Habari za Punde

Rais Dk Shein akutana na kufanya mazungumzo na ujumbe wa madaktari kutoka China

 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akisalimiana na Mkurugenzi wa Nanjing Drum Tower Hospital Bw.Han Guangshu wakati alipofika Ikulu Mjini Zanzibar  leo akiongoza timu ya Madaktari kutoka China,[Picha na Ikulu.]05/04/2018.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa bAraza la Mapinduzi Dk Ali Mohamed Shein akizungumza na timu ya Madaktari kutoka China inayoongozwa na Mkurugenzi wa nanjing Drum Tower hospital Bw.Han Guangshu wakati alipofika Ikulu Mjini Zanzibar  leo

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akizungumza na Mkurugenzi wa Nanjing Drum Tower Hospital Bw.Han Guangshu (kushoto) wakati  alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo akiongoza timu ya Madaktari kutoka China (hawapo pichani),[Picha na Ikulu.]05/04/2018.


STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                        05.04.2018
---
HOSPITALI ya Drum Tower ya Mjini Naijing katika Jimbo la Jiangsu ya nchini China imeahidi kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta ya afya.

Rais wa Hospitali hiyo Han Gungshu akiwa na ujumbe wake wa madaktari kutoka nchini China aliyasema hayo leo wakati alipokuwa na mazungumzo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, Ikulu Mjini Zanzibar.

Katika maelezo yake, Kiongozi huyo ambaye yupo Zanzibar kwa lengo la kuendeleza mashirikiano na mahusiano mema katika sekta ya afya kati ya Serikali ya China na Zanzibar, alieleza kuwa Hospitali hiyo itaendeleza mashirikiano na hospitali za Zanzibar ikiwemo hospitali ya Mnazi Mmoja.

Alieleza kuwa tayari mipango kabambe imeshaandaliwa katika kuanzisha programu mbali mbali kati ya Hospitali hiyo na hospitali ya MnaziMmoja ikiwa ni pamoja na kuanzisha huduma za saratani ya mlango wa kizazi.

Aliongeza kuwa huduma hiyo itatolewa kwa wananchi wa Unguja na Pemba wa mjini na vijijini kwa lengo la kuhakikisha maradhi hayo yanatokomezwa kwa akina mama wa Zanzibar.

Gungshu alimueleza Rais Dk. Shein kuwa Hospitali hiyo iko tayari kutoa ushirikiano wake katika kuendeleza huduma za afya hapa Zanzibar kwa kushirikiana na madaktari wa hapa nchini kwa kuanzisha programu mbali mbali za tiba ambazo zitatoa huduma kwa wananchi wa Zanzibar.

Aidha, kiongozi huyo alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa Jimbo hilo litaendeleza utamaduni wake wa kuleta madaktari kwa awamu hapa Zanzibar ambao wataendelea kufanya kazi za kutoa huduma za afya kwa wananchi wa Unguja na Pemba.
Pamoja na  hayo, kiongozi huyo alimueleza Rais Dk. Shein kuwa mashirikiano zaidi yataendelezwa kati ya hospitali hiyo na hospitali za hapa Zanzibar ikiwa ni pamoja na kuendeleza programu za rasilimali watu katika kada mbali mbali.

Kiongozi huyo ambaye mama yake mzazi aliwahi kufanya kazi katika hospitali Kuu ya MnaziMmoja mnamo miaka ya 70, alisifu mashirikiano wanayopata madaktari kutoka nchini China kutoka kwa wananchi wa Zanzibar hali ambayo huwafanya madaktari hao nao kuzidisha mapenzi na utoaji huduma za afya kwa ndugu zao wa Zanzibar.

Nae Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein alimpongeza kiongozi huyo pamoja na hospitali hiyo ya Drum Tower ya Mjini Naijing katika Jimbo la Jiangsu ya nchini China kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta ya afya.

Katika mazungumzo hayo, Dk. Shein alisema kuwa Jimbo la Jiangsu limekuwa na utamaduni wa kushirikiana na Zanzibar katika kuimarisha sekta ya afya kwa muda mrefu ambapo tokea mwaka 1965 lilianza kuleta madaktari hapa Zanzibar.

Aidha, Rais Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo juhudi za makusudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha sekta ya afya na kusisitiza haja ya kuendelea kuungwa mkono na Hospitali hiyo pamoja na Jimbo lake.

Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo azma ya Serikali kuanzisha kitengo cha upasuaji wa moyo na kueleza haja ya mashirikiano kati ya pande mbili hizo ili kuimarisha sekta ya afya hapa Zanzibar huku akipongeza azma ya hospitali hiyo ya kuanzisha huduma za saratani ya mlango wa kizazi kwa mashirikiano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo juhudi zinazochukuliwa na Serikali anayoiongoza katika kutoa mafunzo ya udaktari ndani na nje ya Zanzibar ikiwa ni pamoja na kuanzisha Skuli ya Udaktari katika Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA).

Kutokana na juhudi hizo,Dk. Shein alieleza haja kwa hospitali hiyo kuendeleza ushirikiano wake kwa kutoa nafasi za masomo katika fani mbali mbali za udaktari wakiwemo madaktari wa meno ili kuondosha kabisa uhaba wa madaktari bingwa katika Hospitali Kuu ya Mnazi Mmoja na Hospitali ya Abdala Mzee pamoja na kuleta madaktari watakaosomesha fani mbali mbali za udaktari katika Chuo hicho.

Pia, Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Serikali ya China chini ya kiongozi wake Rais Xi Jingpig kwa msaada wake mkubwa kwa kuifanyia matengenezo makubwa Hopsitali ya Abdalla Mzee sambamba na kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta  mbali mbali za maendeleo ikiwemo sekta hiyo ya afya hapa Zanzibar.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.