Habari za Punde

Al hajj Dk. Hussein Amewahimiza Wanachama wa CCM Pamoja na Waislamu kwa Ujumla Kuendelea na Ibada kwa siku chache zilizobakia za Mwezi Mtukufu wa Ramadhani

 
MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Al hajj Dk. Hussein Ali Mwinyi, amewahimiza Wanachama wa Chama hicho pamoja na waislamu kwa ujumla kuendelea kukithirisha ibada kwa siku chache zilizobakia za Mfungo mtukufu wa Mwezi wa Ramadhani ili kupata radhi za Mwenyezi Mungu (S.W).

Al hajj Dk. Mwinyi ametoa nasaha hizo kwenye iftari ya pamoja iliyoandaliwa na Ofisi kuu ya Chama hicho, Kisiwandui – Wilaya ya Mjini mkoa wa Mjini Magharibi, alipojumuika na Wanachama wa CCM, viongozi wa chama hicho na jumuiya zake, viongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Aidha, Al hajj Dk. Mwinyi aliwashukuru wanachama wa chama hicho kwa kukubali kwao kujumuika pamoja kwenye futarisho hilo na kueleza kuwa limejenga dhana halisi la umoja, mshikamano, ushirikiano na upendo baina yao kwa kukusanyika pamoja kweye ibada hiyo kama chombo cha siasa.

“Nimefurahi kwa ujio wenu hapa, umezidisha umoja, ushirikiano, upendo na mshikamano kati yetu kama chombo cha siasa, kukutana kwetu pamoja kwenye muktadha huu ni jambo jema” alisifu Al hajj Dk. Mwinyi.

Akizungumza kwenye hadhara hiyo, Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Zanzibar Al hajj Dk. Muhamed Said Muhamed, Dimwa naye alisifu na kushukuru ushirikiano wa pamoja baina ya wanachama wa CCM na viongozi wa Serikali katika kutekeleza kwa vitendo Ilani ya Chama hicho ya 2020 2025 kwa kuimarisha maendeleo ya nchi.

Pamoja na kushukuru uondozi wa chama hicho kwa maandalizi mazuri ya futarisho hilo na kusifu kuwaunganisha pamoja baina ya viongozi wa Chama Cha Mapinduzi CCM, viongozi na wadau wengine wa Serikali pamoja na viongozi wastaafu kwa kuwakushanya pamoja kwenye futari hiyo.

Naye, Katibu wa Kamati Maalum (NEC) Itikadi, Uenezi na Mafunzo CCM Zanzibar, Al hajj Komred Khamis Mbeto Khamis aliwasihi waumini wa dini ya Kiisalaam na wanachama wa CCM kuendelea kuwaombea dua njema viongozi wa nchi ili waendelee kuliongoza vyema taifa pamoja na kuepushwa na shari za mabilisi na viumbe wabaya.

Futari hiyo pia ilihudhuriwa na Wajumbe wa Kamati kuu ya CCM Taifa, akiwemo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Al hajj Hemed Suleiman Abdulla pamoja na viongozi wengine wastaafu akiwemo Balozi Seif Ali Iddi, Makamu wa Pili mstaafu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na wanachama wengine.

Tokea kuaza mwezi Mtukufu wa Ramadhan, Al hajj Dk. Mwinyi ameendeleza utaratibu wa kufutari pamoja na wananchi wa visiwa vya Unguja na Pemba, waumini wa dini ya kiislam, wanajamii kupitia makundi mbalimbali yenye uhitaji pamoja na wananchi wa kawaida ili kujenga dhana nzima ya kudumisha amani, utulivu, mshikamano na ushirikiano uliopo baina wa Serikali na wananchi wake.

IDARA YA MAWASILIANO IKULU, ZANZIBAR

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.