Habari za Punde

Viongozi wa Ushirika Watakiwa kuwa Waadilifu na Nidhamu katika Utanzaji Fedha

Na Bakar Mussa, Pemba

Viongozi wa Chama kikuu cha Ushirika cha akiba na mikopo  Zanzibar, (ZASCUU) wametakiwa kuwa na uadilifu , nidhamu katika utunzaji wa fedha ili kuepusha migogoro kwa Wanachama wa taasisi hiyo.

Akizungumza katika ufunguzi wa mkutano mkuu wa Chama hicho uliofanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Chake Chake Pemba, Naibu Katibu mkuu Wizara ya Fedha ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Ali Khamis Juma, alisema kuwa iwapo uadilifu na Nidhamu katika utunzaji wa Fedha za Wanachama utakuwa na mashaka ni wazi kuwa juhudi za kufikia malengo ya maendeleo kupitia sekta hiyo yatakwama.

Alieleza ili malengo ya chama hicho yaweze kufikiwa ni lazima kwa Viongozi wa  taasisi hiyo kufuata sheria zilizowekwa kwa kufanya mikutano inayowahusu wao na Wanachama wao kwa kuzingatia uwazi na Uwajibikaji kwa kukumbuka kuwa lengo lwa kuanzishwa kwa taasisi kama hizo ni kuwafanya Wananchi wapate mkombozi wao katika harakati za kupambana na umaskini wakipato.

“Nidhamu, uadilifu na usimamizi wa majukumu katika sehemu zozote za kazi ni kitu muhimu , hivyo ni lazima kila mmoja awajibike kwa sehemu aliyopo ili kujenga utendaji bora na wenye maslahi kwa umma,” alisema Naibu Waziri wa Fedha.


Naibu Waziri huyo, alifahamisha kuwa ili ZASCUU, iweze kuwa endelevu ni lazima kuwepo makubaliano ya kweli baina ya Viongozi na wanaoongozwa, zikiwemo utekelezaji wa ahadi zilizowekwa ili kujenga Kuaminiana baina ya Viongozi na Wanachama.

Hata hivyo aliwataka Wanachama wa taasisi hiyo kutowa michango yao iwe ya fedha ama mawazo ya kujenga , yatakayo saidia  kupatikana maendeleo endelevu ambayo yatawawezesha kufikia malengo yao kwa kuinuwa uchumi wa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.

“ Nitafurahi sana nikiona kuwa chama hichi cha ZASCUU, kinaendelea kuwepo na kutowa tija kwa Wanachama wake , jambo ambalo litakwenda sambamba na mkakati wa Serikali wa kukuza Uchumi na kupambana na Umaskini Zanzibar (MKUZA),”alifahamisha .

Juma , aliwasihi Wanachama wa Ushirika huo  kuwa wadadisi wakubwa juu ya ahadi wanazopewa na Viongozi wao jambo ambalo litajenga Nidhamu kwa viongozi wa taasisi hiyo , kwani Viongozi waliowengi wa taasisi   hizo husahau kuwa wao ni Watumishi wa WanaSaccos .

Aliitaka ZASCUU kwa upande wa kisiwa cha Pemba , kujenga utamaduni wa kusaidiana bila ya kuweka mbele faida (Riba) kwani lengo lao ni kuona chama chao kinamuwa endelevu na kinatowa mafanikio makubwa kwa walengwa.

Hata hivyo alitowa wito kwa Viongozi wa Chama hicho kuwa na ratiba ya utendaji wa kazi za kila siku, jambo ambalo litaleta ufanisi na kuondowa malalamiko  yasiokuwa ya lazima.

Kwa upande wake , Ofisa Mdhamini Wizara ya Uwezeshaji , Ustawi wa Jamii Pemba, Mauwa Makame Rajab, alimuhakikishia Naibu Waziri huyo kuwa ZASCUU, itafanya juhudi kujitangaza Kisiwani humo ili kuweza kupata Wanachama wengi zaidi na kukuza mtaji wao.

Aliwataka WanaSaccos , kuondosha migogoro ndani ya Vyama vyao ili ziweze kuendelea na kuleta mafanikio kwa Wanachama wake , ambao bila wao haziwezi kustawi.

Hadi sasa ZASCUU, inajumla ya Vyama (Saccos) 45 wanachama , kati ya hizo 17 ziko Kisiwani Pemba na 28 Unguja , ambapo malengo yao ni kuhakikisha ina Vyama visivyopunguwa 150 vya akiba na mikopo kwa Zanzibar mzima na vinakuwa Wanachama ifikapo mwaka 2018

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.