Habari za Punde

DC MWILAPWA -MAZINGIRA NDIO UHAI WA TAIFA, AIPONGEZA TANGA UWASA KWA KUWEKA JUHUDI KWENYE UTUNZAJI WA MAZINGIRA

MKUU wa wilaya ya Tanga Thobias Mwilapwa akieleza jambo kuhusu umuhimu wa wananchi kutunza mazingira wakati wa ziara ya kukagua shughuli za uhifadhi wa vyanzo vya maji zinazofanywa na uwamakizi  wilayani Muheza kwa ufadhili wa Tanga Uwasa
Afisa Miradi kutoka Tanga Uwasa Ramadhani Nyambuka kushoto akieleza jambo wakati wa ziara hiyo

Na.Assenga Oscar - Tanga.

MKUU wa wilaya ya Tanga Thobias Mwilapwa amesema mazingira ndio uhai wa Taifa na bila mazingira hakuna chochote kinaweza kufanyika hivyo jamii haina budi kuhakikisha wanayatunza na kuyalinda kwa ajili ya vizazi vya sasa na vijavyo.

DC Mwilapwa aliyasema hayo wakati wa ziara ya kukagua shughuli za uhifadhi wa vyanzo vya maji zinazofanywa na uwamakizi Amani wilayani kwa ufadhili wa Tanga Uwasa ikiwa ni wiki ya mazingira ambapo vijiji 18 vipo katika utunzaji wa vyanzo vya Maji na Mazingira katika wilaya Muheza

Alisema kwa sababu bila mazingira hakuna jambo lolote ambalo linaweza kufanyika hivyo ni muhimu kwa jamii kuhakikisha wanaachana na vitendo vya kuharibu mazingira kwenye maeneo yao badala yake washirikiane kuyalinda.

“Kwanza nipongeze ubunifu huu uliofanywa na Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira (Tanga Uwasa) kwa kushirikiana na jamii inayoishi kwenye vyanzo vya maji kuwapa elimu ya ya utunzaji wa mazingira na hivyo kupelekea kuwa mabalozi wazuri katika kutunza mazingira”Alisema

Mkuu huyo wa wilaya alisema jambo kubwa ni jamii kubadilika katika maeneo mbalimbali kuhakikisha wanatunza mazingira kila mtu aweze kunufaika na uwepo wake na Tanga Uwasa wamefanya jitihada za kuondoa malalamiko ya Maji kutoka Muheza wanafaidika wengine kwani hivi sasa kila kijiji kinafaidika na uwepo wa vyanzo vya maji hivyo ni muhimu kutunza mazingira maji yapatikane kwa kila mtu na sasa vijiji vitatu vimeanza kupata maji.

Alisema sehemu kubwa ya maisha ya binadamu yanahitaji maji na asilimia 75 ya mwili wa binadamu ni maji na hata kwenye vitabu vitakatifu vimeandikwa hata roho ya Mungu ilikua imetulia kwenye vilindi vya maji kwa hiyo dhana ya maji ni kubwa katika uhai hivyo tuhakikisha tunatunza mazingira yatupatie maji.

Awali akizungumza wakati wa  ziara hiyo ,Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Tanga Uwasa Mhandisi Rashid Shaban amesema  katika wiki ya Mazingira wameamua kutembelea jamii inayotunza mazingira na kulinda vyanzo vya maji ili kuendelea kuhamamsisha umuhimu wa kulinda vyanzo vya maji.

Alisema wao wafanya kazi za utoaji wa huduma za maji katika wilaya ya Tanga, Muheza na Pangani lakini chanzo cha Maji ni mto zigi ambao unaanzia kwenye milima ya Amani ambapo mito imeanzia hivyo wakalazimika kwenda na Mkuu wa wilaya ya Tanga kumuonesha jitihada za Tanga Uwasa ambazo wanazifanya katika vyanzo vya maji.

