Habari za Punde

Rais Dk Mwinyi aviagiza vyomba vya ulinzi na usalama kufanya uchunguzi wa haraka kubaini chanzo cha ajali ya kuporomoka jengo la beit el Ajaib


 

               

                               STATE HOUSE ZANZIBAR

                       OFFICE OF THE PRESS SECRETARY

                                          PRESS RELEASE

 

Zanzibar                                                                         Disemba 26, 2020

 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi amevitaka vyombo vya Ulinzi na Usalama kufanya uchunguzi  wa haraka ili kubaini chanzo cha ajali ya kuporomoka  sehemu ya jengo la makumbusho la Taifa la Beit al Ajab  iliyotokea Disemba 25, mwaka huu.

 

Dk. Mwinyi ametoa agizo hilo leo, wakati alipofanya ziara ya kutembelea Hospitali ya Rufaa ya Mnazi Mmoja kwa lengo la kutoa  rambi rambi  kwa wafiwa pamoja na kuwapa pole majeruhi wa ajali hiyo.

 

Amevitaka vyombo hivyo kufanya uchunguzi wa kina na wa haraka ili kubaini chanzo cha tukio zima la kuporomoka sehemu ya jengo hilo na kuleta maafa kwa wananchi, ili Serikali iweze kuchukua hatua madhubuti na kwa haraka.

 

Alisema msiba uliotokea ni wa Taifa na hivyo akawapa pole wafiwa pamoja na kuwaombea dua majeruhi wa tukio hilo ili waweze kupona kwa haraka na kurudi katika shughuli  za ujenzi wa Taifa.

 

Aidha, amezitaka mamlaka mbali mbali, ikiwemo mji Mkongwe, Shirika la Nyumba pamoja na taasisi ya Wakfu na Mali ya Amana kufanya tathmin ya haraka ya majengo yote yalioko katika hali mbaya, ili yaweze kufungwa na tathmin hiyo iweze kuielekeza Serikali namna ya  kuyafanyia matengenezo ili kuepusha ajali kama hiyo.

 

Alisema Serikali itagharamia mazishi ya wananchi waliopoteza maisha kutokana na ajali hiyo, sambamba na kuchukua hatua nyingine ili kuhakikisha matukio ya aina hiyo  hayatokei tena.

Katika hatua  nyengine, Dk. Mwinyi alitembelea majeruhi wa jali hiyo waliolazwa hospitalini hapo pamoja na wagonjwa mbali mbali wanaohitaji matibabu  kutokana na sababu mbali mbali ikiwemo ajali.

 

Alieleza kuwa majeruhi waliopatwa na ajali ya kuangukiwa na sehemu ya jengo la Beit Al Ajaib wanahudumiwa vizuri na kusema Serikali itachukua hatua muhimu ili kuhakikisha changamoto ya upungufu wa vifaa pamoja na dawa inapatiwa ufumbuzi.

 

Rais Dk. Mwinyi aliwapongeza wafanyakazi wa Hospitali hiyo, wakiwemo madaktari na wauguzi kwa kazi kubwa na nzuri wanayofanya kuwahudumia wagonjwa na kuwataka kuongeza juhudi.

 

Kutokana na  tukio la kuporomoka sejemu ya jengo la Beit al Ajaib, wananchi Burhani Ali Makune (35) mkaazi wa Mtoni Kidatu pamoja na Pande Makame Haji (25) mkaazi wa Bumbwini walifariki dunia, wakati ambapo Hemed Mattar Abdalla (39), Dhamir Salum Dhamir (37) pamoja na Ali Ramadhan Juma (23) wanaendelea na matibabu Hospitalini hapo.

 

Katika ziara hiyo Dk. Mwinyi aliongozwa na Kaimu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Simai Mohamed Said, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii Halima Maulid Salum pamoja na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji Hospitali ya Rufaa Mnazimmoja Marijani   Msafiri Marijani.

 

Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 

 E-mail: abdya062@gmail.com

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.