RAIS wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi, amesema Uchumi wa
Zanzibar umeathirika kutokana na janga la maradhi ya Corona na kueleza kuwa
imejipanga kikamilifu kukabiliana na ugonjwa huo.
Dk. Mwinyi amesema hayo Ikulu Jijini Zanzibar, alipozungumza na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Dunia, Kanda ya Afrika Dk. Taufila Nyamadizabo.
Amesema pamoja na kuwa suala la Afya kutokuwa la Muungano, Serikali inasubiri mapendekezo ya Kamati ya Kitaifa, ilioundwa hivi karibuni na Serikali ya Jamuhuri ya Muungano, ili kuona njia bora ya kukabiliana na ugonjwa huo.
Aliiomba Benki ya Dunia kuendelea kuisaidia Zanzibar kupitia nyanja mbali mbali, ili iweze kukuza uchumi wake.
Dk. Mwinyi alizitaja sekta za Uchumi wa Buluu pamoja na Utalii kuwa miongoni mwa sekta zilizo katika mipango ya Serikali ili kufanikisha azma ya kuinua uchumi wa Zanzibar.
Aidha, aliipongeza Benki ya Dunia (World Bank) kwa ushirikiano na misaada inayoipatia Zanzibar na kuiwezesha kufanisha miradi mbali mbali ya maendeleo.
Nae, Mkurugenzi Mtendaji Benki ya Dunia, Kanda Afrika Dk. Taufila Nyamadizabo, alisema Benki ya Dunia itaendeleza ushirikiano wake na Zanzibar, pamoja na kuzipatia misaada mbali mbali nchi wanachama.
Aliyataja maeneo ambayo Benki ya Dunia imeweka kipaumbele katika kuzisaidia nchi wanachama ikiwemo Zanzibar katika kipindi hiki, kuwa ni pamoja na kuwajengea uwezo watendaji, kuimarisha mifumo ya ajira pamoja na mifumo ya fedha.
Dk. Nyamadizabo alisema Benki ya Dunia itaendelea kufanyakazi kwa karibu na nchi wanachama katika masuala mbali mbali.
Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024
2231822
E-mail: abdya062@gmail.com
No comments:
Post a Comment