Habari za Punde

SMZ Awamu ya Saba Imepata Mafanikio Makubwa Katika Kuendeleza na Kuimarisha Sekta ya Viwanda na Biashara Nchini.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Uongozi wa Wizara ya Biashara na Viwanda Zanzibar, katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza kuwa  Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Awamu ya Saba imepata mafanikio makubwa katika kuendeleza na kuimarisha sekta ya viwanda na biashara hapa nchini.   

Hayo aliyasema leo, Ikulu mjini Zanzibar alipokutana na uongozi wa Wizara ya Biashara na Viwanda wakati ilipowasilisha utekelezaji wa Mpango Kazi wa Mwaka 2019/2020, na Mpango Kazi wa mwaka 2020/2021.

Rais Dk. Shein alisema kuwa katika kipindi hicho juhudi kubwa zimefanywa katika kuimarisha Sheria, Sera na miongozo mbali mbali sambamba na kuimarisha miundombinu muhimu kwa ukuaji wa sekta ya biashara na viwanda.

Aidha, Rais Dk. Shein alisisitiza kwamba misingi hiyo iliyojengwa ni vyema ikaendelezwa ili Serikali ijayo ya Awamu ya Nane iweze kuanza utekelezaji wa mipango yake kwa kasi zaidi.

Rais Dk. Shein alisema kuwa Wizara hiyo imepata mafanikio makubwa hasa katika kipindi hichi cha miaka mitano chini ya uongozi wa Waziri wa Wizara hiyo hivi sasa Balozi Amina Salum Ali.

Alisema kuwa misingi ya biashara iliyoanzishwa imesaidia sana kukua na kuimarika kwa biashara huria Zanzibar sambama na kuvifufua na kuviendeleza viwanda mbali mbali kikiwemo kiwanda cha Sukari, Mahonda pamoja na ongezeko la uzalishaji wa bidhaa mbali mbali ambazo umesaidia upatikaji wa huduma na usalama wa chakula.

Pia, aliwasifu wawekezaji wa ndani kwa kujenga ujasiri wa kuekeza katika maeneo mapya ya biashara ndani na nje ya nchi katika sekta mbali mbali.

Katika maelezo yake, Rais Dk. Shein alipongeza hatua zilizochukuliwa na Wizara hiyo za kuimarisha na kuanzisha viwanda hapa Zanzibar huku akipongeza mashirikiano yaliopo ambayo yamepelekea kupata mafanikio hayo.

Rais Dk. Shein alieleza matumaini yake makubwa ya kuwa zao la karafuu litaendelea kuimarika pamoja na bei yake ili nchi pamoja na wananchi wake waendelee kupata tija na mafanikio zaidi.

Rais Dk. Shein alitoa pongezi kwa uongozi wa Wizara hiyo kwa kutimiza vyema wajibu wao na kuitumikia ipasavyo Serikali yao na kueleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imepata mafanikio makubwa na hivi sasa tayari imeshaingia katika nchi zenye uchumi wa kati kwani ina nguvu za kiuchumi.

Akizungumzia vikao vya kutathmini utekelezaji wa mpango kazi ambavyo vimekuwa vikifanyika katika kipindi chote cha uongozi wake, Rais Dk. Shein alisema kuwa vikao hivyo (bango kitita) ambavyo ni vya mwisho katika muda wa uongozi wake, vimemsaidia kwa kiasi kikubwa kufuatilia utekelezaji wa mipango ya Serikali katika Wizara zake.

Nae Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee aliupongeza uwasilishwaji Mpango Kazi huo iliyofanywa na Wizara hiyo na kusema kuwa miaka mitano ya uongozi wa Balozi Amina Salum Ali Wizara hiyo imekuwa na mabadiliko makubwa.

Alisema kuwa mikutano hiyo ya (Bango Kitita) imekuwa na msaada mkubwa katika Wizara za Serikali na kueleza haja ya kuendelezwa huku akisisitiza haja kwa viongozi na wafanyakazi wa Wizara hiyo kuendelea kuchapa kazi hasa katika kipindi hichi cha kuelekea uchaguzi mkuu ujao wa mwezi Oktoba mwaka huu.

Mapema Waziri wa Biashara na Viwanda Balozi Amina Salum Ali alieleza kuwa Wizara katika mwaka 2020/2021 inatarajia kuyaendeleza na kuyapima maeneo ya viwanda ambapo Wizara hiyo inaandaa Mpango wa matumizi na upembuzi yakinifu kwa eneo la Dunga.

Aidha, alisema kuwa Wizara inakusudia kuliandaa eneo la Nyamanzi na kuandaa Matamasha mbalimbali ambapo Wizara inakusudia kuliandaa kwa ajili ya ubia eneo hilo kwa hatua za awali kufanya tathmini ya kimazingira na kijamii (ESIA) pamoja na kulisafisha.

Kwa upande wa Shirika la Taifa la Biashara (ZSTC), Shirika hilo limefanikiwa kuzindua mtambo mpya wa uzalishaji wa mafuta ya Mikaratusi katika kiwanda cha  mafuta ya Makonyo na Arki za mimea huko Wawi Pemba.

Alisema kuwa Wizara kupitia Shirika hilo la (ZSTC) inatarajia kuanzisha kiwanda cha kusarifu mwani katika eneo la Chamanangwe Pemba kwa kushirikiana na wawekezaji kutoka Indonesia.

Nao uongozi wa Wizara hiyo ulimpongeza Rais Dk. Shein kwa uongozi wake bora uliotukuka ambao umewawezesha kufanya kazi zao kwa ufanisi mkubwa kutokana na busara, hekima na maelekezo mazuri waliyoyapata kutoka kwa Rais Dk. Shein sambamba na kuimarika kwa sekta ya biashara na viwanda.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.