Na Mwandishi Wetu,MAELEZO DAR ES SALAAM 17.2.2020
Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Magufuli amewataka Viongozi wote wa Serikali waliochukua fedha za
mpango wa kunusuru kaya maskini nchini kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii
(TASAF) na kuzitumia isivyo sahihi kuzirejesha mara moja kwani serikali haipo
tayari kuona fedha hizo zikitumika kinyume na malengo yaliyowekwa.
Akizngumza
katika hafla ya uzinduzi wa Kipindi cha Pili cha Awamu ya Tatu ya Mpango wa
Kunusuru Kaya Maskini wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) leo Jumatatu
(Februari 17, 2020) Jijini Dar es Salaam, Rais Magufuli alisema katika zoezi la
Serikali ilibaini changamoto mbalimbali katika mfuko huo ikiwemo malipo kwa
kaya hewa nchini.
Rais
Magufuli alisema kupitia zoezi la uhakiki wa kaya masikini lililofanyika
kuanzia Novemba 2015 hadi Juni 2017, Serikali iliweza kubaini uwepo wa kaya
hewa 73,651 ambapo kaya 22034 zilithibitika kuwa wanakaya wake si masikini,
kaya 18,700 ambazo hazikujitokeza mara mbili kupokea ruzuku na kaya 9903
zilizohamia vijiji/ mtaa/shehia ambapo mpango haujaanza.
‘’Mkuu
wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda naye pia anasema aliwahi kunufaika na
TASAF na alisema alizitumia katika safari yake ya kwenda Dodoma katika masuala
yake, sasa naomba fedha hizo uzirudishe mara moja kama ulizitumia katika
matumizi hayo uliyoyasema’’ alisema Rais Magufuli.
Aidha
Rais Magufuli alizitaja Halmashauri 10 zilizoathirika zaidi na kaya hewa ni
Songea Manispaa (2,991), Chamwino (1,840), Kinondoni (1,538), Ilala (1,476),
Moshi Manispaa (1,071), Arusha Mjini (851), Temeke (2,012), Dodoma Mjini
(1,334), Buhigwe (862) na Morogoro (954), na kuongeza kuwa hiyo ni aibu sana
kwa viongozi wa Mikoa, Wilaya na Halmashauri hizo.
Aliongeza
kuwa zipo baadhi ya halmashauri 10 zilizojitahidi kudhibiti vitendo vya kaya
hewa na kuwa na iidadi ndogo ya kaya hewa na kuzitaja halmashauri hizo ni
pamoja na Pangani (149), Kilolo (211), Unguja (242), Igunga (76), Mtwara
Mikindani (25), Rorya (207), Mkinga (140), Babati Mji (45), Geita Mjini (56) na
Chunya 140.
Kwa
mujibu wa Rais Magufuli alisema mara baada ya Serikali kubaini kasoro na
changamoto zilizojitokeza awali, katika kipindi cha pili cha Awamu ya tatu ya
TASAF (2020-2023) Serikali imekusudia kupunguza kiasi cha ruzuku kutoka
asilimia 67 hadi 38, ambapo ruzuyku hiyo itatolewa kwa wazee wasiojiweza,
watoto wadogo na kwa watu wenye kiwango kikubwa cha ulemavu.
‘’Awamu
hii mpya tumepanga kuitekeleza katika halmashauri zote 185 na Wilaya 11 za Zanzibar
na asilimia 60 ya fedha, sawa na shilingi trilioni 1.22 zitatumika kutekeleza
miradi ya maendeleo takribani 30,000 kwenye vijiji na mitaa 16,596 Tanzania
Bara na shehia 388 kule Zanzibar’’ alisema Rais Magufuli.
Aliitaja
miradi hiyo ni pamoja na sekta ya afya (Tsh Bilioni 121.736), elimu (Tsh.
Bilioni 365.209), maji Tsh (Bilioni 585.937), barabara (Tsh Bilioni 49.668) na
mazingira (Tsh Bilioni 96.416), ambapo katika kutekeleza miradi hiyo kipaumbele
kitatolewa kutoka kwa watu wenye nguvu wanaotoka kwenye kaya maskini, ambapo
Serikali inatarajia kuzalisha ajira na kuwapatia ujuzi pamoja na stadi za kazi
watu wapatao milioni 1.2.
