Habari za Punde

Balozi Seif Asikiliza Mgogoro wa Wananchi na Mfadhili wa Ujenzi wa Msikiti wa Mitondooni Kisauni.

 Bango la Muonekano wa Msikiti wa Masjid Mitondooni Kisauni Zanzibar utakavyowa ukimaliza ujenzi wake huo O




Na. Othman Khamis OMPR.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi ameziagiza Taasisi zinazosimamia Mipango Miji, Mazingira, Ardhi na Halmashauri kukaa pamoja na Mjenzi wa Jengo la Msikiti wa Mitondooni Kisauni ili kuzitafutia ufumbuzi hitilafu zilizojitokeza katika uendelezaji wa ujenzi huo.

Alisema Taasisi zinayohusika na  Mipango Miji  lazima zihusike kikamilifu katika utafiti wa kina wa michoro ya ujenzi huo na kuridhina nayo kulingana na mazingira ya eneo lenyewe ili hatua za ujenzi ziende bila ya kuibuka kasoro nyengine hapo baadae.

Balozi Seif Ali Iddi alitoa agizo hilo alipofanya ziara fupi ya kukagua  jengo la Msikiti linalojengwa katika Mtaa wa Mitondooni Kisauni  Wilaya ya Magharibi    “ B”linalotarajiwa kuwa na Kitengo cha madarasa ya Elimu ya Dini itakayofundishwa  kwa lugha Nne za Kimataifa.

Alisema ujenzi wa majengo ya Taaluma na Ibada yanayozunguuka Makazi ya Watu ambayo yako  katika maeneo  yasiyo ya kawaida kama vile sehemu zinazotuwama maji yanahitaji kufanyiwa  utafiti  mkubwa  ili kuepuka athari zinazoweza kujitokeza wakati wa kuanza kwa matmizi ya majengo hayo.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alieleza kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar isingepelea kushuhudia mizozo na migongano inayojichomoza kati ya Wananchi na Wafadhili au wadau wanaoamua kusaidia miradi inayotekelezwa kwa faida ya kuinufaisha Jamii.

Balozi Seif  aliziasa Taasisi zinazosimamia masuala mbali mbali Nchini kuhakikisha kwamba zinawajibika ipasavyo kwa Watendaji wake kufuatilia au kukagua miradi wanayoisimamia ili kuwepuka mapema athari inayoweza kujitokeza hapo baadae.

Mapema Mkurugenzi Mtendaji wa Idara ya Mipango Miji na Vijiji Zanzibar Nd. Muhammad Juma  alimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwamba Taasisi yake itakuwa tayari kumsaidia Mjenzi wa Jengo hilo la Msikiti katika azma yake ya kuweka vitenga uchumi vinavyolenga kuuendesha Msikiti huo.

Nd. Muhammad alisema hatua hiyo itachukuliwa kutokana na  hali halisi ya eneo linalojengwa Msikiti huo kuwa na kawaida  ya uhifadhi wa maji yanayotokea milimani  wakati wa msimu wa mvua za Masika unapofikia.

Hata hivyo  Mkurugenzi Mtendaji huyo wa Idara ya Mipango Miji na Vijiji alikiri kwamba  Taasisi yake bado ina ipungufu wa Maafisa wanaohusika na Ukaguzi na ufuatiliaji wa masuala yanayohusu ujenzi katika maeneo mbali mbali Unguja na Pemba.

Ujenzi wa Msikiti Mitondooni uliopo katika Mtaa wa Kisauni  kwa mujibu wa Michoro, Ramani  na maazingira ya eneo lake  unatarajiwa ujenzi wake kulingana na Msikti  Mabuluu uliopo Kinazini Mjini Zanzibar.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.