Habari za Punde

RC Kusini: Migogoro 43 ya ardhi Mkoa wa Kusini tayari imeshapatiwa ufumbuzi


Mkuu wa Mkoa wa Kusini  Unguja Mhe.Rashid Hadid Rashid akitoa taarifa kwa Waandishi wa Habari wa Vyombo mbalimbali  kuhusiana na  utekelezaji wa kazi ndani ya mkoa wake kuanzia Disemba 2020  hadi Juni 2021 huko Ofisini kwake Tunguu Wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja.

PICHA NA FAUZIA MUSSA /MAELEZO ZANZIBAR

Na Khadija Khamis-Maelezo   27/06/2021.

 

Mkuu wa Mkoa Kusini Unguja Rashid Hadidi Rashid amesema jumla ya migogoro 125 ya ardhi iliojitokeza katika mkoa wa kusini Unguja  43  imeshapatiwa ufumbuzi .

 

Akitoa Taarifa  ya utekelezaji wa majukumu ya kiutendaji wa Kimkoa huko Ofisini kwake Tunguu wilaya ya Kati Unguja wakati  akizungumza na waandishi wa habari amesema migogoro iliopatiwa ufumbuzi ni ya wilaya ya kati na kusini Unguja .

 

Alisema  miongoni mwa migogoro iliyokuwa ikilalamikiwa na wananchi ni pamoja na ardhi moja kumilikiwa na watu wawili tofauti .

 

Alifahamisha kuwa ukosefu wa elimu kwa wananchi unachangia wingi wa migogoro kwa kutofahamu taratibu za kisheria kwa zile kesi  ambazo  zimeshatolewa hukumu na Mahakama ya Ardhi au ziko Mahakamani .

 

Akizungumzia ufuatiliaji wa miradi mbalimbali ya kimaendeleo katika awamu ya nane ya uongozi kuanzia mwezi disemba 2020 hadi June mwaka 2021 amesema katika Mkoa wa kusini jumla ya miradi minane mikubwa  imo katika mkoa huo

 

Alisema miongoni mwa miradi hiyo ni  Mradi wa Ujenzi wa Mahakama Kuu Tunguu uko vizuri karibuni utakabidhishwa Serikalini  pamoja na Skuli ya Kibuteni yenye dahalia tayari vijana 113 wanaendelea na masomo katika skuli hiyo.

 

Alifahamisha kuwa mradi wa ujenzi wa hospitali ya Binguni bado haujafikia kiwango kinachotakiwa  kutokana na uhaba wa fedha hivyo Serikali iko mbioni kuufanikisha .

 

Aidha alisema mradi wa umwagiliaji maji  wa kilimo Cheju uko vizuri karibuni utakabidhishwa Serikalini wakati mradi wa Skuli ya kisongo wa elimu ya Amali bado haujakabidhiwa kutokana na matatizo baina ya Mkandarasi na Wizara wakati wowote utakabidhiwa uanze kazi .

 

Akielezea  zaidi Mkuu huyo amefahamisha mradi wa ujenzi wa nyumba za kurekebisha tabia pamoja na mradi wa barabara ya jozani ukongoroni hadi charawe ni miongoni mwa  miradi mikubwa kwa Mkoa huo.

 Aidha amesema wafanyakazi  wanawajibika ipasavyo katika kusimamia wizi na rushwa katika utendaji wa kazi zao hata hivyo wamefanikiwa kukusanya kiasi cha shilling bilioni mia saba kwa Wilaya ya Kati ambapo kwa Wilaya Kusini ni zaidi ya milioni mia tano zimepatikana kwa Halimashauri na Mabaraza kuanzia Desemba hadi june 2020/2021.

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.