Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akizungumza na Uongozi wa Wizara Katiba na Sheria katika kikao cha utekelezaji wa Mpango kazi kwa kipindi cha Julai-Disemba2019 katika ukumbi wa Ikulu Mjini Zanzibar.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameutaka uongozi wa Wizara ya Katiba na Sheria
kuendeleza uadilifu na usimamizi
mzuri wa kazi zao hasa kwa vile Wizara hiyo ndio inayosimamia Sheria.
Hayo ameyasema leo, Ikulu Jijini Zanzibar
alipokutana na uongozi wa Wizara ya Katiba na Sheria wakati ilipowasilisha Utekelezaji
wa Mpango Kazi kwa kipindi cha Julai
hadi Disemba kwa mwaka wa fedha 2019/2020.
Rais Dk. Shein alisema kuwa usimamizi mzuri wa
kazi sambamba na uadilifu kwa viongozi hao ni njia pekee ya kuimarisha utendaji
wa kazi ikiwa ni pamoja na kutoa haki kwa wananchi hasa ikizingatiwa kwamba
Wizara hiyo inaigusa moja kwa moja jamii.
Rais Dk. Shein aliupongeza uongozi wa Wizara hiyo
pamoja na watendaji wote wa kike na wa kiume kwa kutekeleza vyema majukumu yao
ya kazi na kuwasisitiza kuendeleza juhudi zao hizo ili Zanzibar izidi
kuimarisha katika sekta ya sheria.
Alisema kuwa Wizara hiyo imeundwa kutokana na
umuhimu wake mkubwa licha ya kujitokeza kwa baadhi ya changamoto ndogo ndogo pale
ilipoanzishwa ikiwemo uhaba wa nyenzo lakini hata hivyo hatua kubwa imefikiwa na
kuweza kufanya kazi zake vizuri.
Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alisema kuwa ili
watumishi wa Umma katika kada zote waendelee kupata maslahi mazuri Serikali kwa
upande wake itafanya jitihada zake pale tu mapato yatakapoongezeka basi watumishi
wa umma nao watatizamwa kimaslahi.
Rais Dk. Shein alieleza azma ya kuanzishwa kwa
Skuli ya Sheria hali ambayo itasaidia kwa kiasi kikubwa kuimarisha sekta ya
sheria hapa nchini.
Akieleza hatua zinazoendelea za kuanzishwa kwa
Skuli ya Sheria, Rais Dk. Shein alisema haja ya kuwekwa mipango maalum kati ya
Tume ya Mipango ya Serikali na Ofisi ya Utumishi wa Umma kwa ajili ya mipango
ya hapo baadae.
Alieleza kuwa ni wajibu kwa uongozi wa Wizara hiyo
kuzigeuza changamoto kuwa mafanikio, na ukaendelea kufanya kazi zake kwa
ufanisi zaidi hasa ikizingatiwa kuwa kwa upande wa Sheria Zanzibari iko vizuri
na imekuwa ikijipatia sifa.
Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la
Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee alisema kuwa taarifa hiyo imetayarishwa
vizuri na kuwasilishwa vyema huku akisisitiza kuwa Wizara hiyo ni kioo hivyo ni
vyema wakaendelea kutekeleza kazi zao kwa ufanisi huku uongozi huo ukihakikisha
kwamba kila mwenye haki yake anaipata.
Nae Waziri wa Wizara ya
Katiba na Sheria Zanzibar, Khamis Juma Mwalim alieleza kuwa utekelezaji wa Wizara ya
Katiba na Sheria umezingatia Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambayo
imezungumzia sekta ya sheria katika Ibara ya 121 ya Ilani ya CCM ya mwaka 2015-2020.
Aidha, Mipango Mikuu ya Kitaifa ikiwemo MKUZA na
Dira ya Maendeleo 2020 ambapo vyote kwa pamoja vinazingatia na kusisitiza suala
la upatikanaji wa haki, kudumisha amani, utulivu na usalama wa maisha ya
wananchi na mali zao.
Alisema kuwa Wizara imeendelea kuratibu na
kusimamia utekelezaji wa miongozo mbali mbali ikiwemo Sera, Sheria na kanuni
ambapo kwa kipindi hiki imekamilisha matayarisho ya kuanzishwa kwa jukwaa la
pamoja la wadau wa sekta ya Sheria (JSF) na kuandaa rasimu ya Sera ya Skuli ya
Sheria na kuitafsiri kwa lugha ya Kiswahili.
