Habari za Punde

Serikali Kutumia Gharama Kubwa Kulipa Fidia Wananchi Ujenzi wa Barabara

 
SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar, imewaonya waanchi kutojenga maeneo karibu na miundombinu ya barabara, maji na umeme ili kupunguza gharama kwa Serikali.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Al hajj Dk. Hussein Ali Mwinyi ametoa onyo hilo alipojumuika pamoja na waumini wa Kiislamu kwenye Ibada ya Sala ya Ijumaa, iliyoambanata na ufunguzi wa Msikiti wa ijumaa, Masjid Sheikha Naima bint Sultan Al Qasmi pamoja na madrsa, Tomondo Wilaya ya Magharibi B Mkoa wa Mjini Magharibi.

Alisema nia ya Serikali ni kufikisha miundombinu ya barabara maeneo yote yanayohitajiwa na jamii lakini wakati mwengine Serikali inashindwa kutokana na gharama kubwa za ulipaji wa fidia wananchi waliojenga kiholela karibu na maeneo ya barabara.

Alisema, mara nyingi Serikali hukumbana na gharama kubwa za ulipaji wa fidia kwa wananchi kuliko gharama za kutengeneza miundombinu hiyo, alishauri kutolewe vibali maalum kwa wananchi watakaojenga karibu na barabara.

“Mara nyingi matatizo hayo yanatukuta kwasababu watu wajenga ovyo, hawachi hata njia ya kupita gari, anakuja mtu anaweka jengo lake katikati ya barabara, inakua mtihani unapotaka kupitisha miundombinu inakubidi uanze kulipa fidia kwanza, pesa nyingi zinaingia kwenye fidia kabla hujaanza ujenzi wa hiyo barabara”

“Wananchi muwe waangalizi wenyewe, anaejenga sehemu itakayopita barabara mumzuie, hii itawaathiri nyinyi wenyewe msipoifanyia kazi, ombi langu kwenu, watu waambiwe wajenge kwa vibali maalumu, wasijende ovyo wala sehemu zitakazo pita barabara” aliisihi jamii.

Hivyo, Al hajj Dk. Mwinyi ameitaka jamii kuwa mfano bora kwa kukatazana wenyewe kwa wenyewe kutojenga maeneo karibu na miundombinu ya barabara ili kuipunguzia mzigo mzito Serikali.

Al hajj Dk. Mwinyi pia aliitaka jamii kuwafundisha mema ya dini watoto ili waijue dini yao, pamoja na kuipongeza taasisi ya “Al Noor Charitable Agency for the need” kwa kushughuhulika na masuala mengi ya jamii wakiwemo watoto yatima, wajane, watu wazima na wenye ulemavu pamoja na kujishughulisha na huduma za jamii, ikiwemo elimu, maji (visima), kujenga misikiti mikubwa yenye hadhi ya juu na madrasa.

Pia, Al hajj Dk. Mwinyi ameitaka Misikiti mengine kuiga mifano mema kwa kushughulikia na kuyafanyia kazi matatizo yanayoikabili jamii kwenye mitaa yao pamoja na kufanya ibada kwa wingi.

Sambamba na kuwataka waumini wanaoitumia misikiti hiyo, kuitunza na kuikarabati kwa huduma zote zitakazohitajika zikiwemo maji, umeme, kuwalipa wanaohudu misikiti na matengenezo mengine ya lazima.

“Misikiti ifundushe vijana na watoto dini yao, ukiachia mbali kufanya ibada pekee, pia kuitumia vizuri misikiti hiyo” alitoa msisitizo.

Hata hivyo, Al hajj Dk. Mwinyi alieleza jinsi alivyolipokea ombi la ujenzi wa barabara iliyopita kwenye masjidi hiyo na kuahidi kuitengeneza ipitike kwa wepesi.

Akitoa shukurani kwa niaba ya taasisi ya kiislam ya Al Noor ya Zanzibar “Al Noor Charitable Agency for the need” Mkurugenzi wa taasisi hiyo, Sheikh Luay Mohamed Makhfoudh alisema, ufunguzi wa msikiti huo ni maadhimisho ya miaka 20 ya huduma kwa jamii ya Zanzibar waislamu na wasiokua waislamu zinazotolewa na taasisi hiyo tokea ilipozinduliwa kwake mwaka 2003.

Alisema, Masjid Naima bint Hamed Al Qasmi ni msikiti wa 28 kati ya misikiti iliyojengwa na taasisi hiyo, unauwezo wakuchukua hadi waumini 880 ambapo kwa mwaka huu pia wamejenga misikiti mitatu ukiwemo huo na mengine midogo iliyojengwa maeneo ya Kama na Koani.

Alisema, misikiti 20 kati ya 28 inaitwa Markadhi Islami mbali na kutoa huduma za ibada pia ina madrsa zenye uwezo wakuchukua hadi wanafunzi 300, zinazosomesha tahfidh Quran na masomo ya kiingereza na hisabati ili kuongeza nguvu kwenye masomo hayo nchini.

Alisema, wakati wa jioni misikiti hiyo hutoa darsa kwa wanawake na usiku madrsa za misikiti hiyo hutumika kwa mabweni ya wanafunzi kupata misaada ya kujifunza masomo yao ya skuli ili kutoa matokea mazuri masomo yao ya skuli.

Pia alieleza madrsa zao zina wanafunzi zaidi ya 7,000 kati ya hao 550 ni yatima, hivyo, aiitaka jamii kusajili yatima kwenye taasisi za “Al Noor Charitable Agency for the need” hasa waliofiliwa na baba zao ambao husaidiwa kwa huduma majumbani mwao, kusomeshwa hadi nje ya nchi kwa mataifa ya India, Madina, Morocco, Sudan, Uturuki na Yemen.

Taasisi ya “Al Noor Charitable Agency for the need” pia wanashughulikia watu wenye ulemavu, wajane, na watu wazima waliosajiliwa na taasisi hiyo hupewa kipaombele inapopatikana riski ya sadaka.

Mapema akisoma risala ya ufunguzi wa Masjid Sheikha Naima bint Sultan Al Qasmi, pamoja na madrsa yake, Ustadhi Abdul Mabrouk Kitwana kwa niaba ya wananchi wa Tomondo, walimshukuru Al hajj Dk. Mwinyi kwa mapenzi yake ya kujumuika pamoja nao kwenye ibada ya sala ya Ijumaa sambamba na kufikisha shukurani zao za dhati kwa mfadhili wa msikiti huo, Sheikha Naima bint Sultan pamoja na taasisi ya “Al Noor Charitable Agency for the need” kwa kuishirikisha kikamilifu jamii ya Tomondo kwenye ujenzi wa msikiti huo.

IDARA YA MAWASILINO, IKULU ZANZIBAR

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.