Habari za Punde

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Atembelea Msitu wa Itigi 'ITIGI THICKETS'


Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. January Makamba akisalimiana na Bw. Khatib Ally mmoja wa wananchi waliojitokeza kumpokea katika Kijiji cha Aghondi Wilayani Manyoni, Mkoani Singida. Waziri Makamba ametembelea eneo hilo ambalo lina vichaka vya aina yake na vyakipekee barani Afrika. Wananchi wa eneo hilo wamewasilisha ombi kwa Waziri Makamba la kuweka ulinzi wa kutosha na namna bora ya kuhifadhi eneo hilo.


Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. January  Yussuf Makamba ,akimsikiliza Mwananchi anayeshughulikia na uhifadhi wa msitu wa hifadhi ya vichaka vya Itigi, huutumia msitu huo kwa ufugaji wa nyuki na kuvuna asili nyingi kupitia msitu huo.
Sehemu ya vichaka adimu duniani vinavyopatikana Itigi, “Itigi thickets” katika bara la Afrika vichaka kama hivyo vinapatikana Tanzania na Zambia pekee, viko hatarini kutoweka kutoweka kutokana  na shughuli za kibinadamu.
Na.Lulu Mussa. 
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mheshimiwa January Makamba hii leo amehitimisha ziara yake ya kikazi katika Mkoa wa Singida na kuwasili katika Mkoa wa Tabora, ikiwa ni mwendelezo wa kukagua, kutathmini, kuzungumza na viongozi, na wananchi kuhusu maeneo yanayopendekezwa kuhifadhiwa kwa mujibu wa Sheria ya Mazingira, sambamba na uanzishwaji na ufuatiliaji utekelezaji wa Sheria ya Usimamizi Mazingira ya mwaka 2004 katika ngazi za Serikali za Mitaa.

Katika siku ya tatu ya ziara yake Mhe. Makamba ametembelea vichaka vya Itigi ‘Itigi thicket” na kupata fursa ya kuzungumza na viongozi wa wilaya ya Manyoni juu ya namna bora ya kuhifadhi eneo hilo lenye ukubwa wa hekta 410,000 na kuahidi kutuma wataalamu kuandaa andiko la Mradi utakaonufaisha wakazi wa eneo hilo katika sekta uvunaji wa asali kwa njia ya kisasa zaidi.

“Ndani ya muda mfupi nitatuma wataalamu wangu kutoka Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira NEMC, waje wakae na wataalamu wenu na kuandaa Mradi utaonufaisha wakazi wa wanaozunguka eneo lote la msitu ili kutunza na kuhifadhi rasilimali za asili zilizopo katika eneo hili” Makamba alisisitiza.

Katika hatua nyingine Waziri Makamba amemtaka Mkuu wa Wilaya ya Manyoni Bi. Rahabu Jackson kuwasilisha kwake majina wa watalaamu wa Mazingira ambao wana sifa za kuwa Wakaguzi wa Mazingira ili waweze kuteuliwa kwa mujibu wa Sheria.

Pia, ametoa wito wa Halmashauri kuingia makubaliano na Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) ili kukasimu mamlaka kisheria ya kukagua na kusimamia masuala ya mazingira kwa msukumo zaidi.

Vichaka vya Itigi huwa na urefu wa mita 2-5 na katika Bara la Afrika vinapatikana Tanzania na Zambia pekee vinawakilisha bioanuani ya kipekee duniani yenye umuhimu kitaifa na kimataifa na uoto wake ni  muhimu kwa mustakabali wa maisha ya binadamu na wanyamapori.

Imebainika kuwa vichaka vya Itigi viko hatarini kutoweka kutokana na shughuli za kibinadamu kama vile kilimo cha kuhamahama, uchungaji wa mifugo, uchomaji wa mkaa, uvunaji wa mazao ya misitu na uchimbaji wa madini. Hivyo kuna haja ya kuchukua hatua za haraka kuhakikisha uhifadhi endelevu wa vichaka vya Itigi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.