Habari za Punde

Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Mhe.Riziki Pembe Juma Aendelea na Ziara Yake Kisiwani Pemba.



WAZIRI wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Mh. Riziki Pemba Juma akizungumza na Walimu Wakuu wa Skuli za Sekondari Kisiwani Pemba katika ukumbi wa Skuli ya Sekondari Madungu Chake chake Pemba.


Na. Suleiman Juma
WAZIRI wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Mh. Riziki Pembe Juma amewataka Walimu Wakuu wa skuli za sekondari kisiwani Pemba kuendelea kushirikiana zaidi na wazazi katika kuhakikisha ufaulu mkubwa wa wanafunzi unaongezeka.

Mh. Riziki ameyasema hayo wakati akizungumza na walimu wakuu wa skuli za Sekondari kisiwani Pemba katika ukumbi wa skuli ya sekondari Madungu.

Alisema, ufaulu wa wanafunzi unakwenda sambamba na upatikanaji wa ushirikiano wa dhati kati ya walimu na wazazi wa wanafunzi.

Mh. Waziri alieleza kuwa, hivi sasa wazazi wamekua na muitiko mkubwa na wa dhati kuunga mkono jitihada mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuboresha sekta ya elimu nchini.

“Tuendelee kuzidisha mashirikiano baina yetu na wazazi wenzetu katika kulipeleka mbele jahazi la elimu kwani sote ni wasimamizi na tutakwenda kuulizwa kile ambacho tunakisimamia”. alieleza.

Hata hivyo aliwapongeza walimu hao  kwa kazi kubwa wanayoifanya kuhakikisha kiwango cha ufaulu kinaongezeka kwa kasi kubwa kila mwaka nchini licha ya changamoto mbalimbali zinazoikabili sekta hiyo.

Mapema akimkaribisha mgeni rasmi katika mkutano huo Katibu Mkuu Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Dk. Idrisa Muslim Hija alieleza kuwa, serikali inajivunia mafanikio makubwa yaliyotokana na jitihada za walimu hao kwani kila mwaka kiwango cha ufaulu kwa wanafunzi kimekua kikiridhisha.

Akitoa nasaha zake kwa walimu wakuu hao, Afisa Mdhamini Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Nd. Mohamed Nassor Salim alisema walimu wanalo jukumu kubwa la kuwafundisha wanafunzi kwa nia thabiti wakizingatia jicho la serikali linawaangalia walimu katika kuifanya jamii kuwa na maadili na uzalendo wa Taifa lao.

Aidha, aliwataka walimu kutofanya biashara wakati na muda wa kazi ili waweze kufundisha kwa umakini na umahiri mkubwa.   

Nao, walimu hao walieleza changamoto zinazowakabili ikiwemo upungufu mkubwa wa walimu wa masomo ya sayansi katika skuli mbalimbali za sekondari kisiwani humo.

Hata hivyo, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Mh. Riziki Pemba Juma aliwataka walimu wakuu hao kupeleka taarifa za walimu wa sayansi ambao hawajaajiriwa ili changamoto hiyo ipate kutatuliwa haraka.

Katibu Mkuu Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Dk. Idrisa Muslim Hija akimkaribisha Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Mh. Riziki Pembe Juma kuzungumza na Walimu Wakuu wa skuli za sekondari kisiwani


Walimu Wakuu wa skuli za sekondari kisiwani wakipokea nasaha kutoka kwa WAZIRI wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Mh. Riziki Pemba Juma katika Ukumbi wa Skuli ya Sekondari Madungu Chake Chake Pemba.
(Picha na Ali Othman - Pemba)



No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.