Habari za Punde

Kampuni ya Simu ya Zantel Yaboresha Miundombinu ya Mawasiliano Zanzibar.

Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi - Zanzibar, Mhe. Rahma Kassim Ali akikata utepe, wakati akizindua rasmi Minara nane za Mawasiliano jana, Alhamisi, katika kijiji cha Bumbwini Mafufu. Kulia kwake (aliyeshikilia utepe) ni Mkuu wa Zantel-Zanzibar, Mohammed Khamis Mussa.

Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi - Zanzibar, Mhe. Rahma Kassim Ali akimsikiliza Afisa Mkuu wa Teknolojia wa Kampuni ya Zantel, Lucas Nchimbi (aliyesimama katikati) wakati akizungumza kwenye uzinduzi wa Minara nane ya Mawasiliano jana, Alhamisi, katika kijiji cha Bumbwini Makoba. Kulia kwake ni Mkuu wa Zantel-Zanzibar, Bw Mohammed Khamis Mussa.


Katika jitihada za kuboresha huduma za mawasiliano visiwani Zanzibar, Kampuni ya Mawasiliano ya Zantel, imezindua minara nane ya mawasiliano katika maeneo mbalimbali yaliyokuwa na mtandao hafifu ili kuhakikisha wateja wanapata huduma bora.

Minara hiyo iliyopo katika vijiji vya Seacliff, Kisiwa Uzi, Bumbwini Mafufu, Kisiwani, Chambani, Makangale, Maziwa N’gombe na Jongowe imezinduliwa na Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi - Zanzibar, Rahma Kassim Ali.

Akizunguza wakati wa hafla ya uzinduzi, Mkuu wa Zantel-Zanzibar, Mohammed Khamis Mussa alisema lengo ni kuhakikisha Zanzibar yote inapata huduma bora na za uhakika za mawasiliano pamoja na mtandao wa intaneti.

“Zantel tumeendelea kuwa mstari wa mbele katika kuboresha huduma za mawasiliano hapa Visiwani Zanzibar.Leo tuna furaha kukamilisha minara hi inane mipya ambayo itasaidia katika kuongeza ufanisi wa huduma kwa wateja wetu,” alisema.

Aliongeza “Mbali na kusogeza huduma za kupiga simu kwa watu, dhamira ya Zantel kwa sasa ni kuendeleza matumizi ya intaneti na mfumo wa kidijitali katika masoko yetu.  Tunaendelea kuboresha mtandao wetu wa intaneti kutoka kasi ya 2G na 3G na kuweka mtandao wa 4G katika baadhi ya maeneo,” aliongeza.

Pia, aliishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, kupitia Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji pamoja Wakala wa Miundombinu ya Tehama (ZICTIA) kwa kushirikiana kwa karibu na kampuni ya Zantel  ambapo mpaka sasa zaidi ya asilimia 86 ya Zanzibar imeunganishwa na mtandao.

Kupitia ushirikiano na ZICTIA, Zantel imefanikisha kuunganisha zaidi ya minara 33 kwenye mkonga wa Mawasiliano (Fibre) kwa zaidi ya kilomita 28 ambayo imesaidia kuongeza ufanisi wa huduma.

Akizindua minara hiyo, Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi - Zanzibar, Rahma Kassim Ali aliipongeza Zantel kwa uwekezaji mkubwa ambao imeufanya katika kuboresha miundombinu ya mawasiliano kote Unguja na Pemba.

“Kampuni ya Zantel imekuwa karibu sana na serikali katika kutatua changamoto za mawasiliano zinazowakabili wanachi wetu wa Zanzibar, ninawapongeza sana kwa hili,” alisema.

Aliongeza “Mawasiliano ni muhimu sana katika upatikanaji wa taarifa sahihi zinazofika kwa wakati sahihi ili kufanya maamuzi ya kimaendeleo. Ndiyo maana serikali kupitia Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi  imekuwa ikifanya juhudi mbalimbali za Kujenga miundombinu madhubuti ya TEHAMA kama vile Mkonga wa Mawasiliano wa Taifa na vituo vya kutunzia taarifa (data centre) ambayo imesaidia kukuza mawasiliano nchini na kuhakikisha usalama wa mawasiliano.”

Alisema kuwa, kuimarika kwa huduma za mawasilaino kutachangia kukuza uchumi wa Bluu kwa kuimarisha upatikanaji wa taarifa za masoko katika sekta hiyo.

Aidha, Zantel imechukua hatua kadhaa katika kuelimisha wananchi juu ya umuhimu wa intaneti kupitia kampeni yake kabambe ya PASUA ANGA KI ZANTEL 4G ili wateja waweze kuelewa umuhimu wa mtandao na kuweza kunufaika na fursa mbalimbali za kiuchumi na kijamii.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.