Habari za Punde

Uhitaji wa Nyama Waongezeka na Yabainika Sekta Kukua.



Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (Mb), (aliyesimama) akifafanua jambo na kujibu maswali mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge, Kilimo, Mifugo na Maji wakati wa uwasilishaji wa taarifa ya utendaji kazi wa Bodi ya Nyama nchini jijini Dodoma, ambapo Mhe. Ulega amesema malalamiko yaliyojitokeza hivi karibuni ya kupanda kwa bei ya nyama nchini yanaashiria ukuaji wa sekta hiyo ambapo wafugaji wameshauriwa kuwa huu ni muda mzuri kwa wao kuvuna na kuuza mifugo yao. 
Msajili wa Bodi ya Nyama nchini Dkt. Daniel Mushi (aliyesimama) akiwasilisha taarifa ya utendaji kazi wa bodi hiyo mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge, Kilimo, Mifugo na Maji jijini Dodoma na kufafanua kuwa sera ya serikali kwa sasa ni uwepo wa vikundi kwa ajili ya kunenepesha mifugo na kupata mifugo bora inayoendana na mahitaji ya soko la sasa na kwamba hivi karibuni Tanzania itaanza kuuza nyama nchini Saudia Arabia ambapo uhitaji wao ni Tani Laki Sita kwa mwaka. (Picha na Edward Kondela, Afisa Habari - Wizara ya Mifugo na Uvuvi).

Na. Edward Kondela

Serikali imesema malalamiko yaliyojitokeza hivi karibuni ya kupanda kwa bei ya nyama nchini yanaashiria ukuaji wa sekta hiyo ambapo wafugaji wameshauriwa kuwa huu ni muda mzuri kwa wao kuvuna na kuuza mifugo yao.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (Mb) amebainisha hayo leo (20.10.2021) jijini Dodoma, mbele ya wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge, Kilimo, Mifugo na Maji wakati wa uwasilishaji wa taarifa ya utendaji kazi wa Bodi ya Nyama nchini mbele ya kamati hiyo.

Mhe. Ulega amesema kipindi cha nyuma wafugaji walikuwa wakilalamika kutopata masoko ya mifugo yao ila katika kipindi cha sasa uhitaji wa mifugo katika viwanda vya kuchakata nyama nchini umekuwa mkubwa pamoja na hitaji la nyama katika soko la ndani.

“Sekta ambayo ulikuwa hauwezi kuisikia inasemwa, lakini leo inakuwa mjadala hivyo ni wakati mzuri sana kwa wafugaji kuvuna na kuuza mifugo yao.” Amesema Mhe. Ulega

Amesema serikali inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan imetengeneza uhitaji wa nyama baada ya kufungua biashara ya kuuza nyama nje ya nchi hivyo uhitaji wa mifugo kwenye viwanda vya kuchakata hapa nchini umeongezeka.

Kwa upande wake Msajili wa Bodi ya Nyama nchini Dkt. Daniel Mushi ameiambia kamati hiyo kuwa uhaba wa nyama uliojitokeza hivi karibuni na kusababisha bei ya nyama kupanda ni fursa ya kufuga kibiashara na kunenepesha mifugo hiyo

Amesema kwa sasa sera ya serikali ni kuhamasisha uwepo wa vikundi kwa ajili ya unenepeshaji wa mifugo ili kupatikana kwa mifugo bora kulingana na hitaji la soko la sasa hususan kwenye viwanda vya kuchakata nyama nchini.

Ameongeza kuwa hivi karibuni Tanzania kupitia viwanda vilivyopo nchini itaanza kupeleka nyama katika soko la Saudi Arabia na kwamba hitaji la soko hilo ni Tani Laki Sita kwa mwaka hali ambayo itachangia kwa kiasi kikubwa kukuza sekta ya mifugo nchini.

Kuhusu ugonjwa wa midomo na miguu (FMD) ambao unaathiri mifugo na kusababisha Tanzania kushindwa kupeleka nyama katika baadhi ya nchi za nje kulingana na masharti yaliyopo kwenye nchi hizo, akimwakilisha Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo, Msajili wa Baraza la Veterinari Tanzania (RVCT) Dkt. Bedan Masuruli amesema ugonjwa huo umekuwa ukiathiri kwa kiasi kikubwa biashara ya nje na kwamba umekuwa ukisababishwa na uwepo wa wanyama pori.

Amesema ni vigumu kudhibiti ugonjwa huo kwa kuwa Tanzania ina kirusi cha ugonjwa huo ambacho hakipo kwenye chanjo ambazo zinaingizwa nchini kutoka nchi za nje kwa ajili ya kudhibiti ugonjwa huo na kwamba kuna virusi aina saba vya ugonjwa huo.

Amefafanua baadhi ya viwanda ambavyo vimepewa vibali vya kusafirisha nyama kwenda ya nchi vinataratibu ya kuweka mifugo karantini kabla ya kuchinjwa ili kujiridhisha mifugo hiyo kutokuwa na ugonjwa wa midomo na miguu ambao hauathiri binadamu.

Akizungumza wakati akihitimisha kikao cha Kamati ya Kudumu ya Bunge, Kilimo, Mifugo na Maji Mwenyekiti wa kamati hiyo Mhe. Dkt. Christine Ishengoma baada ya kamati kusomewa taarifa ya utendaji kazi wa Bodi ya Nyama nchini, ameishauri Wizara ya Mifugo na Uvuvi kuendelea kuisimamia vyema sekta ya mifugo ili iweze kuongeza mapato kwa kuuza mifugo na mazao yake ndani na nje ya nchi.

Pia, amesema ni vyema elimu iendelee kutolewa kwa ajili ya uzalishaji wenye tija kwenye masoko na uvunaji wa mifugo kusudi uzalishaji uwe wenye tija na kwamba mifugo ipo mingi wafugaji hawapaswi kutokuvuna mifugo yao hali ambayo inasababisha pia viwanda vya kuchakata nyama kutopata malighafi ya kutosha.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.