Habari za Punde

Rais Dk Hussein Mwinyi awashukuru viongozi wa dini kwa kushirikiana na serikali kuhamasisha amani na utulivu nchini


 

STATE HOUSE ZANZIBAR

OFFICE OF THE PRESS SECRETARY

PRESS RELEASE

 Zanzibar                                                                                               09.06.2021

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi ametoa shukurani kwa viongozi wa dini kwa kushirikiana na Serikali ya Awamu ya Nane katika kuhamasisha amani na utulivu hapa nchini.

 

Dk. Mwinyi ameyasema hayo leo Ikulu Jijini Zanzibar wakati alipofanya mazungumzo na viongozi mbali mbali wa dini wakiwemo viongozi wa Dini ya Kiislamu chini ya Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Saleh Omar Kabih na viongozi wa dini ya Kikristo wakiongozwa na Askofu Dickson Kaganga Katibu wa Umoja wa Dini mbali mbali  hapa Zanzibar.

 

Katika maelezo yake Rais Dk. Mwinyi alieleza kuwa utayari wa viongozi hao wa kushirikiana na Serikali ili nchi iendelee kuwa ya amani na utulivu unatoa mwanga mkubwa katika kuijenga nchi.

 

Aliongeza kwamba viongozi wa dini na Serikali wanapaswa kuwa kitu kimoja katika kuendeleza na kuhamarisha masuala ya kijamii, kiuchumi na kimaendeleo.

 

Aidha, Rais Dk. Mwinyi alitumia fursa hiyo kuwapongeza viongozi  hao wa dini kwa kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuijenga amani sambamba na kuondosha ubaguzi hatua ambayo itaiimarisha  nchi na kuiletea maendeleo endelevu.

 

Alieleza kwamba Serikali ya Awamu ya Nane imechukua juhudi za makusidi katika kuhakikisha aina zote za ubaguzi zinaondoka hatua ambayo imeweza kuleta mafanikio makubwa hivi sasa hapa nchini.

 

Rais Dk. Mwinyi alieleza haja kwa viongozi hao kwa pamoja kubeba ajenda ya uchumi wa Zanzibar hivi sasa ambao ni uchumi wa Buluu ili kuweza kufikia malengo yaliyokusudiwa sambamba na kuielewesha jamii juu ya dhana hiyo.

 

Aliongeza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Nane imedhamiria kuja na ajenda ya uchumi wa Buluu kwa kuona kwamba Zanzibar imezungukwa na bahari na kuwa na rasilimali nyingi huku ikizingatiwa kwamba ardhi iliyopo haitoshi.

 

Katika maelezo yake Rais Dk. Mwinyi alifahamisha haja ya kutoa elimu juu ya uchumi wa Buluu ili jamii iweze kuuelewa ipasavyo sambamba na malengo yake na kuwataka viongozi hao kutoa elimu kwa jamii juu ya sekta hiyo.

Rais Dk. Mwinyi katika maelezo yake aligusia changamoto iliyopo katika ukusanyaji wa kodi hapa Zanzibar hali ambayo inatokana na matatizo ya kimifumo hatua ambayo alisema inafanyiwa kazi ili kuhakikisha kila anaepaswa kulipa kodi analipa.

 

Pia, Rais Dk. Mwinyi aligusia suala zima la unyanyasaji wa kijinsia na kueleza jinsi hatua za makusudi zinavyochukuliwa katika kuhakikisha janga hilo linaodoshwa na kutoa shukurani kwa viongozi wa dini kwa mashirikiano wanayoyatoa kutokana na kadhia hiyo.

 

Rais Dk. Mwinyi alieleza jinsi Serikali pamoja na vyombo vyake ilivyoweka mikakati katika kuhakikisha janga hilo linapigwa vita.

 

Aidha, Rais Dk. Mwinyi alieleza azma ya Serikali katika kuliimarisha soko la ajira kwa kuitekeleza ipasavyo miradi yake ya maendeleo iliyoipanga ili kuhakikisha changamoto ya ajira inapatiwa ufumbuzi.

 

Mapema viongozi wa dini kwa upande wao walitumia fursa hiyo kumpongeza Rais Dk. Mwinyi kwa mwanzo mzuri alioanza nao katika kutekeleza azma yake ya kuwaletea maendeleo wananchi wote wa Zanzibar.

 

Viongozi hao walieleza jinsi walivyofarajika na hatua za makusudi anazozichukua Rais Dk. Mwinyi katika kuhamasisha amani, umoja na mshikamano huku wakisisitiza haja kwa viongozi wengine wa Serikali kufuata nyayo zake. 

 

Aidha, walieleza jinsi Serikali ya Awamu ya Nane chini ya uongozi wa Rais Dk. Mwinyi ulivyoweka mikakati ya kuimarisha uchumi wake katika kupitia uchumi wa Buluu huku wakiahidi kuendelea kumuunga mkono ili kuhakikisha maono yake yanatimia.

 

Sambamba na hayo, viongozi hao walieleza jinsi hatua za makusudi zilizochukuliwa na Rais Dk. Mwinyi mara tu baada ya kuingia madarakani za kuhakikisha anawaweka wananchi kuwa kitu kimoja na kuondosha ubaguzi wa aina zote.

 

Viongozi hao, walieleza matarajio makubwa waliyonayo wananchi wa Zanzibar kutokana na uongozi thabiti wa Dk. Mwinyi ambapo kwa muda mfupi aliyoongoza wameanza kupata mwanga wa matumaini sambamba na mabadiliko yaliyopo katika nyanja tofauti.

 

Walieleza na kusifu hotuba zake anazozitoa kwa wananchi katika hafla mbali ziwe za kidini ama kiserikali ambazo zimekuwa dira ya kutekeleza yale yote aliyokuwa akiyaahidi katika Kampeni zake za uchagauzi.

 

Pamoja na hayo, viongozi hao walieleza haja ya kuhakikisha wawekezaji wanawekewa mazingira mazuri ili waendelee kuja kuekeza hapa Zanzibar huku wakiahidi kwa upande wao kuwahamasisha wawekezaji wadogo wadogo nao waendelee kuekeza hapa nchini.

 

Viongozi hao walipata fursa ya kufanya mahojiano na waandishi wa habari na kueleza utayari wao wa kumuunga mkono Rais katika kuimarisha amani, umoja na mshikamano.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.