Habari za Punde

SUZA yatafuta muarubaini ufaulu masomo ya sayansi

 Mkurugenzi Mipango Idara ya Mafunzo ya  Amali, Khalid Masoud Waziri akizindua Warsha ya siku mbili huko chuo cha Walimu Suza katika mradi ulioandaliwa Idara ya Elimu ya kuwawezesha walimu wa sanaa (Art) kuwa Walimu wa sayansi. (Picha na Miza Othman –Maelezo Zanzibar).
 Walimu wakuu, Wasaidizi na Maofisa wa Elimu wa Wilaya za Unguja wakimsikiliza Mgeni Rasmi alipokuwa akizindua Warsha hiyo. (Picha na Miza Othman –Maelezo Zanzibar).
 Mkurugenzi  Khalid Masoud  akiwa katika picha ya pamoja na Wahadhiri wa (SUZA), Walimu wakuu na wasaidizi wa Skuli za Unguja na Maofisa wa Elimu wa Wilaya. (Picha na Miza Othman –Maelezo Zanzibar).
Waandishi wa Habari wakipata Maelezo kutoka kwa Mkuu wa Divisheni ya Vituo vya Ualimu  Maulid Omar Hamad  wakati wa mafunzo ya walimu wakuu na wasaidizi wao yanayoendelea katika ukumbi wa chuo kikuu cha Walimu-SUZA. (Picha na Miza Othman –Maelezo Zanzibar).


Na Bahati Habibu - Maelezo  Zanzibar.                  

Walimu Wakuu wa skuli mbalimbali za Zanzibar, wametakiwa kuwafuatilia vyema walimu walio chini yao ili kuhakikisha ufaulu mzuri katika masomo ya sayansi.

Akizindua warsha ya kuwabadilisha walimu wa masomo ya sanaa kuwa wa sayansi iliyofanyika katika Chuo Kikuu cha Taifa (SUZA) kampasi ya Nkrumah, Mkurugenzi Mipango Idara ya Mafunzo ya Amali  Khalid Masoud Waziri, amesema iko haja kwa walimu kubadilika ili kufikia malengo ya wizara.

Alieleza kuwa walimu wanapaswa kuhakikisha idadi ya wanafunzi wanaofaulu masomo ya sayansi, hesabati na Kiingereza inaongezeka ili kuwajengea mazingira ya kuhimili soko la ajira kwa sasa.

Katika warsha hiyo ya siku mbili kupitia mradi ulioandaliwa na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali chini ya usimamizi wa Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA), Mkurugenzi huyo alisema taasisi nyingi zinapotoa ajira mpya, huangalia zaidi vijana wanaofaulu vizuri masomo ya sayansi kulingana na mahitaji yao.

Nae Mkurugenzi wa Idara ya Mafunzo ya Walimu Salha Said, amewasisitiza walimu kuyafanyia kazi mafunzo watakayopata ili waweze kwenda sambamba na sera ya Serikali ya Viwanda na Masoko kwa kuwaandaa wanafunzi mapema ili taifa lipate wanasayansi walio bora kwa maendeleo.

Ili kufikia lengo hilo, amewataka Walimu Wakuu, Wasaidizi na Maofisa wa Elimu Wilaya za Unguja, kuongeza ushirikiano katika kuhakikisha walimu wanatumia mbinu zilizo bora za ufundishaji katika masomo hayo.

Dk. Maryam Jaffar Ismail, Mshauri Elekezi wa mradi huo, pia amesema, ili kuongeza ufaulu wa wa wanafunzi, ipo haja kwa walimu kupatiwa mafunzo ya lugha ya Kiingereza ambayo ndiyo inayotumika katika ufundishaji wa masomo ya Sayansi na Hesabati.

“Tafauti na ilivyo sasa, walimu wengi wanatumia lugha ya Kiswahili kwa asilimia 98 katika kufundisha masomo ya sayansi, hali inayosababisha wanafunzi wasifaulu vizuri kwa kuwa mitihani huandikwa kwa Kiingereza,” alisema Dk. Maryam.

Aidha, alisema kupitia mradi huo, wanapanga kuwaandalia zawadi walimu na wanafunzi watakaofanya vizuri katika masomo hayo.

Mradi huo wa miaka minne, utahusisha uandaaji wa vitabu vya Sayansi na Hesabu pamoja na lugha ya Kiingereza, na kuwapa mbinu mbalimbali walimu ili kuongeza kiwango cha ufaulu wa daraja la juu kwa wanafunzi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.