Habari za Punde

Uzinduzi wa Umeme Kisiwa cha Fundo Kisiwani Pemba

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, amesema kuwa Serikali imejidhatiti kuzifikisha huduma za umeme katika maeneo yote wanayoishi wananchi kwa kutambua kuwa huduma hizo zinaenda sambamba na maendeleo ya dunia na siyo anasa kama ilivyokuwa hapo zamani.

Dk. Shein aliyasema hayo leo mara baada ya kuzindua umeme katika kisiwa cha Fundo kilichopo Jimbo la Gando, Mkoa wa Kaskazini Pemba ikiwa ni miongoni mwa shamrashamra za kutimiza miaka 54 ya Mapinduzi matukufu ya Januari 12, 1964.

Rais Dk. Shein alisema kuwa ukosefu wa huduma hizo unadumaza juhudi za wananchi katika kujitafutia maendeleo kwani umeme ni msingi wa maendeleo.

Hivyo, Dk. Shein alitoa nasaha zake kwa wananchi wa kisiwa hicho kuongeza kasi, ari na hamasa ya kutafuta maendeleo hasa kwa kujishughulisha na miradi ambayo mwanzo walishindwa kuifanya kwa kukosekana nishati hiyo.

 “Ni jambo la faraja kuona kwamba tumepiga hatua kubwa kufikisha huduma muhimu katika visiwa vidogo vidogo na vijiji vilivyo katika maeneo ya mbali kwani lengo letu ni kuhakikisha kila mwananchi wa Zanzibar popote alipo anapata huduma za umeme, afya, elimu, maji safi na salama na huduma nyenginezo”,alisema Dk. Shein.

Aidha, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa viongozi wote wa Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira pamoja na Shirika la Umeme (ZECO) na Bodi yake kwa kuwa wepesi wa kutekeleza maagizo yake kwa kusimamia vyema Ilani ya CCM ya Uchaguzi kwa kipindi kilichomalizika na kilichopo hivi sasa cha 2015-2020.

Alieleza kuwa hatua hiyo ni utekelezaji wa Ilani hiyo na kutumia fursa ya kukisoma kipengele kinachoelezea utekelezaji huo mbele ya maelfu ya wananchi waliohudhuria katika hafla hiyo kutoka Mikoa na wilaya zote za Pemba.

Pia, Dk. Shein alieleza kufurahishwa kwake kwa kumekuwepo na wataalamu wa hapa hapa Zanzibar ambao wamefanya kazi hiyo kutokana na ujuzi wao na uwezo wa kuufikisha umeme kwenye visiwa kwa kuzipitisha nyaya za umeme chini ya bahari.

Aliwapongeza wananchi wote wa kisiwa cha Fundo kwa kushirikiana na ZECO tangu hatua za mwanzo za utekelezaji wa mradi huo hadi pale umeme ulipoanza kuwaka pamoja na ukarimu na mashirikiano walioyonayo na umoja wao.

Dk. Shein aliongeza kuwa yeye anapotoa ahadi kwa wananchi huwa hasahau kwani anakumbuka wakati akiwa katika Kampeni za Uchaguzi mwaka 2010 akiwa Chanjani Chokocho katika uwanja wa “Black Wizard” aliahidi kuwa kisiwa cha Makongwe na Kisiwa 
Panza ataufikisha umeme ahadi ambayo tayari ameshaitekeleza.

Alieleza kuwa hivi sasa Serikali imeshafikisha umeme katika visiwa saba vya Zanzibar ambapo visiwa hivyo ni Tumbatu na Uzi kwa upande wa Unguja na Kojani, Kisiwa Panza, Makongwe, Mwambe Shamiani na Fundo kwa upande wa Pemba.

Dk. Shein alisema kuwa hivi sasa Serikali inaendelea na visiwa vitatu vilivyobaki ambavyo ni Uvinje, Kokota na Njau vyote vipo Pemba ambapo Serikali imejipanga kufikisha umeme katika visiwa hivyo kabla ya kumalizika mwaka 2020.

Sambamba na hayo, Dk. Shein aliwaleza wananchi wa kisiwa cha Fundo kuwa ameliona tatizo la usafiri wa bahari wanaoupata wananchi wa kisiwa hicho na kuahidi kuwa Serikali italitafuatia muwarubaini wa tatizo hilo.

