Na Mwashungi Tahir Maelezo 26-9-2020.
Mwenyekiti wa Klabu ya kusoma vitabu Maryam Hamdani amewataka wanafunzi na jamii kujenga utamaduni wa kusoma vitabu katika Maktaba ili kupata kufahamu mambo mbali mbali.
Amesema wanafunzi watapokuwa utamadini wa kusoma vitabu watazidi kupata upanuzi zaidi wa kujua mambo na kuweza kuwasaidia katika masomo yao na kufahamu mambo mengi yaliyo kwenye vitabu.
Akizungumza na wanafunzi wa kidato cha nne kutoka skuli ya Amani Abeid Karume ya Kinuni, Mwanakwerekwe A na Benmbella huko katika ukumbi wa Maktaba Kuu Zanzibar ilioko Maisara wakati wa kuwasilisha uchambuzi Riwaya ya kitabu cha Takadini na kutolewa ufafanuzi namna ya kujibia mitihani .
Amesema lengo la klabu hiyo ni kuwashajihisha wanafunzi kupenda kusoma na kujifunza kutunga vitabu kwani utunzi ni fani nzuri inayoweza kumkomboa mwanafunzi na kupata uelewa zaidi katika kujiendeleza.
Amefahamisha kuwa vitabu vingi vinapatikana sehemu za Maktaba lakini kwa sasa hata katika mitandao pamoja na kwenye simu na kurahisisha kupata masomo unayoyahitaji ili kusoma sehemu yoyote kwa amani na utulivu.
“Acheni kutumia simu kwa matumizi yasiyokuwa sahihi tumieni kwa lengo la kujifunza mambo ambayo yanaendana na wakati wenu “, aliwaasa wanafunzi hao.
Mwenyekiti huyo amewataka wazazi kuwa karibu na watoto wao kuwatengea muda wa kudurusu masomo yao kwa lengo la kuweza kufahamu zaidi na kutosau waliyofundishwa na sio kuwapa majukumu.
“Natoa wito kwa wazazi na walezi muwe karibu watoto wetu kwa kuwalinda na kuwashajihisha kushughulikia masomo yao”, alisema Mwenyekiti Maryam Hamdan.
Nae Katibu wa Klabu hiyo Dkt Mwanahija Ali Juma amewataka wanafunzi hao kuwa watulivu kuzingatia mafunzo waliyoyapata kuhusu jinsi ya kufanya uchambuzi wa vitabu na kuweza kufanya vizuri katika mitihani yao na pia walimu kwa wenzao.
Ameeleza kuwa tangu kuanzishwa klabu hiyo wameweza kupata mafanikio makubwa katika kukikuza Kiswahili kwani jamii imekuwa na mwamko wa kusoma vitabu katika maktaba na kupata uelewa umuhimu kuzitumia huduma hiyo.
“Kusoma sio lazima darasani elimu ni bahari someni vitabu na majarida ili muweze kupata mambo muhimu muelimishe jamii”, alisema Katibu huyo.
Mkurugenzi wa Bodi ya Huduma za Maktaba Kuu Sichana Haji Fum amesema Serikali inatambua kuwa baadhi ya wazazi na walezi hawana uwezo wa kuwanunulia watoto wao vitabu kwa hivyo imeweka Maktaba na vitabu vyote kwa akili wenye kuhitaji afike ili akakidhi mahitaji yake bila ya malipo na kupata usumbufu.
Maktaba hiyo imekuwa ikifanya uchambuzi wa vitabu mbali mbali kwa wanafunzi tayari wamevifanyia vitabu vingi ikiwemo Mwanayungi Hulewa, na Mzimu wa Watu wa Kale.
No comments:
Post a Comment