Habari za Punde

Wanawake Pamoja na Wananchi Kuzingatia Kutunza Amani Iliyopo Hivi Sasa na Baada ya Uchaguzi


Mke wa Rais wa Zanzibar Mama Mwanamwema Shein akihutubia katika hafla ya ufunguzi wa Kongamano Maalum la Wanawake "Umoja Wetu Wanawake Ndio Nguvu Yetu" lililofanyika katika ukumbi wa Afisi ya CCM Mkoa wa Mjini Kichama Amani Jijini Zanzibar.

Mapema Mgeni Maalum wa Kongamano hilo Mama Mwanamwema Shein katika hotuba yake alieleza kuwa Kongamano hilo maalum limeandaliwa na Umoja wa Wake wa Viongozi kwa kushirikiana na Umoja wa Wanawake wa Tanzania (UWT).

Mama Shein alitumia fursa hiyo kuwasihi wanawake pamoja na wananchi  wote kuzingatia umuhimu wa kutunza amani iliyopo hivi sasa na baada ya uchaguzi.

Alieleza kuwa bila ya amani hakuna lolote linaloweza kufanikiwa kwani bahati mbaya ni kuwa wanawake na watoto ndio wanaoathirika sana wakati amani na usalama vinapotoweka.

“Tumuombe Mwenyezi Mungu atujaalie tuweze kushiriki katika uchaguzi Mkuu kwa amni, salama na utulivu”,alisema Mama Shein.

Mama Shein alitoa pongezi zake kwa wanawake kwa kuchagua kauli mbiu ya Kongamano hilo isemayo “Umoja wetu ndio nguvu yetu”, na kueleza kuwa anakubaliana na kauli mbiu hiyo kutokana na ukweli na umuhimu wake.

Alisema kuwa wanawake wakiwa pamoja ndio watakuwa na nguvu zaidi ya kufanya uwamuzi unaofaa kwa faida yao na kusisitiza kuwa uwamuzi unaofaa hivi sasa ni kuipigania CCM ili ishinde katika nafasi zote za uongozi katika uchaguzi Mkuu ujao.

“Tusisahau maneno ya wazee wetu yasemayo “Umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu”.

Aidha, Mama Shein alisema kuwa umoja na mshikamano ni mambo ya msingi katika kukipatia ushindi wa kishindo Chama Cha Mapinduzi na kuwataka wagombea wa nafasi mbali mbali katika chama hicho ni vyema wavunje makundi yao na waunge mkono wagombea wote waliopitishwa na CCM na kuendelea kuwa kitu kimoja.

Pamoja na hayo, alisema kuwa Mgombea wa Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM Dk. Hussein Mwinyi ni mtu makini, mwenye uzoefu mkubwa katika uongozi na anaependa maendeleo.

Nae Mgeni rasmi katika Kongamano hilo Mwenyekiti wa (UWT) Gaudentia Kabaka aliwataka wagombea wote wanawake waliogombea nafasi mbali mbali za uongozi kuwa kitu kimoja na kufahamu kuwa huo walioupata ni uteuzi si ushindi kwani wapo walioshinda kwa kura nyingi lakini hawakuteuliwa na badala yake wameteuliwa wale wenye kura kidogo.

Alieleza kuwa CCM ni chama kikubwa na kueleza kuwa wanawake wanajukumu kubwa la kutafuta kura za Ubunge, Uwakilishi, Udiwani pamoja na Urais wa Jamhuri ya Muungano na Urais wa Zanzibar.

Alitumia fursa hiyo kuupongeza mchakato wa kuwapata viongozi ndani ya CCM ulivyofanyika na kuwataka wagombea ndani ya CCM kufahamu kuwa katika mchakato huo wa kuwapata wagombea hakukuwa na chuki wala uadui kwani CCM ina katiba nzuri inayokwenda kwa kanuni na taratibu nzuri.

Kwa upande wake kiongozi wa Umoja wa Wake wa Viongozi MamaAsha Balozi alitoa pongezi kwa Mama Shein kwa ushirikiano wake mkubwa katika kufanikisha Kongamano hilo pamoja na kueleza hatua zilizofikiwa na Umoja huo.

Katika Kongamano hilo Mada mbali mbali zilitolewa ikiwemo “Wanawake Kutokata Tamaa”, aliyotolewa Balozi Amina Salum Ali, Waziri wa Biashara na Viwanda, Mada ya “Amani na Utulivu”,iliyotolewa na Sharifa Abeid Salum kutoka Ofisi ya Makamo wa Pili wa rais wa Zanzibar na Mada ya Tatu ilikuwa ni “Uzalendo na Mshikamano” iliyotolewa na Catherine Peter Nao Katibu wa Idara ya Uenezi Zanzibar.

Sambamba na hayo Kongamano hilo liling’arishwa na burudani mbali mbali kikiwemo kikundi cha Taarab cha “Big Star” cha Chama Cha Mapinduzi (CCM) huku Dj Maarufu wa Zanzibar Kul Para akionesha mbwembwe zake katika tasnia ya muziki.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.