Habari za Punde

NEC Yaagiza Waliopoteza Vitambulisho Kupiga Kura Uchaguzi Mdogo wa Diwani.

NEC-DODOMA
16.10.2017

Tume ya Taifa ya uchaguzi imesema kuwa Wapiga kura waliopoteza vitambulisho vya kupigia kura watapata fursa ya kupiga kura kwenye uchaguzi mdogo wa Madiwani wa Kata 43 unaotarajiwa kufanyika Novemba 26, mwaka huu.

Hayo yamesemwa leo (16.10.2017) na Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Bw. Ramadhani Kailima Mjini Dodoma ikiwa ni siku ya pili ya mafunzo ya siku tatu kwa wasimamizi na wasimamizi wasiadizi wa uchaguzi yanayoratibiwa na kuendeshwa na NEC.

Bw. Kailima amesema wapiga kura hao wataruhusiwa kutumia vitambulisho vya uraia vinavyotolewa na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), Hati ya kusafiria na Leseni ya udereva.

“Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwa kuzingatia kifungu namba 62 (a) cha Sheria ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, ambacho kinasema mpiga kura aliyeandikishwa kwenye daftari atakwenda mwenyewe kwenye Kata aliyojiandikisha na kituo alichopangiwa” Amesema.

Ameeleza kuwa hatua hiyo ni kumridhisha msimamizi wa kituo au msimamizi msaidizi wa uchaguzi kwamba yeye ndiye mpiga kura halali na kuongeza kuwa kifungu hicho kinamtakaMpiga Kura aonyeshekadi yake ya kupigia. Aidha, kinaeleza kwambaTume inaweza ikaelekeza utambulisho mwingine wowote utakao msaidia mpiga kura kuweza kupiga kura iwapo  hana kadi.

Bw.Kailima amesema kuwaTume ya Taifa ya Uchaguzi kwa kuzingatia kifungu hicho, katika uchaguzi mdogo utakaofanyika Novemba 26, 2017 imetoa maelekezo kwa Wasimamizi wa Uchaguzi kuruhusu wapiga Kura waliojiandikisha kwenye Dafatari la kudumu la Wapiga Kura kutumia Hati ya kusafiria, kitambulisho cha Taifa kilichotolewa na NIDA na leseni ya udereva.

Bw. Kailima amesemaruhusa hiyo imetolewa kwa sharti moja kwamba majina na herifu yaliyopo kwenye kitambulisho hicho yafanane na majina na herufi zilizopo kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura.

Ameongeza kuwa NEC itakutana na vyama vya siasa hivi karibuni kuwajulisha juu ya maagizo hayo na kusisitiza kwamba tofauti yoyote itakayo kuwepo kwenye majina itamnyima mpiga kura fursa ya kupiga kura.

Bw. Kailima amesema maamuzi hayo yamefikiwa kutokana na kuwepo kwa changamoto kubwa kwenye daftari la kudumu la wapiga kura ambalo kwa mara ya mwisho liliboreshwa mwaka 2015.

“ Katika kipindi chote hichi (2015-2017) inawezekana kwa namna moja ama nyingine, kuna baadhi ya wapiga kura wamepoteza kadi zao za kupigia kura na kwa sababu hatujaboresha na sheria inasema watapata hizo kadi baada ya daftari kuboreshwa, wanaweza wakakosa fursa ya kupiga kura kwenye uchaguzi wa madiwani wa kata 43, lakini wengine kadi zao zimeharibika kiasi kwamba haziwezi kusomeka, na wengine kadi zao zimechakaa kabisa kwa sababu moja ama nyingine kutokana na mazingira yaliyopo,” amesema.

Wakitoa maoni yao juu ya agizo hilo la NEC, washiriki wa mafunzo hayo wamepongeza hatua hiyo na kusema kwamba itakuza wigo wa demokrasia nchini kwa kuwapa fursa wapiga kura halali ambao kwa sababu zilizoko nje ya uwezo wao wamejikuta hawana kadi za kupigia kura licha ya kwamba ni wapiga kura halali waliojiandikisha.

Bw. Abdul Kasembe ambaye ni Afisa Uchaguzi kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru, Mkoani Ruvuma amesema kuwa amefurahishwa na uamuzi huo akieleza mambo mengi yamejitokeza kati ya mwaka 2015 mpaka sasa.

“Sisi tumefurahia agizo hili kwa kuwa litawapa fursa wananchi ambao pengine wangeikosa fursa kwa kuwa hawana kadi japokuwa wamejiandikisha”.

Bi. MargaretNakayinga, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Urambo, Mkoani Tabora amesema agizo hilo limeleta fursa kwa watu ambao pengine wangekosa fursa ya kupiga kura kwa kupoteza kadi ya kupigia kura au kwa kuharibika kwa kadi zao. Tutakaporudi huko tutawatangazia wananchi ili wajitokeze kwa wingi kupiga kura..”.


Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto, Mkoani Tanga, Bw. Kazimbaya Makwega amesema kuwa agizo hilo ni muafaka na limezingatia mazingira ya Kitanzania kwa kuwa watu wanaweza kupoteza kadi au kuharibikiwa na kadi zao na kukosa fursa ya kupiga kura.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.