Habari za Punde

Ofisi ya Mtakwimu Mkuu inajivunia hatua kubwa iliyopiga ya uboreshaji wa takwimu kwa njia ya teknolojia

Mtakwimu Mkuu wa Serikali  Mayasa Mahfoudh Mwinyi akisoma hotuba katika Maadhimisho ya kilele cha siku ya Takwimu Afrika yalifanyika Ofisi za Mtakwimu Mkuu wa Serikali Mazizini Zanzibar.

Naibu Katibu Mtendaji Tume ya Mipango Zanzibar Dk.Juma Malik Akili akizungumza na wadau wa sekta mbali mbali (hawamo pichani) kuhusu umuhimu wa takwimu katika kilele cha kuadhimisha siku ya takwimu Afrika huko Ofisi za Mtakwimu Mkuu wa Serikali Mazizini Zanzibar.


PICHA NA MWASHUNGI TWAHIR MAELEZO ZANZIBAR.

Na Mwashungi Tahir      Maelezo     18-11-2020.

Kuwepo kwa mashirikiano  ya utoaji wa taarifa za uhakika katika taasisi za Serikali kutasaidia  kupata takwimu zilizo sahihi  ambazo zitasaidia katika kupanga mipango bora ya  maendeleo ya Nchi.

Ameyasema hayo Naibu  Katibu Mtendaji Tume ya Mipango Zanzibar  Dr Juma Malik Akili kwa niaba ya ya Katibu Mtendaji wa Timu hiyo  leo huko katika Ukumbi wa  Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali Zanzibar ilioko Mazizini wakati wa Maadhimisho ya siku ya Takwimu Afrika.

Amesema kwamba maendeleo yoyote ya kweli katika Nchi zote duniani yanatokana na Takwimu zinazozalishwa  kwa mifumo mizuri ambazo zitakuwa za kweli na za uhakika.

Amesema Serikali ya awamu ya nane imeanza kuleta mabadiliko ya haraka katika Serikali ikiwa na lengo ya kuweka mipango ilio bora  katika kupatikana uhakika wa Takwimu zilizo sahihi.

“Wito wangu kuwa na mashirikiano na Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali Zanzibar katika utoaji wa takwimu zilizo sahihi”, alisema Naibu huyo.

Nae Mtakwimu Mkuu wa Serikali Zanzibar Mayasa Mahfoudh Mwinyi amesema ikiwa Afrika inaadhimisha siku ya Takwimu Ofisi ya Mtakwimu Mkuu inajivunia hatua kubwa iliyopiga ya uboreshaji wa takwimu kutoka katika matumizi ya karatasi na pia kutumia ukusanyaji wa takwimu kwa njia ya teknolojia.

Aidha amesema maadhimisho ya Siku ya Takwimu duniani  yanaandaliwa kwa lengo la kuielimisha jamii juu ya umuhimu na jukumu la kila mmoja wetu katika ukusanyaji uchambuzi na uwasilishaji wa Takwimu sahihi  kwa ajili ya mipango ya maendeleo ya nchi za Afrika.

Pia amesema Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali inawaomba wadau mbali mbali na jamii kwa ujumla kutoa mashirikiano ya dhati katika suala zima la utoaji wa taarifa sahihi ili kuwa na takwimu bora kwa mipango ya maendeleo ya nchi yetu.

Kwa upande wa washiriki  wa sekta mbali mbali katika maadhimisho hayo  wamesema licha ya maendeleo yaliyopatikana wanahitaji kupatiwa elimu ili kuondosha changamoto ndogo ndogo za utumiaji wa mitandao.

 Siku ya Takwimu ya Afrika huadhimisha kila ifikapo tarehe 18 Novemba ambapo kauli mbiu ya mwaka huu  ni uimarishaji wa mifumo ya Takwimu  Kitaifa kwa uzalishaji wa taarifa na utoaji wa Takwimu  ili kuwepo kwa amani na maendeleo endelevu Barani Afrika.

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.