Habari za Punde

Wananchi Zanzibar Waaswa Kutumia Hati Miliki za Ardhi Kujikwamua Kiuchumi

Na Mwandishi wetu- Unguja

Wananchi  Visiwani Zanzibar wameaswa ktumia hati miliki za kumiliki ardhi kujiletea maendeleo  ili kuendana na falsafa ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) inayolenga kujenga uchumi  wa buluu unaowanufaisha wananchi wote.

Hayo yamesemwa na Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi ya Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge Tanzania (MKURABITA) Bi Immaculata Senje wakati wa hafla ya kukabidhi hati miliki za kumiliki ardhi zipatazo 50  kwa wananchi wa Welezo wilaya ya Magharibi A, Unguja leo Februari 9, 2021 baada ya urasimishaji ardhi.

“ Hati miliki za ardhi mlizopata ni mtaji hivyo zitumieni katika kujiendeleza kwa kuanzisha shughuli za uzalishaji kupitia mikopo kutoka katika taasisi za fedha kama mabenki ambayo yemeonesha dhahiri kuwa yako tayari kuwakopesha kwa kutumia hati hizi”, alisisitiza Bi. Senje

Akifafanua amesema kuwa dhamira ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibari (SMZ) ni kuona wananchi wananufaika na rasilimali zilizopo ikiwemo ardhi hivyo kila mwananchi ana wajibu wa kuhakikisha anatumia fursa hiyo ya urasimishaji ardhi katika kujiletea maendeleo.

Mratibu wa MKURABITA Dkt. Seraphia Mgembe  amesema kuwa wananchi waliopata hati hizo wanapaswa kuwa chachu  kwa wale ambao bado hawajarasimisha maeneo yao kwa kutumia hati hizo kupata mitaji katika taasisi za fedha.

Aliongeza kuwa katika maeneo mengi  wananchi waliofikiwa na mpango huo wametumia hati zao kukopa na kukuza mitaji yao hali iliyowawezesha kuchangia katika kujenga uchumi na kuzalisha ajira.

“ Kila Mwananchi hapa Zanzibar ana jukumu la kuunga mkono juhudi za Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) Dkt. Hussein Ali Mwinyi kupitia hati hizi na kushiriki kikamilifu katika kujiletea ukombozi wa kiuchumi kama inavyosisitiza Serikali”, alieleza  Dkt. Mghembe.

Naye Afisa kutoka Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ) Bw. Ali Alhaj Masoud amesema kuwa Benki hiyo iko tayari kuwakopesha wananchi kwa kutumia hati za kumiliki ardhi zilizotolewa na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.

MKURABITA  kwa kushirikiana na wizara za kisekta za Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) ikiwemo Wizara ya ardhi na Maendeleo ya Makaazi imewezesha kutolewa kwa hati za kumiliki ardhi   kwa wakaazi wa Pemba na Unguja tangu kuanza kwa urasimishaji hadi sasa.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.