Habari za Punde

Rais Dk. Mwinyi afanya mazungumzo na Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Nape Moses Nnauye Ikulu Zanzibar

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na Uongozi wa Wizara ya Habari,Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Tanzania ukiongozwa na Waziri wa wizara hiyo Mhe.Nape Moses Mnauye, (kulia kwa Rais) alipofika Ikulu Jijini Zanzibar kwa mazungumzo na kujitambulisha mazungumzo yaliofanyika katika ukumbi wa Ikulu.(Picha na Ikulu)
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akimsikiliza Waziri wa Habari,Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Tanzania Mhe. Nape Moses Nnauye, alipofika Ikulu Zanzibar kwa mazungumzo na kujitambulisha na Ujumbe wake, mazungumzo hayo yaliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar.(Picha na Ikulu)
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na Ujumbe wa Wizara ya Habari,Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Tanzania  ukiongozwa na Waziri wa wizara hiyo Mhe.Nape Moses Mnauye.(kulia kwa Rais) na (kushoto kwa Rais ) Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Mhandisi Zena Ahmed Said.(Picha na Ikulu)
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na Waziri wa Habari,Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Tanzania Mhe.Nape Moses Nnauye, baada ya kumaliza mazungumzo yao alipofika Ikulu Jijini Zanzibar kwa mazungumzo na kujitambulisha leo 20-1-2022.(Picha na Ikulu) 

STATE HOUSE ZANZIBAR

OFFICE OF THE PRESS SECRETARY

PRESS RELEASE

Zanzibar                                                                                       20.01.2022

---

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi ameeleza matumaini yake makubwa katika kuimarisha  mashirikiano kati ya pande mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwa ni pamoja na kukuza sekta ya mawasiliano.

 

Rais Dk. Mwinyi aliyasema hayo leo wakati alipofanya mazungumzo na Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Nape Moses Nnauye Ikulu Zanzibar akiwa amefuatana na ujumbe wake.

 

Katika mazungumzo hayo Rais Dk. Mwinyi alimpongeza Waziri Nape kwa kupata wadhifa huo na kuahaidi kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendeleza ushirikiano uliopo ili kuweza kufanikisha kuwapatia wananchi wote mawasiliano sambamba na kushirikiana katika nyanja nyengine muhimu zilizokuwemo katika Wizara hiyo ili pande mbili hizo ziweze kwenda kwa pamoja katika maendeleo.

 

Alieleza kwamba kuweko kwa mradi wa kusambaza minara ambao itawekwa minara ipatayo 42 katika Shehia zipatazo 38 Unguja na Pemba kutasaidia kwa kiasi kikubwa kuweza kuwapatia mawasiliano bora wananchi, mradi utakao simamiwa na Mfuko wa Mawasilano kwa wote (UCSAF) ulioanzishwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

 

Nae Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Nape Moses Nnauye kwa upande wake aliahidi kutekeleza majukumu yake ipasavyo na kueleza kwamba ushirikiano uliopo kati ya Mfuko wa Mawasiliano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni mzuri.

 

Alisema kwamba mradi huo utafanyika kwa kiasi ya TZS Bilioni 6.9, ambao pia, umezingatia Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), pamoja na maelekezo aliyoyatoa katika ziara zake alizozifanya katika mikoa ya Zanzibar ambapo iligundulika kwamba kuna baadhi ya maeneo katika visiwa vya Unguja na Pemba hawapati mawasiliano bora ya simu.

 

Sambamba na hayo, Waziri Nape alimuhakikishia Rais Dk. Mwinyi kwamba Wizara anayoiongoza itatoa mashirikiano ya kutosha hasa kwa kutambua kwamba ni Wizara ya Muungano.

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.