Habari za Punde

Jumuiya ya Good People Hope Box yatoa msaada kwa watu wenye mazingira magumu Kidimni

 


Katibu  Mkuu wa Wizara ya Maendeleo  ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto bi Abeida  Rashid  Abdallah amesema Wizara itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo katika kusaidia maendeleo ya jamii hasa wenye mazingira magumu na wasiojiweza ili kuwapunguzia ukali wa maisha.

Akizungumza baada ya kuwakabidhi  msaada wa chakula mbali mbali kwa watu wenye  mazingira magumu Wajane,  Wazee wasiojiweza, watu wenye ulemavu na Watoto Yatima huko Kidimni, amesema  kuna baadhi ya Watoto wanaishi katika mazingira  magumu hivyo michango na misaada mbalimbali inahitajika ili kuwasaidia watu hao.

 
Amesema kuna baadhi ya watu wamekuwa wakitumia mianya hiyo ya kutoa misaada na hatimae  kuwafanyiwa vitendo vya udhalilishaji watoto na hata wazee, jambo ambalo linaleta athari kubwa katika jamii.

Hivyo amesema ni vyema jamii pamoja na Jumuiya mbalimbali kushirikiana na  Wazee na Wizara wanapohitaji kutoa misaada ili kusaidia kupunguza vitendo vya ukatili na udhalilishaji wa kijinsia katika jamii.

Hata hivyo bi Abeida ameishukuru Jumuiya hiyo ya Good People Hope  Box kwa kutoa msaada huo wa chakula na kuwaomba kuendelea kusaidia  Jamii kama hiyo ili kusaidia kuwapunguzia ukali wa maisha.

Nao waanzilishi wa Jumuiya  ya Good People Hope  Box, bibi Mi Sook Chol pamoja na  mumewe bwana   Kwan I'il Park wamesema wamekuwa wakisaidia kutoa huduma katika Jumuiya mbali  mbali kwa lengo  la kupunguza ukali wa maisha kwa watu wasiojiweza, wenye mazingira magumu, watu wenye ulemavu pamoja  na Watoto Yatima ili kuwapunguzia ukali wa maisha.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Jumuiya  Wazee ndugu  Amani  Suleiman  Kombo kwa niaba ya wazee wezake ametoa  shukurani kwa msaada waliopatiwa na kuomba wasichoke kutoa  kila watakapojaaliwa.

Msaada uliotolewa ni pamoja na Mchele,  Sukari, unga wa sembe, mafuta ya kupikia,chumvi, sabuni ya kufulia, pamoja na msuwaki na dawa ya meno.


IMEANDALIWA NA KITENGO CHA UHUSIANO WIZARA YA MAENDELEO YA JAMII JINSIA WAZEE NA WATOTO ZANZIBAR. 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.