MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar,
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Al hajj Dk.
Hussein Ali Mwinyi, amewahimiza Wanachama wa Chama hicho pamoja na
waislamu kwa ujumla kuendelea kukithirisha ibada kwa siku chache zilizobakia za
Mfungo mtukufu wa Mwezi wa Ramadhani ili kupata radhi za Mwenyezi Mungu (S.W).
Al hajj Dk. Mwinyi ametoa nasaha hizo kwenye iftari ya
pamoja iliyoandaliwa na Ofisi kuu ya Chama hicho, Kisiwandui – Wilaya ya Mjini
mkoa wa Mjini Magharibi, alipojumuika na Wanachama wa CCM, viongozi wa chama
hicho na jumuiya zake, viongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Aidha, Al hajj Dk. Mwinyi aliwashukuru wanachama wa chama
hicho kwa kukubali kwao kujumuika pamoja kwenye futarisho hilo na kueleza kuwa
limejenga dhana halisi la umoja, mshikamano, ushirikiano na upendo baina yao
kwa kukusanyika pamoja kweye ibada hiyo kama chombo cha siasa.
“Nimefurahi kwa ujio wenu hapa, umezidisha umoja,
ushirikiano, upendo na mshikamano kati yetu kama chombo cha siasa, kukutana
kwetu pamoja kwenye muktadha huu ni jambo jema” alisifu Al hajj Dk. Mwinyi.
Akizungumza kwenye hadhara hiyo, Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Zanzibar Al hajj Dk. Muhamed Said Muhamed, Dimwa naye alisifu na kushukuru
ushirikiano wa pamoja baina ya wanachama wa CCM na viongozi wa Serikali katika
kutekeleza kwa vitendo Ilani ya Chama hicho ya 2020 2025 kwa kuimarisha
maendeleo ya nchi.
Pamoja na kushukuru uondozi wa chama hicho kwa maandalizi
mazuri ya futarisho hilo na kusifu kuwaunganisha pamoja baina ya viongozi wa
Chama Cha Mapinduzi CCM, viongozi na wadau wengine wa Serikali pamoja na
viongozi wastaafu kwa kuwakushanya pamoja kwenye futari hiyo.
Naye, Katibu wa Kamati Maalum (NEC)
Itikadi, Uenezi na Mafunzo CCM Zanzibar, Al hajj Komred Khamis Mbeto Khamis
aliwasihi waumini wa dini ya Kiisalaam na wanachama wa CCM kuendelea kuwaombea
dua njema viongozi wa nchi ili waendelee kuliongoza vyema taifa pamoja na
kuepushwa na shari za mabilisi na viumbe wabaya.
Futari hiyo pia ilihudhuriwa na
Wajumbe wa Kamati kuu ya CCM Taifa, akiwemo Makamu
wa Pili wa Rais wa Zanzibar Al hajj Hemed Suleiman Abdulla pamoja na viongozi
wengine wastaafu akiwemo Balozi Seif Ali Iddi, Makamu wa Pili mstaafu wa Serikali
ya Mapinduzi ya Zanzibar na wanachama wengine.
Tokea kuaza mwezi Mtukufu wa Ramadhan, Al hajj Dk. Mwinyi
ameendeleza utaratibu wa kufutari pamoja na wananchi wa visiwa vya Unguja na
Pemba, waumini wa dini ya kiislam, wanajamii kupitia makundi mbalimbali yenye
uhitaji pamoja na wananchi wa kawaida ili kujenga dhana nzima ya kudumisha
amani, utulivu, mshikamano na ushirikiano uliopo baina wa Serikali na wananchi
wake.
IDARA YA MAWASILIANO
IKULU, ZANZIBAR
No comments:
Post a Comment