa hili.
“Alipenda
mashirikiano na kuheshimu mawazo ya kila mmoja na wakati wote alikuwa mchangamfu
na mwenye tabasam….alikuwa na uwezo mkubwa wa kuhimili changamoto za uwongo
kila zinapotokea”, alisema Dk. Shein.
Aidha,
aliongeza kuwa Rais Mkapa alikuwa kiongozi asiyependa fitina na majungu na siku
zote huwapongeza wanaofanya vizuri pamoja na kuwasamehe wale wanaotubu makosa
yao kwake kwa dhati.
Rais Dk.
Shein alisema kuwa Rais Dk. Shein alikuwa mstari wa mbele katika kutetetea na
kuzienzi tunu za Taifa zikiwemo umoja wa Watanzania, Mapinduzi ya Zanzibar na
Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.
Katika
kuamini kwake umuhimu wa kuendeleza umoja na mshikamano miongoni mwa mataifa ya
Afrika Marehemu Mzee Mkapa alitoa mchango mkubwa katika kuanzishwa upya kwa
Jumuiya ya Afrika Mashariki ili kuumarisha mtengemano wa nchi na wananchi wa nchi
za Afrika Mashariki.
Rais Dk.
Shein alisema kuwa Marehemu Mkapa alikuwa muumini wa dhati wa amani ya nchi
ambapo katika kutilia mkazo umuhimu wa kutunza amani kwa maendeleo ya Taifa
katika moja ya hutoba zake alisisitiza umuhimu huo kwa kusema
“Nchi hii
ni nchi yetu sote ni ya watoto wetu na vizazi vyetu vijavyo. Ikiwa na amani ni
amani ya Watanzania wote ikiwa ya vurugu ni vurugu itakayowaathiri Watanzania
wote. Tukivurugana MwenyeziMungu hatotupa ardhi nyengine,tuamue basi kuijenga
Tanzania ya demokrasia ya kweli, Tanzania inayoheshimu haki za binaadamu,
Tanzania inayopiga haraka hatua za maendeleo, Tanzania ya amani, upendo, umoja
na mshikamano”.
Pamoja na
hayo, Rais Dk. Shein, alisema kuwa Marehemu Mzee Mkapa alikuwa na sifa ya
kuibua vipaji vya viongozi wachanga, kuwajenga na kuwakuza na hatimae viongozi
hao kutoa mchango mkubwa katika Taifa.
Rais Dk.
Shein alisema kuwa yeye mwenyewe binafsi alijifunza mambo mengi sana na kupata
mashirikiano ya hali ya juu kutoka kwa Marehemu Rais Mkapa kwa kiasi cha kupata
weledi mkubwa wa kuyatekeleza majukumu yake katika uongozi.
Vile vile,
Rais Dk. Shein aliwasihi Watanzania kuendelea kuwa wamoja, kuyaenzi na
kuyadumisha yale yote aliyoyaacha Mzee Mkapa huku akisisitiza kuwa ni vyema
kuzingatia fikra na mawazo yake kupitia hotuba zake mbali mbali pamoja na yale yaliomo
katika kitabu chake cha “My Life My Purpose” (Maisha yangu Kusudi langu).
Rais Dk.
Shein aliongeza kuwa kwa niaba ya Wananchi na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
anaungana na wanafamilia, ndugu, marafiki na Watanzania wote katika kipindi
hichi kigumu cha majonzi na huzuni.
Rajab Mkasaba, Ikulu
Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment