Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein Azungumza na Uongozi wa Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Uongozi wa Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ, Wakiwasilisha Taarifa ya Utekelezaji wa Mpango Kazi kwa mwezi wa Julai hadi Disemba 2029 /2020, uliofanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein ameitaka Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa ma Idara maalum za SMZ kushirikiana na Wizara Afya na kuwa na  mipango ya pamoja itakayowezesha uendelezaji wa kituo cha Afya Mbuzini na kuwa Hospitali ya Wilaya Magharibi ‘A’.

Dk. Shein amesema hayo Ikulu Jijini Zanzibar, wakati akipokea taarifa ya Utekelezaji ya mpango kazi ya Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara maalum za SMZ, kwa kipindi cha Julai hadi Disemba 2019/2020.

Alisema jengo hilo linaweza kuendelezwa kupitia bajeti za Wizara hizo na ujenzi wake kufanyika awamu kwa awamu, ili liweze kuwasaidia wananchi wa maeneo hayo na vitongoji jirani.

Alisema jengo hilo la zamani lililogharimu fedha nyingi katika ujenzi wake lipo mahala pazuri na linafaa kuendelezwa kwa dhamira ya kuwasaidia wananchi katika upatikanaji wa huduma za Afya.

“Jengo lile lipo mahala pazuri, lipo barabarani litaweza kuwasaidia wananchi wa Wilaya Magharibi ‘A’ likiendelezwa na kuwa hospitali ya Wilaya “, alisema.

Aidha, Dk. Shein aliwakumbusha Wakuu wa Mikoa juu ya dhima waliyonayo katika ulinzi na usalama wa Mikoa yao kwa kuhakikisha hakuna mgeni au mwekezaji anaefanya shughuli zinazoashiria uvunjifu amani na kuingilia usalama wa  nchi.

Kauli ya Rais Dk. Shein ilikuja kufuatia taarifa ya kuwepo raia wa kigeni kutoka nchini Uingereza alietengeneza makaazi juu ya mibuyu katika eneo la Pete, huku kukiwa na viashiria kadhaa  katika makaazi hayo vinavyohatarisha usalama wa nchi.

Kwa kushirikiana na vyombo vya Ulinzi na Usalama , aliagiza kufanyika uchunguzi ili kubaini uhalali wa mgeni huyo kuwepo nchini na kumiiliki eneo hilo pamoja na vifaa anavyomiliki, vinginevyo hatua za kiusalama zichukuliwe dhidi yake.

Aidha, aliwataka viongozi wa Wizara hiyo pamoja na Viongozi wa Mkoa Kusini na Wilaya Kusini kukutana na akinamama wa shehiya Kizimkazi wanaojishughulisha na kazi za kutanda dagaa na kuwasikiliza , ili kuona vipi wataweza kuwasaidia kuendeleza shughuli zao , huku kukiwa na katazo la kuepukana na uharibifu wa mazingira katika ghuba ya Menai.

Vile vile, aliushauri uongozi wa Wizara hiyo kuandaa utaratibu maalum utakaowezesha kupatikana maeneo mbadala, ili vijana wanaoondoshwa katika maeneo waliyojikusanya muda mrefu na ambayo hayako rasmi waweze kuondoka na kwenda kuendeleza maisha yao katika maeneo mapya.

Rais Dk. Shein aliukumbusha uongozi wa Wilaya ndogo Tumbatu umuhimu wa kutoa taaluma kwa manahodha na wananchi kuepuka kujaza abiria na mizigo katika vyombo vya baharini kupita kiasi, ili kuepuka athari zinazoweza kujitokeza.

Akigusia changamoto zinaoikabili Hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani, Dk. Shein aliutaka uongozi wa Wilaya hiyo kuwafahamisha wananchi juu ya maharibiko ya baadhi ya vifaa muhimu vya uchunguzi, wakati ambapo Serikali imekuwa ikifanya juhudi za kuvifanyia matengenezo, na kubainisha kuwa matatizo yaliopo ni ya muda.