“Tunachokifanya ni kuwawezesha wananchi wale wanaoishi kandokando ya vyanzo vya maji wafanye shughuli zingine ambazo haziathiri uharibifu wa mazingira ambazo zinaathiri vyanzo vya maji na hivyo kujiingizia kipato na kuendesha maisha yao”Alisema

Mhandisi Shabani alisema kupitia wadau ambao ni wananchi waliopo vijijini shughuli zao nyingi zinahusisha kilimo, kukata miti ambayo sio rafiki kwa mazingira wameona washirikiane nao kuwawezesha kufanya shughuli zingine mbadala kuliko kufanya shughuli zinazoathiri vyanzo vya maji.

Alisema madhara makubwa yanayotokana na uharibifu wa mazingira ni pamoja na ardhi kuwa wazi na wa wale wanaolima mvua zikinyesha zinabeba udongo hupelekwa mtoni na kusababisha udongo kujaa kwenye bwawa na hivyo kusababisha gharama kubwa kwa mamlaka ili kununua dawa.

"Kwani uharibifu huo unapelekea kazi ya kusafisha maji ni mwananchi ndio atakae umia kwa kuwa ni lazima bei ya maji itapanda kwani tunasafisha maji kuondoa vumbi na kemikali itabidi Mamlaka iingie gharama kununua dawa"Alisema

Hata hivyo Afisa Miradi kutoka Tanga Uwasa Ramadhani Nyambuka alisema mambo wanayoyafanya katika uhifadhi wa ardhi ni kuhakikisha tope haliendi mtoni kwa kutumia ubunifu wa kilimo cha matuta.

"Huku tunafanya kilimo cha matuta kwa kutunza ardhi ambapo inapunguza kasi ya maji yanapotoka juu milimani kuzuia kuepusha mmomonyoko na hivyo maji yanakuja taratibu yanafika sehemu yanatuama yanaenda hatua nyingine inafanya udongo ujitenge na maji safi yanaenda mtoni"Alisema Nyambuka.

Alisema mradi huo wa utunzaji wa mazingira ulianza tokea mwaka 2013 ambapo elimu ilianza katika vijiji vitano ambavyo vilikuwa na jumla ya wanachama 473 ambao waliunda kikundi cha Uwamakizi

Alisema kati ya vijiji hivyo 18 ni vijiji vitatu ndio vimeanza kupata huduma ya maji kwasasa ambavyo ni Kimbo, Shembeleza na Mashewa.

Nyambuka alisema muungano huo haukuwa rahisi kwa wananchi kuelewa Tanga Uwasa inahitaji nini katika utunzaji wa mazingira lakini kadiri walivyokuwa wakitoa elimu kwa wananchi kila kijiji ili kuelimisha umuhimu wa utunzaji wa mazingira waalianza kueleza na kuanza kufanya kilimo kisichoathiri vyanzo vya maji ili kuendelea kulinda vyanzo vya Maji.

“Katika kufanikisha malengo ya utunzaji wa Mazingira na vyanzo vya Maji,Tanga Uwasa tumefanikiwa kutumia vikundi vya hamasa  kilianzishwa na wananchi wenyewe wa kwa kuanzisha UWAMAKIZI na kuanza kuzunguka vijiji vyote vyenye vyanzo vya maji na kuanza kutoa elimu,hamasa na mpaka sasa vijiji vinavyojihusisha na utunzaji wa mazingira imefika 18 na vikiwa na wanachama 1540 “Alisema

Hata hivyo Mwenyekiti wa kikundi cha Umakizi,Twaha Rajabu amesema jamii inayozunguka vyanzo vya maji walikua wanakawaida ya kufanya shughuli za kibinadamu ambazo sio rafiki,ufanyaji kazi huo ulisababisha uchafuzi wa vyanzo vya maji kuelekea bwawa la Mabayani ambayo ndio inalisha Tanga mjini

"Hivyo kutokana na shughuli za kibanadamu ambazo zilileta uharibifu,Mamlaka ya Maji Tanga Uwasa walianza na sisi uwamakizi ili kuepusha  na kunusuru uharibifu wa  vyanzo vya maji katika shughuli hizo tunatoa elimu kwa jamii kuacha kuchafua vyanzo vya maji,na wapande mazao ambayo ni rafiki kwa vyanzo vya maji kuacha mita 5 zisiguswe kabisa na mita 55 kupanda miti ambayo inakua rafiki kwa mazingira ambayo ni Kakao na Pilipili Manta" alisema Rajab

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.