Habari za Punde

Serikali yazindua rasmi sera ya Diaspora ya Zanzibar


Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi leo imezindua rasmi sera ya Diaspora ya Zanzibar yenye lengo la kujenga mazingira yatakayowaezesha wanadiaspora kushiriki na kuwafanya waweze kutoa mchango wao kwa maendeleo ya Zanzibar.

Akizungumza katika hafla maalum ya uzinduzi wa sera hiyo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mheshimiwa Issa Haji Ussi Gavu, amesema kuweko kwa sera hiyo hivi sasa kutaiwezesha Serikali kuchukua hatua mbali mbali za kisekta ambazo zitaelezea na kutoa maelekezo kuhusiana na masuala muhimu ya Diaspora na maendeleo ya Zanzibar.

Amefahamisha kuwa kufuatia uzinduzi huo, Serikali hivi sasa itakuwa na fursa nzuri ya kuwashajihisha Wanadiaspora wote kushiriki katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi, sambamba na kuainisha fursa na wajibu wa wanadiaspora wa Zanzibar popote walipo.

Katika utekelezaji wa sera hiyo, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar itaijengea uwezo Idara inayoshughulikia masuala ya Diaspora kwa kuipatia wataalamu, nyenzo za kutekeleza majukumu yake pamoja na kuifanya kuwa kituo muhimu cha kupata taarifa zinazohusiana na masuala ya Diaspora.

Vile vile Mheshimiwa Gavu amesema kuzinduliwa kwa sera hiyo kutaiwezesha Serikali kusimamia kikamilifu taarifa zinazohusiana na masuala ya Diaspora na kuwashirikisha rasmi wanadiaspora kwa lengo la kurahisisha kujenga imani na kuimarisha mashirikiano kati yao na Serikali.

Aidha, Serikali kupitia sera hiyo inakusudia kutumia taaluma na ujuzi wa wanadiaspora kwa maendeleo ya Zanzibar na kuratibu masuala ya utumaji wa fedha kutoka kwa wanadiaspora kwani amesema, fedha hizo zinachangia sehemu kubwa katika jitihada za maendeleo.

Sambamba na hatua hiyo, Serikali itawatumia wanadiaspora katika jitihada za Uwekezaji Vitega Uchumi pamoja na kuimarisha sekta ya Utalii ambayo imekuwa ikitoa mchango mkubwa katika kuchangia pato la taifa.

Hafla hiyo ambayo ilifanyika katika ukumbi wa zamani wa Baraza la Wawakilishi uliopo Kikwjuni Mjini Zanzibar, ilihudhuriwa pia na Katibu Mkuu Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Salum Maulid Salum, Wanadiaspora wa Zanzibar na Waandishi mbali mbali wa habari waliopo Zanzibar.

Akimkaribisha Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Salum Maulid Salum amesema kuzinduliwa kwa sera hiyo ni matunda ya jitihada za muda mrefu za Serikali ya Mapinduzi Zanzibar katika kujenga mafahamiano mazuri kati ya Serikali na Wanadiaspora.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.