Aidha, alitaka kuangalia upya taratibu za ajira, vyeo na uhamisho kati ya Unguja na Pemba kwa wafanyakazi wa sekta za Afya na Elimu walioko katika Ugatuzi ili kudhihirisha dhana na malengo ya Ugatuzi, wakati ambapo hivi sasa Wizara zinazohusika na sekta hizo zinaonekana kuendelea kushughulikia mambo hayo badala ya Halmashauri za Wilaya.

Vile vile, aliwataka watendaji wa Halmashauri kote nchni kusimamia matumizi bora ya masoko kwa kuhakikisha wafanyabaishara wanapanga bidhaa zao katika maeneo yaliowekwa an Serikali badala ya kupanga barabarani.

Mapema, akiwasilisha taarifa ya Utekelezaji ya mpango kazi kwa kipindi cha Julai hadi Disemba 2019/2020, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais na Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara maalum za SMZ Haji Omar Kheir alisema katika kipindi hicho Ofisi hiyo imepata mafanikio makubwa, baada ya kuidhinishiwa jumla ya shilingi 107,297,564,386/ ikiwa ni asilimia 95 ya makadirio.

Alisema miongoni mwa mafanikio hayo ni utekelezaji wa maamuzi ya Serikali ya kuanzisha mfumo wa Ugatuzi na kupeleka madaraka kwa wananchi.

Alisema Serikali kupitia Wizara ya Fedha na Mipango imeendelea kutoa fedha za ruzuku lwa Serikali za Mitaa ili kuziwezesha kutekeleza maukumu yao, ambapo kwa kipindi cha Julai – Disemba,2019 ilifanikiwa kupata ruzuku ya shilingi 39,009,250,003/, ikiwa sawa na asilimia mia moja.

Alisema katika kipindi hicho pia kulifanyika uzinduzi wa Vitambulisho vipya vya Mzanzibari mkaazi vyenye kutumia mfumo wa  kisasa, ambapo zoezi la ugawaji wake kwa wananchi lilianza rasmi Novemba 27, 2019 katika Wilaya ya Micheweni Pemba.

Aidha, alisema mfumo wa Usajili wa Vizazi umefanikiwa kufikishwa na kufungwa katika baadhi ya Hospitali ili kurahisisha upatikanaji wa  vyeti vya kuzaliwa kwa wakati.

Alieleza kuwa utoaji wa vyeti vya kuzaliwa ulianza kufanyika katika Wilaya kumi (10), huku taratibu za kurejesha  Mkonga wa Taifa  Wilaya ya Kaskazini ‘B’ zikianza.

Katika hatua nyengine, Waziri Kheir aliipongeza Serikali kwa kusimamia kwa vitendo tamko la Elimu bila malipo na kubainisha kuwa katika kipindi hicho imefanikiwa kununua mabuku kwa ajili ya wanafunzi wote wa skuli za msingi na maandalizi.

Alisema katika mwezi wa Disemba 2019, jumla ya makontena 32 yenye mabuku ya kuandikia, mabuku ya mahudhurio ya wanafunzi na kadi za maendeleo za wanafunzi ziliwasili nchini kutoka China na hatimae zoezi la ugawaji kufanyika katika Wilaya zote 11 za Unguja na Pemba.

Alieleza kuwa shughuli za uhamasishaji wa uandikishaji wa wanafunzi wa elimu ya msingi na maandalizi ulifanyika ambapo wanafunzi wapya 79,371 waliandikishwa.

Hata hivyo alisema pamoja na changamoto ya kutoingiziwa fedha, Baraza la Jiji la Zanzibar lilifanya uchaguzi wa Mheshimiwa Meya na Naibu Meya , sambamba na kubuni na kuandaa mapendekezo ya miradi minane kwa ajili ya kufanyiwa upembuzi yakinifu na kupanga utekelezaji wake.

Aidha, Mkuu wa Mkoa Kusini Unguja Ayoub Mohamoud alisema Uongozi wa Mkoa huo umo katika maandalizi ya kuanzisha mahakama ya Halmashauri ya Wilaya Kusini kama ilivyo kwa Wilaya Kati, ili kuharakisha uchukuwaji wa hatua dhidi ya makosa mbali mbali, ikiwemo ya wizi wa rasilimali za misitu ya Serikali.  

Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 
 E-mail: abdya062@gmail.com

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.