Habari za Punde

Milele Foundation yatiliana saini na chuo cha taaluma za sayansi ya afya kusaidia huduma za afya vijijini

 Mratibu wa Milele Zanzibar Foundation Ali Bakari Amani akitoa maelezo ya Mradi wa Champion in Health utakavyowasaidia wanafunzi watakaojiunga na mradi huo katika kipindi cha miaka mitatu wakati wa utiaji saini katika Chuo cha Taaluma za Sayansi za Afya kiliopo Mbweni Nje kidogo ya Mji wa Zanzibar.
 Kaimu Mkuu wa Chuo cha Taaluma za Sayansi za Afya Zanzibar Dkt. Amina Abdulkadir akitiliana saini na Mkurugenzi Mtendaji wa Milele Zanzibar Foundation Yusouf Luiz  mkataba wa maridhiano ya kuimarisha huduma za Afya vijijini kupitia mradi wa Champion in Health.
  Baadhi ya wanachama wa Champion in Health wakifuatilia utiaji saini mkataba wa maridhiano kati ya Milele Zanzibar Foundation na Chuo cha Taaluma za Sayansi za Afya Zanzibar katika sherehe zilizofanyika Chuoni Mbweni nje kidogo ya mji wa Zanzibar.

Picha ya pamoja ya viongozi wa Milele Zanzibar Foundation  na Chuo cha Taaluma za Sayansi za Afya Zanzibar na baadhi ya wanafunzi watakaofaidika na mradi wa Champion in Health baada ya sherehe za utiaji saini kumalizika katika chuo hicho.
Picha na Makame Mshenga.

Na Ramadhani Ali/Maelezo 

Milele Zanzibar Foundation imetiliana saini mkataba wa maridhiano na Chuo cha Taaluma za Sayansi za Afya Zanzibar mradi wa kuboresha kiwango cha ubora wa utoaji wa huduma za afya katika maeneo ya vijijini.

Mradi huo wa miaka mitatu ujulikanao kwa jina la Champion in Health utaangalia changamoto za  Afya vijijini ambako kunaupungufu mkubwa wa wafanyakazi  kutokana na vijana wengi kukosa  hamu ya kufanyakazi katika maeneo hayo.

Akizungumza wakati wa kutia saini mradi huo katika Chuo cha Taaluma za Sayansi za Afya Mbweni, Mratibu wa Milelele Foundation Zanzibar Ali Bakari Amani alisema vijana 98 wakiwemo waliomaliza masomo mwaka huu 2016 na wengine wanaoendelea na masomo  Chuoni hapo watafaidika.

Aliyataja masharti ya  wanafunzi kuingia katika mradi huo kuwa ni  wale waliofanya vizuri katika masomo,  wawe tayari kufanya kazi vijijini baada ya kumaliza masomo na wazee wawe hawana uwezo wa kuwasomesha.

 Ameyataja maeneo makuu ya Mradi kuwa ni kuwapatia nafasi za masomo nje ya nchi wanafunzi walioteuliwa kuingia katika mradi, kuwaendeleza  na kuwajengea uwezo.

Kaimu Mkuu wa Chuo cha Taaluma za Sayansi za Afya Zanzibar Dkt. Amina Abdulkadir amewataka wanafunzi walioingia katika maradi huo kuutumia vizuri msaada huo na amewashauri kufuata sharti la kuwa tayari kufanya kazi sehemu yeyote watakayo pangiwa.

Mkurugenzi Kinga na Elimu ya Afya Dkt Fadhil Abdalla aliipongeza Milele Zanzibar Foundation kwa kuangali changamoto zinazoikabili jamii hasa vijijini na kuzitafutia ufumbuzi unaofaa.

Amesema Wizara hivi sasa inatilia mkazo  kuimarisha ubora wa utoaji huduma vijijini baada ya maeneo mengi kuwa na vituo vya afya na Milele Zanzibar Foundation imekuwa ikitoa msukumo mkubwa katika sula hilo tokea kuanzishwa kwake miaka minne iliyopita.

Mradi wa Champion in Health umetiwa saini na Kaimu Mkuu wa Chuo cha Taaluma za Sayansi za Afya Zanzibar DKT. Amina Abdulkari na Mkurugenzi Muendeshaji wa Milele Zanzibar Foundation Yusouf Luiz Caires

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.