Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na
Mazingira) Mhe. Khamis Hamza Khamis akiwa katika ziara ya kikazoi ya kukagua
uzingatiaji wa sheria ya mazingira katika kiwanda cha mafuta ya alizeti cha
Pyxus kilichopo eneo la Kizota jijini Dodoma leo Juni 18, 2022.
Wamiliki wa viwanda watakiwa kutenga fungu la kusaidia
utunzaji mazingira
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na
Mazingira) Mhe. Khamis Hamza Khamis ametoa rai kwa wamiliki wa viwanda nchini
kutenga fungu kwa ajili ya shughuli za kimazingira.
Ametoa rai hiyo leo Juni 18, 2022 alipofanya ziara ya
kikazi ya kujionea uzingatiaji wa sheria ya mazingira katika kiwanda cha
kuzalisha mafuta ya alizeti cha Pyxus kilichopo eneo la Kizota jijini Dodoma.
Mhe. Khamis alisema kuwa mataifa mbalimbali
yaliyoendelea hutoa fedha kwa nchi zinazoendelea kwa kutambua kuwa wao ndio
chanzo cha uharibifu wa mazingira kutokana na hewa ya ukaa wanayozalisha.
Alisema viwanda havina budi kuchangia shughuli za
mazingira na za kijamii kwa ujumla zikiwemo upandaji miti, utoaji elimu kuhusu
uhifadhi na utunzaji wa mazingira.
“Nawapongeza kiwanda hiki cha Pyxus nimesiki mnafanya
shughuli za kupanda miti katika eneo lenu hivyo natoa wito kwa viwanda vingine
nchini viwe na utaratibu huu ili tuhakikishe tunatunza mazingira,” alisema.
Aidha, naibu waziri huyo aliagiza wamiliki wa viwanda
vyote nchini viwe na mfumo mzuri wa kutibu na kudhibiti majitaka ili
kuhakikisha hayatiririki na kumwagika kwenye makazi ya watu hali inayoweza
kuhatarisha afya na mazingira.
Sambamba na hilo pia alielekeza viwanda vidhibiti moshi unaotokana
na shughuli za viwandani usisambae katika makazi ya watu hali inayoweza
kuwasababishia matatizo ya kiafya. Alielekeza pia viwanda vidhibiti kelele
zinazotokana na mashine za viwandani zisiwe kero kwa wananchi kwani zinaweza
kuwasbabishia matatizo ya masikio.
Kwa upande wake Meneja Rasilimaliwatu wa kiwanda cha
Pyxus Bw. Gideon Mutta alisema uongozi wa kiwanda hicho umepokea maelekezo hayo
na kuahidi yatashughulikwa.
Hata hivyo, alisema wana changamoto ya miundombinu ya mfumo
wa majitaka ambapo kutokana na hali hiyo aliomba Mamlaka ya Majisafi na Usafi
wa Mazingira Mjini Dodoma (DUWASA) kuwasaidia na kuona namna ya kuwaungasnishai
na mfumo wa Jiji la Dodoma.
No comments:
Post a Comment