Habari za Punde

Wizara ya habari watakiwa kuendeleza ushirikiano

Na Mwandishi wetu
WATENDAJI na wafanyakazi  wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo, wametakiwa kuendelea kushirikiana katika kutekeleza majukumu waliyopangiwa katika taasisi zao.

Wito huo umetolewa jana na Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Mhe. Bihindi Hamad Khamis katika tafrija iliyoandaliwa na uongozi wa Wizara hiyo kuwapongeza watendaji na wafanyakazi wake kwa ushirikiano waliotoa kufanikisha utekelezaji malengo ya Wizara na kupitishwa kwa bajeti yake ya mwaka wa fedha 2014-2015.

Mhe. Bihindi aliwaambia wafanyakazi hao kwamba mafanikio ya Wizara hiyo katika kuwapatia huduma bora wananchi yanategemea utendaji kazi wa pamoja wa wafanyakazi hao katika sehemu zao za kazi.

“Kufanikiwa kwa Wizara katika kutekeleza malengo yake na hatimae kupitishwa bajeti ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2014-2015, kumechangiwa kwa kiasi kikubwa na ushirikiano, hivyo endelezeni ushirikiano huo,” alisisitiza.

Aidha Mhe. Bihindi ameipongeza Kamati ya Baraza la Wawakilishi ya Mifugo, Utalii, Uwezeshaji na Habari kwa kufanya kazi kwa karibu na Wizara, pamoja na kuishauri vyema hali iliyosaidia Wizara kutekeleza vyema majukumu yake, pamoja na kupitishwa bajeti yake ya mwaka wa fedha 2014-2015.

Mhe. Bihindi aliiahidi Kamati hiyo kwamba Wizara itaendelea kuipa ushirikiano na kuomba ushauri mara kwa mara katika utekelezaji majukumu yake.

Akitoa shukurani katika hafla hiyo, Mjumbe wa Kamati hiyo Mhe. Asha Bakari Makame, alisisitiza ushirikiano kwa watendaji na wafanyakazi wa Wizara hiyo ili waweze kuitumikia vyema jamii ikizingatiwa kuwa inahusika na mambo yanayohusu maisha ya kila siku ya wananchi.

Pia aliihakikishia Wizara hiyo kwamba Kamati itaendelea kutoa ushirikiano na ushauri kila itapoombwa na uongozi wa Wizara.

Katika hafla hiyo iliyofanyika ukumbi wa Salama hoteli ya 
Bwawani Mjini Zanzibar, iliyoshirikisha watendaji na wafanyakazi wa Wizara hiyo wakiongozwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo, Dk. Ali Mwinyikai, pia ilihudhuriwa na Wajumbe wa Kamati ya Baraza la Wawakilishi ya Mifugo, Utalii, Uwezeshaji na Habari ikiongozwa na Mwenyekiti wake, Mhe. Mlinde Mabrouk Juma.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.