Habari za Punde

NMB,Vodacom na Just Fit Wadhamini Mashindano ya Zanzibar International Marathon Yanayotarajiwa Kufanyika Mwezi Julai 2021.Zanzibar.

Meneja wa Benki ya NMB Tawi la Zanzibar Ndg. Abdalla Duchi, Benki ya NMB imedhamini Mashindano ya Kimataifa ya Mbio za Zanzibar International  Marathon, akimfanyia usajili wa kushiriki Marathon Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe.Hemed Suleiman Abdalla, wakati Kamati ya Zanzibar Marathon walipofika ofisini kwake Vuga Jijini Zanzibar kwa mazungumzo.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla akikabidhia pea ya viatu vya raba kwa ajili ya kushiriki katika mashindano ya Kimataifa ya Zanzibar International Marathan na Balozi wa Kutangaza Marathon Salama Jabir, hafla hiyo imefanyika katika Ofisi ya Makamu Vuga Jijini Zanzibar.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla akizungumza na Kamati ya maandalizi ya mashindano ya mbio za Zanzibar International Marathon zinazotarajiwa kufanyika Julai 18, Mwaka huu.

Na.Kassim Abdi.OMPR Zanzibar.                                                                                                             

Wananchi wametakiwa kujisaajili katika ushiriki wa Mashindano ya mbio za Zanzibar international marathon zinazotarajiwa kufanyika julai 18 mwaka huu.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla alitoa wito huo alipokutana na kufanya mazungumzo na kamati ya maandalizi ya mashindano hayo walipofika Ofisini kwake Vuga Jijni Zanzibar.

Alisema kwa kuwa mashindano hayo yamepata Baraka za Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la  Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi itatoa taswira njema endapo watu wengi watajitokeza kushiriki ikiwemo wenyeji na wageni kutoka mataifa mengine.

 Aidha Mhe. Hemed aliipongeza kamati hiyo kwa uzalendo wao kwa kujitolea kufanya maandalizi ya mashindano hayo jambo ambalo pia litasaaidia kuitangaza Zanzibar na vivutio vyake vya kitalii.

“Mashindano haya ya Marathoni yatakapofanyika yatasaidia kwa kiasi kikubwa wataali kuvitembelea vivutio vyetu ikiwemo na maeneo ya kihistoria”. Alisema Makamu wa Pili

Mhe. Hemed aliahidi kuwa serikali ya Mapinduzi Zanzibar itatoa kila aina ya ushirikiano katika mashindano hayo kutokana na jambo  litachangia kuwaunganisha wazanzibar na wageni kutoka maeneo tofauti.

Akigusia suala la udhimini wa mashindano hayo Makamu wa Pili wa Rais alisema serikali itazungumza na makampuni mbali mbali pamoja na mashirika yaliopo Zanzibar ili kushiriki kikamilifu.

Pia Mhe. Hemed alizipongeza taasisi ambazo tayari zimeanza kujitokeza kudhamini mashindano hayo ikiwemo Benki ya NMB, Vodacom, Just Fit na mabalozi wa kuitangaza Marathoni hiyo.

Alisisitiza kwamba, serikali kwa sasa imejipanga kuimarisha na kurejesha hadhi ya michezo Zanzibar hasa katika kuamsha ari kwa vijana wake kuchangamkia fursa zinazopatika ndani yake.

Nae Waziri wa Utalii na Mambo ya Kale ambae pia ni Kaimu Waziri wa Habari, vijana, Utamaduni na Michezo Mhe. Leila Muhamed Mussa alisema kuwepo kwa mashindano hayo ya marathon kutasaidia kuunga mkono azma ya Rais Dk. Mwinyi ya kukuza Uchumi wa Zanzibar hasa kupitia Uchumi wa Buluu ambapo sekta ya utalii ni moja kati ya maeneo ya uchumi huo.

Nao viongozi wa kamati hiyo wakiongozwa na Hassan Suleiman Zanga walimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kuwa lengo la Marathon hiyo kufanyika zanzibar ni kuhamasisha utalii hasa katika kipindi hichi cha mripuko wa maradhi ya covid 19 ambapo inaonekana sekta hiyo kususua katika mataifa mbali mbali.

Walieleza  kuwa, asilimia 20 ya mapato yatakayopatikana katika mashindano hayo yatafikishwa kwa wazee wasiojiweza, watoto yatima pamoja na watu wenye mahitaji maalum ili kutoa mchango wao kwa makundi hayo maalum.

Kamati hiyo ya mashindano pia imekamisha zoezi la kumfanyia usajili Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ambapo atashiriki katika mashindano hayo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.