Habari za Punde

SMZ Inafungua Ukurasa Mpya wa Maendeleo Kwenye Uchunguzi wa Ubora wa Bidhaa hapa Nchini kwa Kuzingatia Viwango vya Kimataifa.

 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akiondoa pazia kuashiria kuweka Jiwe la Msingi la Uzinduzi  wa Maabara Nne Mpya za Taasisi ya Viwango Zanzibar (ZBS) Maruhubia Wilaya ya Mjini Unguja na (kushoto kwa Rais ) Mke wa Rais wa Zanzibar Mama Mariam Mwinyi, na Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja Mhe.Idrissa Mustafa Kitwana na (kushoto) Waziri wa Biashara na Maendeleo ya Viwanda Zanzibar Mhe. Omar Said Shaban, uzinduzi huo uliyofanyika leo 15-3-2023

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema inafungua ukurasa mpya wa maendeleo kwenye uchunguzi wa ubora wa bidhaa hapa nchini kwa kuzingatia viwango vya Kimataifa.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi, ameyasema hayo alipozindua maabara mpya nne za kisasa za taasisi ya viwango Zanzibar, ZBS Maruhubi wilaya ya Mjini mkoa wa Mjini Magharibi Unguja.

Alisema Serikali ina nia ya dhati ya kulinda afya na usalama wa wananchi kwa kuchukua hatua stahiki za kupima ubora wa bidhaa mbalimbali zinazotumiwa nchini.

Dk. Mwinyi alieleza taifa linashuhudia mafanikio makubwa ya utekelezaji wa malengo ya Serikali mara baada ya uzinduzi wa maabara nyengine nne, za Vimelea, Maabara ya Vifungashio, Nguo na Ngozi na Maabara ya Umeme yenye vifaa vya kisasa vyenye uwezo mkubwa wa kupima sampuli na kutoa majibu ya kuaminika kwa kutumia teknolojia za kisasa.

“Ni matumaini yetu uwezo wa maabara hizi utaleta ufanisi wa haraka katika kupata majibu ya sampuli za bidhaa zinazoingizwa na zinazozalishwa nchini” alieleza Dk. Mwinyi.

Akizungumzia suala la kukuza uchumi wa nchi na kupunguza umaskini, Rais Dk. Mwinyi alisema suala hilo linakwenda sambamba na hatua ya kuimarisha maendeleo ya viwanda na biashara, aliongeza Serikali kupitia Baraza la Wawakilishi ilitunga Sheria ya Viwango ya Zanzibar Na. 1 ya mwaka 2011 ambayo ilianzisha taasisi ya (ZBS) mwaka 2012 na kupewa jukumu la kuweka viwango na kusimamia ubora wa bidhaa na huduma ikiwemo kuhakikisha soko la Zanzibar linakuwa na bidhaa zenye ubora unaostahili.

Alisema, moja kati ya changamoto kubwa iliyoikabili taasisi ya ZBS ni kutokuwepo kwa baadhi ya maabara zenye uwezo wa kupima sampuli za bidhaa na kupata matokeo kwa muda muwafaka nakueleza awali ZBS ilipeleka sampuli zake kwenye maabara za taasisi nyengine kama vile za TBS, Tanzania bara lakini sasa Serikali imelipatia ufumbuzi wa kudumu tatizo hilo kupitia maabara hizo mpya.

Hata hivyo, Dk. Mwinyi aliwataka watendaji wa ZBS kufanyakazi kwa bidii, ubunifu, uaminifu na kujiamini katika kusimamia majukumu yao na kuwaeleza kwamba kazi zao ni muhimu kwa maendeleo ya viwanda, biashara na wajasiriamali katika kuimarisha soko la bidhaa na kukuza maendeleo ya uchumi wa Zanzibar.

Akizungumza kwenye hafla hiyo, Waziri wa Biashara na Maendeleo ya Viwanda Omar Said Shaaban alisema suala la viwango ni moja ya mazingira mazuri ya biashara Zanzibar.

Alieleza Zanzibar haiwezi kufanyabiashara kwa bidhaa zisizo na viwango na kuongeza kuimarika kwa maabara za ZBS ni moja ya maagizo ya serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Alisema Wizara imezindua mfumo wa kisasa utakaorahisisha maombi ya leseni za biashara kupitia teknolojia ya kisasa utakaojumuisha mamlaka 45 zinazotoa leseni na kuunganisha taasisi nyengine za Serikali zinazotegemeana zitakazofanyakazi pamoja na kuongeza, maendeleo hayo ni mafanikio ya miaka miwili ndani ya uongozi wa awamu ya nane ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Naye, Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi wa Viwango Zanzibar, (ZBS) Yussuf Nassor Majid alisema mbali ya mafanikio makubwa yaliyofikiwa na taasisi hiyo kwa kuzindua maabara nne za kisasa pia wanatarajia kuwa na kituo kikubwa cha ukaguzi wa magari kitakachokuwa na uwezo wa kukagua magari 150 kwa siku, alikitaja kuwa kuwa  chA mfano kwa Afika Mashariki na Kati pamoja na maabara ya vifaa vya ujenzi itakayofadhiliwa na World Bank itakuwa na uwezo wa kupima vifaa vyote vya ujenzi vikiwemo nondo, kokoto, matofali, saruji, bati na vifaa vyengine vya ujenzi.

IDARA YA MAWASILIANO

IKULU, ZANZIBAR

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.