RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Hussein Ali Mwinyi amesema kuwa matukio mbali mbali yakiwemo kushuka kwa
kiwango cha hali ya usalama husababisha kuporomoka kwa utalii. Rais Dk. Mwinyi
aliyasema hayo leo katika uzinduzi wa
Kikosi cha Polisi wa Utalii na Diplomasia, hafla iliyofanyika katika ukumbi wa
Sheikh Idriss Abdulwakil, Kikwajuni Jijini Zanzibar.
Katika hotuba
yake Rais Dk. Mwinyi alisema kuwa baadhi ya nchi zimepoteza watalii baada ya
kushuka kwa kiwango cha hali ya usalama pamoja na mambo mengineyo yakiwemo kutokea
kwa machafuko ya kisiasa, vita vya wenyewe kwa wenyewe, miripuko ya maradhi na
majanga.
Alisema kuwa uchumi
wa Zanzibar ulitetereka kwa kiwango kikubwa kutokana na kuibuka kwa janga la
maradhi ya UVIKO 19 ambapo hili ni janga la Kimataifa lakini pia, ziko nchi
kadhaa duniani ambazo zimepoteza watalii kutokana na matukio ya ndani ya nchi
zao.
Rais Dk. Mwinyi
alieleza kwamba uanzishwaji wa Kikosi cha Polisi wa Utalii kwa madhumuni ya
kulinda na kuimarisha usalama wa watalii ni hatua muhimu na inayoendana na
dhamira ya kuhakikisha watalii na wageni wanaoitembelea Zanzibar wako salama na
wakirejea kwao wanakuwa mabalozi wazuri wa kuitangaza kwa mambo mazuri.
Hivyo, alitumia
fusra hiyo kwa kuwataka viongozi watakaopewa dhamana ya kuongoza Kikosi hicho wajifunze
kutokana na mafanikio na changamoto zilizojitokeza katika utekelezaji wa
majukumu ya Kikosi kilichofanana na hicho kilichokuwepo hapo awali.
“Imani yangu ni
kwamba, Askari watakaoteuliwa katika kikosi hiki wataendelea kutekeleza
majukumu yao kwa kuzingatia maadili ya kazi ya uaskari ipasavyo, wakijuwa kwamba
wao wakichafua basi itakuwa ni vigumu kwa watalii kuiamini taasisi nyengine
ikiwa wale waliopewa majukumu ndio wanaharibu”,alisema Rais Dk. Mwinyi.
Aidha,
aliwanasihi wananchi wa Mikoa, Wilaya na Shehia zote za Unguja na Pemba
kushirikiana na askari hao ili kuhakikisha wageni wanaoitembelea Zanzibar
pamoja na wananchi wote wanaishi katika mazingira yaliyo salama na yenye amani
na utulivu.
Dk. Mwinyi
aliwataka wadau wa Utalii kushirikiana na kufanya kazi kwa pamoja na Serikali
katika kuiendeleza sekta ya utalii ili kuinua uchumi, kukuza ajira, kutoa
huduma bora na kuimarisha mitaji na faida kwa wawekezaji waliojitolea kuja
kuwekeza nchini.
Alisisitiza
kutafutwa njia na mbinu za pamoja za kuyaunganisha makundi ya wajasiriamali na
sekta ya utalii ili kuwasaidia kupata masoko ya bidhaa wanazozalisha na huduma
zanazotoa ili wajasiriamali hao wadgo wadogo na wao wafaidike na utalii.
Sambamba na
hayo, Rais Dk. Mwinyi aliyataja mambo ambayo bado hayajafanywa vizuri ikiwa ni
pamoja na utoaji wa huduma kwa wageni hasa katika viwanja vya ndege na
bandarini pamoja na utoaji wa huduma za upimaji wa maradhi ya UVIKO 19.
Alisema kwamba
bado hajaridhishwa na msongamano na foleni ndefu katika madeski ya kutolea
viza, malipo ya benki, ukaguzi wa mizigo, utoaji huduma kwa wateja na ucheleweshwaji
unaosababishwa na uzembe wa watendaji katika viwanja vya ndege.
Nae Waziri wa
Utalii na Mambo ya Kale Lela Muhamed Mussa alisema kuwa kikosi hicho kipya cha
Polisi wa Utalii, maandalizi yake yalianza mwezi wa Aprili mwaka huu 2021 kwa
Wizara ya Utalii na Mambo ya Kake kushirikiana na Wizara ya Nchi Afisi ya Rais
Tawala za Mikoa na Vikosi vya SMZ pamoja na Jeshi la Polsi kwa kuunda Kamati
maalum ya kuratibu uanzishwaji wa kikosi hicho.
Aliitaja Jumuiya
ya Watembeza Wageni Tanzania (TATO) pamoja na Kikosi cha Polisi Utalii cha
Diplomasia Arusha ambapo taasisi hizo
zimeweza kusaidia kwa kiasi kikubwa katika kutoa uzoefu wa jinsi gani
wamefanikiwa katika kukabiliana na uhalifu kwa upande wa Tanzania bara hasa
Mkoa wa Arusha ambako wageni wengi hutembelea.
Waziri Lela alisema
kuwa gharama yote inayohitajika katika kuwekeza kwenye Kikosi hicho ni Bilioni
8 ambapo gharama za operesheni za kila siku ni takriban milioni 500 kwa mwaka hivyo,
alizitaka sekta binafsi na wadau wa maendeleo kuunga mkono juhudi hizo za
Serikali ya Awamu ya Nane za Kupambana na Uhalifu kwa wageni.
Mapema, akisoma
risala kwa niaba ya Kamishna wa Jeshi la Polisi Zanzibar, Kamishna Msadiizi wa
Jeshi la Polisi (ACP) Eugene Emanuel alisema kuwa Kikosi hicho cha Polisi
Utalii kilichozinduliwa hivi leo kitakuwa na askari wasiopungua 150 kutoka kikosi
cha Polisi, Uhamiaji, JKU, KMKM, KVZ,KZU na Chuo cha Mafunzo Zanzibar.
Alisema kuwa
askari hao watagawanywa katika Mikoa yote mitano ya Zanzibar ambapo kila Mkoa
utakuwa na Kituo kikubwa cha Utalii chenye askazi 30 na kufuatiwa na vituo
vidogo vitakavyojengwa katika maeneo yanayotembelewa zaidi na watalii.
Alieleza kwamba
kwa upande wa Unguja vituo hivyo vitajengwa huko Nungwi, Kendwa, Kiwengwa,
Matemwe na Pwanimchangani Mkoa wa Kaskazini Unguja na Mkoa wa Kusini ni Chwaka,
Uroa, Jambiani, Paje, Michamvi na Kizimkazi na kwa upande wa Mjini Magharibi vitajengwa
huko Forodhani, Mtoni, Fumba, Uwanja wa Ndege na Chukwani na kwa upande wa
Pemba vitajenwga Chakechake na Makangale.
Katika hafla
hiyo, Rais Dk. Mwinyi pia, alikabidhi vyeti maalum vya shukurani kwa Wakufunzi wa
kikosi hicho pamoja na kuwakabidhi Wakuu wa Vikosi Maalum vya SMZ Vitambulisho
vya Polisi wa Utalii na Diplomasia ambapo mapema akiwasili katika eneo hilo alianza
kwa kupokea Gwaride Maalum la Kikosi cha Polisi wa Utalii.
Imetayarishwa na kitengo cha Habari
Ikulu Zanzibar
No comments:
Post a Comment