Habari za Punde

Mwaka Kogwa Kufanyika Mwezi wa Julai 17, 2020 .

Mwenyekiti wa Kamati ya Mwaka Kogwa Mwita Masemo Makungu wa kwanza (Kushoto) akielezea kuhusu maandalizi ya Skukuu ya Mwaka kogwa huko Makunduchi Mkoa wa Kusini Unguja, wa kwanza (kulia) ni Mkuu wa Kamati hiyo Ali Hatibu na (wakati kati ) ni Mjumbe wa Kamati ya Mwaka Kogwa Haji Ramadhan Haji.
Picha na Maryam Kidiko – Maelezo Zanzibar.
Na Bahati Habibu – Maelezo.          29/06/2020.
Wazanzibari  wametakiwa kulinda kuzienzi na kuzitangaza mila na desturi zinazowatambulisha kwa mataifa mengine ili kuwa endelevu kwao na vizazi vijavyo .
Hayo yameelezwa na mwenyekiti wa kamati ya  skukuu ya mwaka kogwa Bwana Mwita Masemo Makungu wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari huko Makunduchi katika kijiji cha Koba Wilaya ya Kusini Unguja.
Amesema miongoni mwa mila za kizanzibari ni sikukuu ya mwaka kogwa ambazo hufanyika  Makunduchi kila mwaka  ambazo kwa sasa zinatambulika kuwa ni sherehe za kitaifa ambapo wageni wa ndani na nje ya nchi huhudhuria skukuu hiyo .
Aidha ameeleza kuwa skukuu hiyo ni miongoni mwa mila na tamaduni zilizoletwa na watu waliotoka bara la Asia na kufikia katika kijiji hicho  cha Makunduchi ambapo mwanzo walikipa jina la Kae kuu lenye maana ya sehemu inayoishi watu .
 Nae katibu wa kamati hiyo Ali Khatibu Ali  amesema  Skukuu ya Mwaka Kogwa ni kitu wanachojivunia kutokana na  kusheherekewa na  watu wa matifa mbali mbali  hivyo kuwa ni chanzo cha mapato kwa Taifa na nembo ya Taifa.
  Sambamba na hayo amewataka watu wanaoishi Makunduchi kuwa wakarimu  kwa wageni watakaohudhuria katika Skukuu hiyo kwa kuwapikia chakula cha asili na kuwatembeza sehemu za kihistoria katika kijiji chao.
Nae mjumbe wa kamati ya mwaka kogwa Haji Ramadhan amewataka vijana kuhudhuria  kwa wingi katika kuadhimisha skukuu hiyo ambayo ni ya asili hasa kwa wale wenye asili ya Makunduchi.
 Aidha amewataka wale wote watakaohudhuria Skukuu ya Mwaka Kogwa  kuwa na tahadhari ya kujikinga na maradhi ya korona ambapo skukuu hiyo  inatarajiwa kufanyika tarehe 17 ya mwezi wa saba  kwa mwaka huu.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.