Habari za Punde

Balozi Sokoine Asisitiza Umuhimu wa Kumaliza Changamoto za Kibiashara Kati ya Tanzania na Zambia

 

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Joseph Sokoine akihutubia katika hafla ya ufunguzi wa Mkutano wa Kumi wa Tume ya Pamoja ya Kudumu ya Ushirikiano (JPC) kati ya Tanzania na Zambia unaofanyika kuanzia tarehe 11 hadi 14 Oktoba 2022 jijini Lusaka, Zambia. Pembeni yake ni Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Uwekezaji, Biashara na Viwanda, Bw. Ally Gugu.

Tanzania na Zambia zimedhamiria kumaliza changamoto za kibiashara na usafirishaji zinazowakabili wafanyabiashara ili kuruhusu biashara na usafirishaji wa bidhaa ufanyike bila vikwazo baina ya nchi hizo.

Hayo yamebainishwa katika hotuba ya ufunguzi iliyosomwa na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Joseph Sokoine wakati wa Mkutano wa Tume ya Kudumu ya Pamoja ya Ushirikiano (JPC) kati ya Tanzania na Zambia ngazi ya Wataalam unaofanyika leo tarehe 12 Oktoba 2022 jijini Lusaka Zambia.

Balozi Sokoine aliwasisitiza watendaji kutumia  mkutano huo kuandaa mikakati ya pamoja itakayosaidia kuondoa vikwazo vya kibiashara na kutengeneza mazingira wezeshi kwa sekta ya umma na binafsi ili ziweze kufanya uwekezaji utakaoleta maendeleo endelevu kwa ajili ya maslahi mapana ya kiuchumi kwa pande zote mbili.

“Tanzania ina dhamira ya dhati ya kuimarisha ushirikiano wake wa kindugu na kihistoria na Zambia ili kuendeleza jitihada zilizoasisiwa na waasisi wa mataifa yetu kwa kuweka mfumo rasmi wa ushirikiano unaowezesha ufuatiliaji wa utekelezaji katika masuala ya ushirikiano” alisema Balozi Sokoine.

Aidha, alieleza kuwa ushirikiano imara na wenye mafanikio ni ule unaojengwa kwa mfumo rasmi ambao unaruhusu kukutana na kufanya majadiliano ya mara kwa mara hivyo, alieleza kuwa ana amini kupitia mkutano huu maeneo yote ya ushirikiano yenye changamoto yatajadiliwa kwa kina kwa maslahi ya nchi zote mbili na wananchi wake.

Naye Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Zambia, Bw. Chembo Mbula alieleza kuwa ni muhimu majadiliano yakaangalia kwa kina maeneo muhimu yatakayowezesha pande zote mbili kuwa na mchango katika maendeleo ya mtangamano wa kikanda.

“Nchi zetu zimepiga hatua kiuchumi na katika maendeleo ya jamii tangu kumalizika kwa mkutano wa tisa wa Tume ya Pamoja ya Kudumu ya ushirikiano baina yetu, hivyo ni vyema majadiliano yakaendana na uhalisia wa mabadilika hayo” alisema, Bw. Mbula.

Pamoja na mambo mengine mkutano huu utapitia na kujadili utekelezaji wa maazimio ya Mkutano wa Tisa wa Tume ya Kudumu ya pamoja ya ushirikiano kati ya Tanzania na Zambia uliofanyika tarehe 25 na 26 Februari 2016 jijini Dar es Salaam.

Mkutano huo ulioanza tarehe 11 Oktoba 2022 kwa ngazi ya Wataalam, utafuatiwa mkutano wa Makatibu Wakuu na utahitimishwa kwa  mkutano wa ngazi ya Mawaziri utakaofanyika tarehe 14 Oktoba 2022 jijini humo.

-Mwisho-

 

Imetolewa na:

Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.