RAIS wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi amesema ana
matumaini makubwa kuwa mabadiliko ya Sheria ya Makadhi yanayofanyika yataondoa
utata pamoja na migongano ya kiutendaji katika mhimili wa Mahakama hapa nchini.
Dk. Mwinyi amesema hayo Ikulu Zanzibar, alipozungumza na Kamati ya Sheria mpya ya Makadhi na kupokea taarifa ya mwelekeo wa Rasimu hiyo inayoongozwa na Mwenyekiti Wakili Mwandamizi wa Serikali Saleh Mbaraka.
Amesema kutokana na dhamira njema iliopo, ana imani kubwa kuwa sheria ijayo ya Makadhi itakuwa nzuri, yenye tija, isiyo na mivutano na yenye mwelekeo wa kujenga.
Alisema pale rasimu hiyo itakapofikishwa katika ngazi ya Baraza la Mapinduzi, wajumbe wa Baraza hilo watapata fursa ya kuipitia, sambamba na Kamati ya sheria ya Baraza hilo kushauri juu ya vipengele vinavyofaa kuingizwa au kupunguzwa.
Dk. Mwinyi aliwashukuru wajumbe wa Kamati hiyo kwa dhamira ya kuja na sheria mpya ya Makadhi kutokana na mahitaji yaliopo, akibainisha hatua ya kuwashirikisha wadau itawezesha kupata mchango wa maoni ya kutosha.
Nae, Jaji Mkuu wa Zanzibar Khamis Ramadhan Abdalla pamoja na mambo mengine alisema kuongoza mhimili wa Mahakama, ambamo ndani yake kuna Kadhi mkuu, kunahitajika busara kubwa.
Mapema, Mwenyekiti wa Kamati ya Sheria mpya ya Makadhi Wakili Mwandamizi Saleh Mbaraka, alisema lengo la sheria hiyo ni kuongeza wigo wa kutafuta haki ndani ya Mahakama za Kadhi pamoja na kuleta uharaka katika maamuzi ya kesi.
Alisema sheria hiyo inalenga kurejesha dhana ya kuwatambua masheikh wabobezi , pamoja na kuwa na utaratibu wa kuweka Hati mbali mbali na kuweza kutumika katika Mahakama mbali mbali Duniani.
Aidha, alisema itatoa msukumo katika hati mbali mbali (ikiwemo za ndoa) kuweza kukubalika katika mataifa mbali mbali.
Wakili Mbaraka alieleza kuwa kwa kipindi kirefu Serikali imekuwa ikipoteza fedha nyingi katika kuwasomesha Masheikh katika nchi mbali mbali Duniani ikiwemo Saud Arabia, kupitia fedha za Serikali au za wahisani, lakini matokeo yake pale masheikh hao wanaporerjea nchini huachwa bila kutumika.
Alisema kupitia sheria hiyo Masheikh hao watatambuliwa ili waweze kutoa mchango wao na kubainisha hatua hiyo itatoa ajira kwao.
Imetayarishwa na Idara ya Mawasiliano
Ikulu Zanzibar.
No comments:
Post a Comment