Pia, alitumia fursa hiyo kueleza historia ya umeme hapa Zanzibar na kusema kuwa Zanzibar ni nchi ya mwanzo kupata huduma hiyo katika nchi za Afrika mashariki na kati na kwa upande wa umeme wa barabarani Zanzibar ulianza kuwaka mwanzo kuliko mji wa London.  

“Umeme huu ni wa kweli na sio umeme feki … natoa pongezi kwa ZECO kwa kuwakopesha wananchi hawa umeme pamoja na kuwapunguzia malipo ya kuwaungia umeme, nasema ahsanteni sana”, alisema Dk. Shein.

Aidha, aliwataka wananchi wa kisiwa cha Fundo kujiandaa kuwa walipaji wazuri wa umeme hasa ikizingatiwa kuwa Srerikali inalipa fedha nyingi kutoka Tanzania Bara unakotoka umeme huo, hivyo kila mmoja aone fahari kulipa kwa wakati na kwa mujibu wa matumizi yake, ili huduma hizo ziweze kupatiakna kwa wote.

Kwa upande mwengine Dk. Shein alitoa indhari kuwa umeme ni hatari na kuwataka wananchi wa kisiwa hicho kuchukua tahadhari wakati wanapoutumia.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alisisitiza kuendeleza umoja wao na mshikamano wao kwani umoja wao na ndio uliopelekea MwenyeziMungu kuwapelekea neema hiyo ya umeme na kuwataka wasihasimiane kwa siasa na kuwataka kuengeza nguvu katika maendeleo huku wakitambua kuwa vyama vya siasa ni sare tu ya dunia.

Nae Waziri wa Ardhi, Maji,Nishati na Mazingira Salama Aboud Talib alimpongeza Dk. Shein kwa kuwa makini katika kutekeleza ahadi anazoziahidi kwa wananchi huku akieleza mashirikiano makubwa yaliopatikana kutoka kwa wananchi.

Mapema Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Alhalil Mirza, alieleza kuwa mradi huo wa usambazaji wa umeme umehusisha ujenzi wa njia kuu za umeme wa kilovolti 33 kutoka Ukunjwi hadi 

Ras Ukunjwi na pia ndani ya kisiwa cha Fundo wenye jumla ya kilomita 7.29.
Uwekaji wa transfoma nne katika vijiji vya Kimeleani, Ngagu, Ndooni na Mabaoni, ujenzi wa  njia ndogo za umeme zenye  jumla ya kilomita 8 na ulazaji wa waya wa bahari wenye urefu wa kilomita 2.5.

Aliongeza kuwa mradi huo umegharamiwa na Searikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa jumla ya TZS Bilioni 2,078,222,518 ambapo kati ya fedha hizo Serikali imetoa Bilioni 1.7 na ZECO imechangia milioni 302.2

Alieleza kuwa kazi ya ujenzi wa umeme mkubwa, umeme mdogo na uwekaji wa transfoma zilimalizika mwezi Aprili, 2017 na kazi ya ulazaji wa waya baharini ilimalizika tarehe 6 Agosti 2017 na kumalizika tarehe 11 Agosti 2017.

Katibu Mkuu huyo alieleza kuwa kazi zote za upelekeaji wa umeme kisiwani humo zimefanywa na kusimamiwa na wataalamu wazalendo wa ZECO huku akieleza kuwa tayari nyumba 340 kati ya nyumba 640 zimeshatiwa umeme kisiwani humo.

Alisema kuwa katika kufikia malengo ya Dira 2020 na MKUZA III Serikali kupitia ZECO imeshafikisha huduma ya umeme kwa asilimia mia moja 100% kwa Shehia zote za Unguja na Pemba ambapo ni sawa na asilimia 91% kwa ngazi ya Vitongoji.

Nao wananchi wa kisiwa hicho walitoa pongezi kubwa kwa Dk. Shein kwa kutimiza ahadi hiyo ya kuwapelekea umeme na kumuombea dua Mungu ampe nguvu zaidi ili azidi kuendelea kuwasaidia wananchi wake anaowaongoza.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.