Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Mwinyi Amekutana na Ujumbe Madaktari Bingwa Kutoka Nchini Saudi Arabia Ikulu Zanzibar

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi (kulia) alipokuwa akizungumza na mgeni wake  Balozi  wa Saudi Arabia Nchini Tanzania Mhe.Yahya Ahmed Okeish, alipofika kujitambulisha leo Ikulu Jijini Zanzibar.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi, ameipongeza Serikali ya Saudi Arabia kwa jitihada kubwa wanayoitoa Tanzania kuungamkono miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo sekta ya Afya, maji, miundombinu ya barabara na kusaidia uzalishaji umeme.

Dk. Mwinyi ameyasema hayo Ikulu, Zanzibar alipozungumza na Balozi wa Saudi Arabia nchini Tanzania, Mhe.  Yahya Ahmed Okeish aliefika kujitambulisha.

Rais Dk. Mwinyi alisema kuwepo kwa ubalozi huo nchini ni mwendelezo wa ushirikiano mwema uliopo baina ya Tanzania ikiwemo Zanzibar na Saudi Arabia.

Dk. Mwinyi aliipongeza Serikali ya Saudi Arabia kwa ushirikiano wanaoutoa Tanzania Bara kwenye uzalishaji wa umeme, kuungamkono ujenzi wa barabara ya Wete, Pemba pamoja na kusaidia ukarabati mkubwa kwenye hospitali kuu ya Mnazi Mmoja ambayo inatarajiwa kufanya upasuaji mkubwa zaidi mara baada ya kumalizika kwa ukarabati wa vyumba vya upasuaji vinavyotarajiwa kuwa na vifaa vya kisasa kwa msaada wa Mfuko wa Saudia.

Pia, Rais Dk. Mwinyi, aliikaribisha Serikali ya Saudi Arabia kuwekeza kwenye Shamba la Makurunge, Bagamoyo, linalomilikiwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, ambalo linafaa kwa uwekezaji wa Kilimo, Uvuvi na Utalii.

Halikadhalika, Dk. Mwinyi aliendelea kuishukuru Serikali ya Saudi Arabia kwa msaada mkubwa kwa Zanzibar kupitia sekta ya afya ambapo imetoa timu ya madaktari wa upasuaji iliyojitolea kuweka kambi na kuwatibu Wazanzibari.

Aidha, Dk. Mwinyi aliipongeza timu ya madaktari 21 kutoka Saudi Arabia waliojitolea kuweka kambi ya matibabu kwenye jimbo la Gando kisiwani Pemba ambako waligundua zaidi ya kesi 680 na kufanya upasuaji.

Alisema, kambi za matibabu ni moja ya eneo muhimu la ushirikiano uliopo baina ya Zanzibar na Saudi Arabia kwani zimekua na msaada mkubwa kupunguza changomo nyingi kwenye sekta ya afya nchini.

Mbali na sekta ya afya pia Rais Dk. Mwinyi aligusia maeneo mengine ya ushirikiano wao ikiwemo uwekezaji, biashara, uvuvi na kilimo cha Samaki kupitia sekta ya Uchumi wa Buluu.

“Tunahitaji uwekezaji zaidi, hasa kwenye Sekta ya Uchumi wa Buluu, nchi yetu imezungukwa na bahari, Sera yetu kuu ya uchumi ni ‘Uchumi wa Buluu’, hivyo tunahitaji uwekezaji mkubwa kwenye eneo hilo, kupitia uvuvi na kilimo cha Samaki” Dk. Mwinyi alimweleza Balozi huyo.

Rais Dk. Mwinyi aliipongeza tena Saudi Arabia kuwa kuchaguliwa kuwa mwenyeji wa maonesho makubwa ya biashara duniani, (Expo 2023).

Naye, Balozi, Yahya Ahmed Okeish alisema Saudi Arabia imekua na msaada mkubwa kwa bara la Afrika ikiwemo Tanzania ambapo Zanzibar pia itanufaika kwa kiasi kikubwa na fursa nyingi baada ya kusainiwa kwa makubaliano ya mamilioni ya dola za Marekani zilizoelekezwa Afrika.

Alisema, Tanzania na Saudi Arabia kwa muda mrefu, zimekua zikibadilishana uzoefu baina yao kupitia sekta mbalimbali za ushirikiano wao.

Balozi Yahya pia aliambatana na timu ya mataktari wa upasuaji 21 kutoka Saudi Arabia ambao walikuwepo kisiwani Pemba kwenye jimbo la Gando walikoweka kambi ya matibabu kwa maradhi mbalimbali.

Akizungumza kiongozi wa timu ya madaktari hao, Dk. Aiman Al Soluman alisema, waligundua kesi 689 kati ya wagonjwa wengi waliojitokeza kwenye kambi ya matibabu yao, kati yao kesi 303 zilifanyiwa upasuaji.

Alisema, wagonjwa wa upasuaji wa jumla walikua 124 kati yao 76 walifanyiwa upasuaji wa jumla, pia alieleza waligundua matatizo ya mfumo wa mkojo kwa watoto na watu wazima kwa kesi 112 na kesi 78 zilifanyiwa upasuaji.

Dk. Al Soluman pia aligusia operesheni ya viungo vya mwili zilivyopotea au kupata athari ikiwemo makovu makubwa, (plastic surgery) alisema walipata kesi 60 na 56 zilifanyiwa upasuaji.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi (kulia) alipokuwa akipokea zawadi kutoka kwa  mgeni wake  Balozi  wa Saudi Arabia Nchini Tanzania Mhe.Yahya Ahmed Okeish, alipofika kujitambulisha leo Ikulu Jijini Zanzibar.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi (kulia) akifuatana na  mgeni wake  Balozi  wa Saudi Arabia Nchini Tanzania Mhe.Yahya Ahmed Okeish, alipofika kujitambulisha leo Ikulu Jijini Zanzibar 
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi (katikati) alipokuwa akizungumza na Ujumbe wa Madaktari Ishirini na Moja kutoka Nchini Saudi Arabia,waliofika Kisiwani Pemba katika Jimbo la Gando kutoa huduma mbali mbali za kiafya kwa Wananchi,walifika Ikulu Jijini Zanzibar leo kumsalimia Mhe.Rais wakiambatana na  Balozi  wa Saudi Arabia Nchini Tanzania Mhe.Yahya Ahmed Okeish pamoja na Mbunge Jimbo la Gando Mhe.Salim Mussa Omar , (wa pili kulia). 08/12/2023.
 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi (kulia) alipokuwa akizungumza na Ujumbe wa Madaktari Ishirini na Moja kutoka Nchini Saudi Arabia,waliofika Kisiwani Pemba katika Jimbo la Gando kutoa huduma mbali mbali za kiafya kwa Wananchi,walifika Ikulu Jijini Zanzibar leo kumsalimia Mhe.Rais wakiwa na  Balozi  wa Saudi Arabia Nchini Tanzania Mhe.Yahya Ahmed Okeish, (wa pili kulia).
                                                 8/12/2023.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.