Aidha, alisema kuwa Wizara katika kuhakikisha
kwamba azma ya serikali ya kuona kwamba wananchi wananufaika kwa kupata huduma
ya msaada wa kisheria mambo mbali mbali yamefanyika ikiwa ni pamoja na
kuchapisha na kusambaza nakala za Sheria ya Msaada wa Kisheria kwa lugha nyepesi
ili ieleweke na kutumika ipasavyo.
Alieleza kuwa Afisi ya Mwanasheria Mkuu imeendelea
na kazi yake ya msingi ya kuishauri Serikali katika masuala mbali mbali ikiwemo
ya mikataba.
Pia, Tume ya Kurekebisha Sheria imeendelea
kuzifanyia mapitio Sheria 4 na kufanya uchambuzi wa matumizi ya Sheria 44
zinazotumika Zanzibar pamoja na kuziweka katika lugha nyepesi ya Kiswahili
ikiwemo Sheria ya Ukomo wa Madai ya mwaka 1917 na Sheria ya Kamisheni ya Wakfu
na Mali ya Amana ya mwaka 2007.
Pamoja na hayo, alisema kuwa uratibu wa masuala ya
kidini umeendelea ambapo Kamisheni ya Wakfu na Mali ya Amana imeendelea na
hatua za kuanzisha mfuko wa Hijja ambapo matarajio ni kuuzindua katika mwaka
huu wa fedha.
Aidha, mkakati wa kudhibiti migogoro ndani ya ndoa
na utoaji wa talaka kiholela unaendelea na sasa matokeo ya utafiti wa ongezeko
la talaka yameanza kutumika katika semina na utatuzi wa migogoro inayofikishwa
katika Ofisi ya Mufti wa Zanzibar. Aidha,
mafunzo ya muongozo wa kufundishia kwa walimu wa vyuo vya Qur-an na mafunzo kwa
wana ndoa watarajiwa yameendelea kutolewa.
Mapema Katibu Mkuu wa Wizara hiyo George Joseph
Kazi akisoma taarifa ya Utekelezaji wa Mpango Kazi wa Wizara hiyo alieleza
jinsi juhudi zilinavyochukuliwa katika
kuratibu masuala mbali mbali ikiwa ni pamoja na mafunzo kwa maafisa habari
kuhusu uandishi bora wa taarifa za kisheria.
Nao viongozi wa Wizara hiyo walieleza
kuwa katika uongozi wa Rais Dk. Shein sekta ya sheria imepata mafanikio makubwa
sana huku wakieleza mafanikio
yalivyopatikana katika Wizara hiyo ikiwa ni pamoja na kupungua kwa ongezeko na
migogoro ya talaka kutokana na mafunzo yanayotolewa na Ofisi ya Mufti Zanzibar.
Aidha, viongozi hao walieleza
suala la ushahidi wa kesi zikiwemo za ubakaji jinsi zinavyokosa ushahidi licha
ya juhudi kubwa zinazochukuliwa na mahakama lakini wakati mwengine umakini wa
wananchi katika ushahidi unakosekana.
Pia, viongozi hao wamepongeza
utaratibu huo wa Bangokitita jinsi unavyowasaidia katika kutekeleza majukumu
yao pamoja na hatua wanazozichukua katika suala zima la upatikanaji wa haki.
Wakieleza kuhusu mfuko wa
Hijja, viongozi hao walieleza kuwa Mfuko huo ukianzishwa utawasaidia sana hasa
vijana kuhiji mapema ikilinganishwa na hivi sasa ambapo wananchi wengi husubiri
mpaka wapate viinua vyao mgongo na ndipo wakahiji jambo ambalo hata Serikali
itafaidika.
Hata hivyo, uongozi huo
ulieleza kuwa kutokana na maradhi ya Virusi vya Corona yaliosambaa duniani Serikali
ya Saudia Arabia imezuia ibada ya Umra lakini Kamisheni ya Wakfu na Mali ya
Amana imeambiwa matayarisho yote ya ibada ya Hijja mwaka huu yaendelee kama
kawaida.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment