Habari za Punde

Waziri Gavu Afungua Mafunzo ya Siku 10 ya Mapishi na Ukarimu Kwa Wahudumu wa Viongozi na Wageni Zanzibar..

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Issa Haji Gavu akifungua Mafunzo ya Siku Kumi kwa Wahudumu wa Viongozi na Wageni Zanzibar, Mafunzo hayo Yanatolewa na Wakufunzi kutona Taasisi ya China Natinal Research Institute of Food and Fermentation Industries Corporation Ltd.(CNRIFFI) uzinduzi huo umefanyika katika Ukumbi wa Sheikh Idrisa Abdulwakil Kikwajuni Zanzibar.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amepongezwa kwa juhudi anazoendelea kuzichukua katika kuhakikisha Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inakuwa na wataalamu na nguvu kazi yenye ujuzi na inayokwenda sambamba na mahitaji na mabadiliko ya karne ya 21.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Issa Haji Ussi Gavu alitoa pongezi hizo katika hotuba yake ya ufunguzi wa mafunzo ya Mapishi na Ukarimu yanayoendeshwa na wakufunzi kutoka China, hafla iliyofanyika katika ukumbi wa Sheikh Idrisa Abdulwakil, Kikwajuni mjini Zanzibar.

Katika maelezo yake, Waziri Gavu alieleza kuwa juhudi za Rais Dk. Shein zinafahamika katika kuhakikisha kwamba kunakuwepo ushirikiano mzuri kati ya Zanzibar na Washirika wa maendeleo katika suala zima la utoaji wa mafunzo na kuwajengea uwezo wafanyakazi katika sekta zote muhimu za kiuchumi na kijamii hapa nchini.

Alitumia fursa hiyo kutoa shukrani kwa Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China kwa kukubali kuendelea kutoa mafunzo hayo kwa kuzingatia ombi maalum kutoka kwa Rais Dk. Shein mara baada ya kufanya mazungumzo na Balozi Mdogo wa China aliyepo Zanzibar Xie Xiaowu.

Alisema kuwa mafunzo hayo ni miongoni mwa matunda ya jitihada za Rais Dk. Shein na kila mmoja anathamini sana fursa hiyo inayotokana na juhudi zake katika kuwajengea uwezo wafanyakazi.

Waziri Gavu aliwaeleza washiriki wa mafunzo hayo wkamba wanaunga mkono kwa ukamilifu, maamuzi na makubaliano yaliyofikiwa na viongozi wa pande zote mbili ya kuendesha mafunzo hayo hapa Zanzibar ili kuweza kutoa fursa ya kushiriki watendaji wengi zaidi kwa mkupuo mmoja.

Aliongeza kuwa mwaka huu wa 2018 wapo washiriki 50 na mwaka jana 2017 mafunzo hayo yalishirikisha watendaji 30 hali ambayo ni ya kupiongezwa na inaonesha mafanikio makubwa kwa kuendesha mafunzo hayo hapa Zanzibar ambapo itawapa fursa ya kufahamu masuala watakayofundishwa katika mazingira ya nyumbani waliyoyazoea na wanayoyafanyia kazi.

Aidha, Waziri Gavu alitoa shukurani za dhati kwa Taasisi ya “China National Research Institute of Food and Fermentation Industries Corporation Ltd” kwa kuendeleza ushirikiano mzuri uliopop baina ya Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na  hatimae kukubali kuja tena hapa Zanzibar kwa ajili ya kuendesha na kusimamia mafunzo.

“Jamhuri ya Watu wa China na Zanzibar zina uhusiano wa kihistoria na kidugu, tuna jukumu la kuhakikisha kwamba ushusiano huo unalindwa na kuendelezwa...njia moja ya kufanya hivyo ni kuhakikisha kwamba tunashiriki vizuri katika mafunzo haya na tunawapa wenzetu hawa mashirikiano yanayohitajika”,alisema Waziri Gavu.

Sambamba na hayo, Waziri Gavu aliwataka washiriki wa mafunzo hayo kujua kwamba wana jukumu la kutoa huduma moja kwa moja kwa viongozi, wageni na watalii au kutoa mafunzo kwa wanafunzi wanaotarajia kwenda kutoa huduma za aina hiyo baada ya mafunzo yao.

Aliwahimiza kuzingatia kwa umakini mkubwa mambo watakayofundishwa ili waweze kwenda kuyatekeleza mambo hayo kivitendo katika sehemu zao za kazi huku wakijiamini kwa kutoa michango na kuuliza masuali kila wanapohisi hawajafahamu au wanapoona ipo haja ya kufanya hivyo kwa faida ya washiriki wengine.

Nae Balozi Mdogo wa China anayefanya kazi zake hapa Zanzibar Xie Xiaowu alitoa pongezi kwa kufunguliwa mafunzo hayo na kueleza kuwa China itaendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuendeleza sekta mbali mbali za maendeleo yakiwemo mafunzo ya ndani na nje ya nchi.

Alieleza kuwa Chuo hicho kinachotoa mafunzo hayo kimeanza zoezi hilo kwa nchi zinazoendelea tokea mwaka 2005 na kueleza kuwa tayari wameshaendesha mafunzo kwa watu wapatao 4600 kutoka nchi 133 zinazoendelea hadi mwishoni mwa Agosti mwaka huu 2018.

Balozi huyo alitumia fursa hiyo kwa kutoa pongezi kwa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa kusimamia vyema mafunzo hayo.

Pamoja na hayo, Balozi Xie alieleza kuwa Rais wa China Xi Jinping katika mkutano wa Beijing hivi karibuni aliahidi kuendelea kuziunga mkono nchi za Afrika katika kuendeleza sekta mbali mbali za maendeleo ambapo hatua hiyo ni miongoni mwa ahadi hiyo.

Akizungumza katika hafla hiyo ya ufunguzi wa mafunzo hayo Msaidizi wa Rais wa Taasisi ya “Cina National Research Institute of Food and Fermentation Industries Corporation Ltd” Bi Luo Yanqin alisema kuwa kutokana na Zanzibar kutegemea zaidi sekta ya utalii katika uchumi wake, mafunzo hayo yanamsaada mkubwa katika kuimarisha sekta hiyo hapa nchini.

Kiongozi huyo wa Taasisi hiyo alieleza kuwa mafunzo hayo sio tu yatasaidia kupata uwelewa juu ya utoaji wa huduma katika hoteli, ofisi na nyumba za viongozi lakini pia yatajenga daraja la kuimarisha uhusiano wa kihistoria uliopo kati ya Zanzibar na China.

Washiriki wa mafunzo hayo, wametoka Ofisi mbali mbali za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, ikiwemo Ikulu na nyumba za makaazi ya Rais wa Zanzibar za Unguja, Pemba, Dar-es-Salaam na Dodoma, Ofisi ya Baraza la Mapinduzi, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, nyumba za viongozi wastaafu, walimu kutoka Taasisi ya Utalii ya Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA), ambayo inatoa mafunzo ya mapishi na uakarimu, Mamlaka ya Viwanja vya Ndege pamoja na Hoteli ya Verde.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.