Kwa
upande wake Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na
Utawala Bora), George Mkuchika alisema katika kipindi cha pili cha Awamu ya
Tatu ya TASAF, Serikali imejipanga kuhakikisha kuwa changamoto zote
zilizojitokeza katika awamu ya kwanza zinapatiwa ufumbuzi ikiwemo kufikia
asilimia 30 ya kaya zilizobaki katika maeneo yote nchini.
Anaongeza
kuwa kipindi cha kwanza cha Awamu ya tatu ya TASAF iliyoanza kutekelezwa
kuanzia mwaka 2013 imekamilika Desemba mwaka 2019, ambapo asilima 70 ya
walengwa wote wamenufaika na mfuko huo kwa kuwawezesha wananchi wa kipato cha
chini kuweza kubuni miradi iliyowawezesha kujikwamua kiuchumi.
Waziri
wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Mohamed Abood Mohamed alisema
utekelezaji wa miradi ya TASAF umekuwa ni wenye mafanikio makubwa kwa upande wa
Zanzibar ambapo katika awamu ya kwanza iliyoanza mwaka 200-2005 jumla ya miradi
75 iliyogharimu kiasi cha Tsh Bilioni 3 ilitekelezwa na Serikali.
Akizungumza
katika hafla hiyo, Rais Rais wa Zanzibar, Dkt. Ali Mohamed Shein katika hotuba
yake iliyosomwa Naye Makamu wa Pili wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar,
Balozi Seif Ali Idi alisema wananchi wa Zanzibar wamenufaika kwa kiasi kikubwa
na miradi ya TASAF ambapo kwa sasa wananchi kutoka ndani na nje ya nchi,
wamefika Zanzibar kwa ajili ya kujifunza mafanikio hayo yaliyopatikana.
Dkt.
Shein alisema Serikali ya Mapinduzi Zanzibar itaendelea kutoa ushirikiano na
wadau wote wa maenndeleo ili kuhakikisha kuwa awamu ya tatu ya TASAF
itafanikiwa na kuleta tija iliyokuwa kwa wananchi wa Zanzibar na Tanzania kwa
ujumla.
Naye
Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF, Ladislaus Mwamanga alisema katika kipindi cha
kwanza cha awamu ya tatu ya TASAF, kiasi cha Tsh trilioni 1.46 kimetumika
ambapo utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini umefanyika katika Mamlaka
za Serikali 159 kwa Tanzania Bara pamoja na Wilaya zote 11 kwa upande wa
Zanzibar.
‘’Utekelezaji
wa kipindi cha kwanza cha Awamu ya tatu ya TASAF katika Mpango wa Kunusuru Kaya
Maskini nchini ulijikita katika kutoa ruzuku kwa masharti, kutoa ajira ya muda,
kuongeza kipato, kujenga na kuboresha miundombinu na kujenga uwezo katika ngazi
zote za utekelezaji’’ alisema Mwamanga.
Aliongeza
kuwa utekelezaji wa kipindi cha kwanza cha Awamu ya Tatu ya TASAF katika Mpango
wa Kunusuru Kaya Maskini umekuwa na mafanikio makubwa ambapo jumla ya miradi
8,809 yenye thamani ya Tsh Bilioni 130 kutoka vijiji/shehia 2,578 ilibuliwa na
kutekelezwa na jamii ambapo jumla ya Tsh. Bilioni 97.5 zimetumika kulipa ujira
kwa walengwa kwa walioshiriki kufanya kazi kwenye miradi.
Naye
Mwakilishi wa Benki ya Dunia Ofisi ya Dar es Salaam Ms Preet Arora, ameipongeza
Serikali ya Tanzania kwa kuwa na mradi bora zaidi duniani ambao umewawezesha
wananchi wa kipato cha chini kuweza kujiongeza kipato pamoja na kumudu gharama
mbalimbali za huduma za kijamii ikiwemo elimu, afya n.k.
No comments:
Post a Comment