Habari za Punde

Dk Shein aanza ziara Mkoa wa Kaskazini Pemba:Apokea taarifa ya kazi ya Mkoa



NA HAJI NASSOR, PEMBA
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe: Dk Ali Mohamed Shein, amesema baada kuitangaza Ilani ya uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015/2020, lazima sasa kuhama ofisini na kwenda kwa wananchi, kuona utekelezaji wake ulipofikia.
Dk Shein, ameeleza hayo ukumbi wa chuo cha SUZA Mchanga mdogo wilaya ya Wete kisiwani Pemba, wakati akuzungumza na wananchi, viongozi wa chama na serikali, mara baada ya kupokea taarifa ya kikazi ya Mkoa wa kaskazini Pemba.
Alisema, huu sio wakati tena wa kuganda ofisini ni lazima kuziacha kwa muda, na kwenda kwa wananchi waliomchagua, ili kuangalia kile alichokiahidi juu ya utekelezaji wake.
Alisema kukaa ofisini kwa muda mrefu, hakuwasaidii wananchi na wala hakuna ushuhuda wa kile kilichofanyika, hivyo ni lazima kuwatembelea.
Alieleza kuwa, ndio maana kwenye ripoti hiyo ya Mkoa, hataki kusema chochote, hadi hapo atakapoisoma na kutembelea maeneo husika, kuona utekelezaji wake.
“Mimi nimeshaipokea ripoti, na kwa vile nipo Pemba mwenyewe ntakwenda kuona haya yaliomo kwenye taarifa, maana sasa lazima sisi viongozi tuhame ofisini na twende moja kwa moja kwa wananchi kujiridhisha”,alifafanua.
Akizungumzia kuhusu ripoti hiyo, rais huyo wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, aliupongeza mkoa huo kwa taarifa nzuri na ilioshiba.
Alisema ijapokuwa hajaisoma yote ripoti hiyo, lakini kutokana na uwasilishwaji wake na alivyopokea taarifa, imeandaliwa vya kutosha na ina utekelezaji ndani yake.
“Taarifa yenu ya kikazi kwa kweli imeshiba na imebeba utendaji wa kazi wa kila idara, lakini leo sisemi kitu hadi nikimaliza ziara yangu, nasubiri kwenye majumuisho ntasema na kuuliza”,alisema Dk Shein.
Katika hatua nyengine, rais huyo wa Zanzibar, amewapongeza wananchi, viongozi wa chama na serikali kwa kuhudhuria kwenye uwasilishaji wa taarifa hiyo, na kusema hapo ndio watapata taarifa sahihi.
“Mimi nashangaa kuona baadhi ya mawaziri, makatibu wakuu na viongozi wengine hawashiriki ziara kama hizi ambazo ni za kiutendaji, na wala sio za kujifurahisha”,alifafanua.
Aliongeza kuwa, yeye baada ya kuchaguliwa na wananchi aliamua kuwachagua wasaidizi wake, sio kwa kujuana wala kuangalia sura bali, ni kwa kumsaidia hivyo kama kwenye ziara hiyo hawashiriki anashindwa kuwafahamu.
“Kiongozi wa chama kwenye utekelezaji wa Ilani hii ya CCM ya mwaka 2015/2020 ana nafasi yake na halikadhalika sisi viongozi wa serikali kama mawaziri tunawajibu wetu mkubwa, lazima tuwepo”,alifafanua.
Akiwasilisha taarifa hiyo ya kikazi, Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Pemba Mhe: Omar Khamis Othman alisema maendeleo makubwa yameshapatikana ndani ya Mkoa huo, ikiwa ni pamoja na maji safi na salama.
Hata hivyo Mkuu huyo wa Mkoa, alimueleza rais huyo wa Zanzibar kuwa, changamoto kubwa inayowakabili katika kuzimaliza kesi za udhalilishaji ni wananchi kutokuwa tayari kutoa ushahidi mahakamani.
“Tumefanikuwa kuunda kamati za mkoa na wilaya juu ya kupinga udhalilishaji, lakini sasa wananchi bado baadhi yao wamekuwa wasugu kushirikiana na vyombo vya kisheria”,alilalmikia.
Aidha alifafanua kuwa, ushirikiano mkubwa uliopo baina ya wananchi na kamati ya ulinzi na usalama August 20, mwaka huu, walikamata kete 560 zinazodhaniwa kuwa dawa za kulevya.
Wakati huo huo, Rais huyo wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe: dk Ali Mohamed Shein, mara baada ya kuweka jiwe la msingi skuli Chimba wilaya ya Micheweni aliwapongea wananchi hao kwa uamuzi huo wa kujenga skuli kwa nguvu zao
Alisema uamuzi wa kujiletea maendeleo ndio unaofaa kuungwa mkono na kuigwa na kila mmoja, kwani maendeleo hasa ya sekta ya elimu inategemea pia nguvu za wananchi.
“Mimi niwapongeze wananchi wa Shehia ya Chimba kwa uamuzi sahihi na adhimu wa kuwajengea watoto wenu skuli ya karibu na sasa masafa ya kilomita sita yatawaondoka”,alieleza.
Hata hivyo Rais huyo wa Zanzibar amemuagiza Mkuu wa Mkoa wa kaskazini Pemba, kuzipitia skuli zote za mkoa huo, na iwapo atabaini kuna waalimu watoro atoe taarifa kwa waziri wa elimu ili wafukuzwe kazi.
“Wapo waalimu kwanza ni watoro skuli na hujifanya wanaumwa, lakini hawaendi hospitali na hujikalia nyumbani na wanakula mshahara, waripoti na kisha wafukuzwe kazi”,alifafanua.
Akisoma risala ya ujenzi huo Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Micheweni Hamad Mbwana Shehe alisema, ujenzi huo wa madarasa matano na ofisi mbili za waalimu, umeshagharimu shilingi million 37.35.
Alisema kati ya fedha hizo shilingi 600,000 ni nguvu za wananchi, shilingi 900,000 ni mchango wa Jumuia ya Maendeleo Tumbe, shilingi 3,500,000 kutoka Halmashauri, wakati mfuko wa jimbo wa mwakilishi na mbunge jimbo la Tumbe umechangia zaidi ya shilingi 31.4 milioni
Aidha amesema kwa sasa wanahitaji zaidi ya shilingi million 17, 534,000 kwa ajili ya milango, madirisha, rangi, dari na vyoo, ili wanafunzi waanze kuitumia.
Rais huyo wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi pamoja na ujumbe wake, utaendelea na ziara yake ya siku tano asubuhi wilaya ya Wete kwa kukagua shughuli mbali mbali za kimaendeleo ikiwa ni pamoja na uzinduzi wa kituo cha afya cha mama na mtoto cha Junguni.

                   


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.