Habari za Punde

Tatizo la Maji Jumbi Kupatiwa Muarubaini Wake. Mwakilishi wa Jimbo la Tunguu Akabidhi Mipatra ya Kusambazia Maji Safi na Salama.

Mwakilishi wa Jimbo la Tunguu Zanzibar Mhe. Simai Mohammed Said akikabidhi mipira ya kusambazia maji kwa Wananchi wa Kijiji cha Jumbi Meli Nane, kwa Kamati ya Maendeleo ya Jimbo hilo,Hafla hiyo imefanyika katika Tawi la CCM Jumbi Wilaya ya Kati Unguja Mkoa wa Kusini Unguja.
KATIBU Kamati ya Maendeleo Jimbo la Tunguu Ramadhan Haji Ameir akitoa shukurani zake kwa niaba ya Wananchi wa Jumbi meli nane juu ya Misaada wanayopatiwa na Mwakilishi na Mbunge wa Jimbo hilo.
MWENYEKITI wa Tawi la CCM Jumbi meli nane Joram Anton Magaruka akizungumza katika makabidhiyano  hayo.(Picha na Abdallah Omar -Maelezo Zanzibar)
Na Salum Vuai
WANANCHI wa shehia ya Jumbi iliyoko jimbo la Tunguu Wilaya ya Kati, sasa watashusha pumzi baada ya tatizo la uhaba  wa maji linalowakabili kwa muda mrefu kupata muarubaini wake.

Afueni hiyo imekuja baada ya viongozi wa jimbo la Tunguu kukabidhi mipira mitatu ya kusambazia maji katika maeneo ya wadi hiyo.

Mipira hiyo iliyokabidhiwa juzi na Mwakilishi wa jimbo hilo Simai Mohammed Said katika tawi la CCM Jumbi, imegharimu shilingi 2,500,000.

Akitoa shukurani zake kwa niaba ya wananchi wa Jumbi, Katibu wa kamati ya maendeleo Ramadhan Haji Ameir, alisema upatikanaji wa mipira hiyo utawakomboa zaidi akinamama ambao kimsingi ndio wanaohangaika.

Alieleza kuwa kwa sasa wamekuwa wakitumia maji ya kisima ambayo hayana uhakika wa usalama kiafya, na pale wanapohitaji ya bomba hulazimika kwenda masafa ya mbali.

“Angalau sasa wananchi wa shehia ya Jumbi tutanenepa na tutafanya shughuli zetu kwa utulivu kwani shida ya maji imekuwa ikichukua muda wetu mwingi na kutuchosha sana,” alisema.

Aliwashukuru Mwakilishi, Mbunge pamoja na diwani wa wadi ya Tunguu kwa juhudi kubwa  wanayochukua kutekeleza kwa vitendo Ilani ya Chama cha Mapinduzi.

Sheha wa shehia ya Jumbi Muhidini Haji Machano, alisema hatua hiyo imeleta faraja kwao kwani imeongeza nguvu baada ya wananchi kuanza kutafuta mipira miwili kati ya mitano iliyokuwa ikihitajiwa.

Hata hivyo, aliwaomba wakaazi wa shehia yake hasa vijana kujitokeza kwa wingi kufanya kazi ya kuchimba misingi kwa ajili ya kulaza mipira hiyo, ambayo alisema inatarajiwa kuanza mara moja.

“Tulichokuwa tukikitaka tayari tumekipata, sasa ni juu yetu kuonesha mshikamano ili tuanze kazi na kuimaliza kwa haraka. Ninawaambia vijana hakuna kulala,” alisisitiza Sheha huyo.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Tunguu Simai Mohammed Said kwa niaba ya Mbunge na diwani, alieleza kuwa dhamira yao kuu ni kuhakikisha kero ya maji katika jimbo lote linabaki kuwa historia.

Alisema mchakato wa kuzipatia ufumbuzi changamoto zinazolikabili jimbo hilo zitakuwa endelevu ili kuwawezesha wananchi kuishi maisha yaliyo bora kwa kuwapa unafuu katika upatikanaji wa huduma muhimu hasa maji safi na salama.

“Tunaelewa sasa ujenzi wa miji mipya ya Jumbi na Tunguu umeshika kasi, bila shaka kuna haja ya kusambaza maji na huduma nyengine za msingi kwa wakaazi wote. Tutaendelea kuunganisha nguvu katika kulifanikisha jambo hili,” alieleza Mwakilishi huyo.

Aidha, aliwashukuru wananchi wote wa Jumbi na jimbo zima la Tunguu kwa ushirikiano wanaowapa viongozi wao, akisema ndio unaowaongezea nguvu za kuwatumikia kwa ufanisi.      

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.