Kada ya Uuguzi Watakiwa Kuongeza Weledi, Nidhamu na Uadilifu Katika Utoaji wa Huduma za Afya Zanzibar

KATIBU Mkuu Wizara ya Afya Zanzibar, Dk. Mngereza Mzee Miraji ameitaka kada ya uuguzi kuongeza weledi, nidhamu na uadilifu katika utoaji wa huduma za afya, akisema kuwa  Serikali inategemea mchango mkubwa kutoka kwa wauguzi watarajali waliohitimu mafunzo yao.

KATIBU Mkuu wa Wizara ya Afya Zanzibar, Dk. Mngereza Mzee Miraji ameitaka kada ya uuguzi kuongeza weledi, nidhamu na uadilifu katika utoaji wa huduma za afya, akisema kuwa  Serikali inategemea mchango mkubwa kutoka kwa wauguzi watarajali waliohitimu mafunzo yao.

Akizungumza katika kikao kilichowakutanisha wauguzi waliomaliza mafunzo ya utarajali Tanzania bara na viongozi wa Wizara ya Afya kilichofanyika ofisi za wizara hiyo Mngereza alisema kuwa Serikali inaendeleza mkakati wa kuimarisha huduma kwa wananchi kupitia uinarishaji wa rasilimali watu, huku wauguzi wakiwa nguzo muhimu katika mpango huo.

“Tunatarajia muwe mabalozi wa huduma bora. Uadilifu, huruma na kufuata maadili ya kazi ni msingi wa hadhi ya kada yenu. Serikali inawahitaji, na wananchi wanawategemea,” alisema Mngereza.

Katika maelezo ya mpango mkakati wa Wizara ya Afya, Katibu Mkuu alieleza kuwa Serikali inatekeleza vipaumbele kadhaa, ikiwemo kuimarisha huduma za msingi, kuondoa changamoto za upatikanaji wa huduma vijijini, na kuongeza ufanisi wa vituo vya afya na kubainisha kuwa Wauguzi ndio nguzo  muhimu Katika kufanikisha mpango huo.

"Tunahitaji muwe sehemu ya mageuzi haya, kwa kuzingatia maelekezo ya Serikali na viongozi wenu wa afya,” alisisitiza Mngereza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Uuguzi na Ukunga, Mwanaisha Juma  Fakih aliwataka wauguzi waliomaliza mafunzo hayo kuhakikisha wanazingatia kanuni na maadili ya taaluma kila wanapokuwa kazini, akibainisha kuwa taaluma ya uuguzi inahitaji nidhamu na utu.

“Maadili na uwajibikaji ndio silaha yetu. Muuguzi anayeheshimu muda wa kazi, anayefanya kazi kwa weledi na anayeheshimu utu wa mgonjwa, huyo ndiye tunayemtaka katika mfumo wa afya. Taaluma hii haiwezi kusimama bila maadili,” alisema Mwanaisha .

Aliongeza kuwa vitendo vinavyodhalilisha taaluma havitavumiliwa na wizara, huku akiwasisitiza kuifahamu vizuri miongozo ili kuepuka migongano ya kitaaluma.

Alisisitiza umuhimu wa kutoa huduma zenye heshima, salama na zinazozingatia thamani ya mgonjwa, huku akihimiza matumizi sahihi ya rasilimali, lugha (customer care) na uwajibikaji wa kitaaluma.

"Utendaji wenu ni lazima uendane na  muonekano wenu ni muhimu kuzingatia maadili na kujali utu, hii itawaongezea thamani na kuonesha utofauti wa kiutendaji kabla na baada ya kurudi masomoni" Alisema  Mwanaisha

Kikao hicho pia kilitoa mwongozo wa kina kuhusu usajili na utoaji wa leseni ya uuguzi kupitia Baraza la Wauguzi na Wakunga Zanzibar ambapo mrajisi wa Baraza hilo Vuai Kombo Haji aliwakumbusha wahitimu kufuata taratibu zote za kujisajili na kubainisha kuwa usajili sahihi ni hatua ya kwanza ya kutambulika kisheria kama mtaalamu.

 “Ni wajibu wenu kuhakikisha mnapata leseni, maana bila ya nyaraka hizi hamtaruhusiwa kutoa huduma popote nchini,” alieleza Vuai

Baadhi ya wauguzi waliomaliza mafunzo ya utarajali  waliipongeza Wizara kwa kuandaa mafunzo hayo Ambayo yamewajengea uwezo na uzoefu kutoka Katika hospital  walizofanya Mafunzo hayo Kwa vitendo na kubainisha kuwa yamewajenga kujiamini.

“Tumepata mwanga wa nini Serikali inatarajia kutoka kwetu. Tuko tayari kufanya kazi kwa bidii na kuheshimu utu wa wagonjwa.” alisema Amina mmoja wa wahitimu hao.

Kikao hicho kililenga kuhakikisha wahitimu hao wanarudi rasmi makazini wakiwa na uelewa wa pamoja, misingi ya maadili, na dhamira ya kutoa huduma bora kwa wananchi.




Post a Comment

0 Comments