Wizara
ya Sanaa, Utamaduni na Michezo yasaini mkataba jengo la ghorofa sita
Na
Eleuteri Mangi, WSUM, Dodoma
Katibu
Mkuu wa Wizara ya Sanaa, Utamaduni na Michezo Dkt. Hassan Abbasi amesaini
mkataba wa ujenzi wa jengo la Wizara hiyo awamu ya pili lenye ghorofa sita na
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) Dkt. Maulid Banyani
litakalojengwa eneo la Mji wa Serikali Mtumba Jijini Dodoma.
Akizungumza
katika hafla hiyo ya utiaji saini leo Septemba 22, 2021 jijini Dodoma, Dkt.
Abbasi amesema jengo hilo litakuwa na ofisi za kisasa pamoja na mahitaji yote
yanayohusika katika sekta za Sanaa, Utamaduni na Michezo.
“Jengo
hili litakuwa la kihistoria kwa kuwa Wizara hii haijawahi kumiliki jengo la
hadhi hii nzuri, matarajio yetu jengo hili litakuwa kichocheo cha sekta hizo
kutoa huduma bora na stahili kwa wadau wa sekta na wanananchi kwa ujumla”
amesema Dkt. Abbasi.
Aidha,
Dkt. Abbasi amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia
Suluhu Hassan kwa kutoa fedha za ujenzi wa jengo hilo ambazo ni Bilioni 22.843
zipo na zitatolewa kulingana na taratibu za Serikali ambapo linatarajiwa
kukamilika ndani ya miezi 24 sawa na miaka miwili kuanzia sasa.
Katibu
Mkuu huyo amewahimiza Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) ambao ni watekelezaji wa
mradi wa ujenzi wa jengo hilo pamoja Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) ambao ni
wasanifu na wabunifu wa majengo hayo wakamilisha mradi huo kwa wakati na kwa
ubora unaotakiwa kwa kuwa wao ni mabingwa wameaminiwa kwa uzoefu wao katika
masuala ya ujenzi.
Akisisitiza
Serikali inavyodhamiria kusimamia sekta hizo, Katibu Mkuu Dkt. Abbasi amesema
hadi sasa Serikali imetenga fedha takriban bilioni 9 kuboresha viwanja na
kujenga maeneo ya burudani na kupumzikia wananchi, bilioni 1.5 za Mfuko wa
Sanaa na Utamaduni, bilioni 1.35 kugharimia timu za Taifa pamoja na bilioni 1.3
kujenga shule ya michezo kitaifa (Sports Academy) katika Chuo cha Maendeleo ya
Michezo Malya mkoani Mwanza.
Serikali
inatekeleza hayo yote ikitambua sekta za Sanaa, Utamaduni na Michezo ni nguvu
laini ambazo zinatambulisha taifa duniani kwa kazi zake ikiwemo muziki,
utamaduni, filamu na michezo na hivyo kuwapa wananchi burudani na furaha hatua
inayosaidia kuepuka magonjwa yasiyo ya lazima.
Kwa
upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) Dkt. Maulid
Banyani ameishukuru Wizara na Serikali ya Awamu ya Sita kwa kuwaamini na kuwapa
kazi ya ujenzi wa majengo ya Serikali kwa kuwa waliomba na wamepewa kazi hiyo
na kuahidi kuitekeleza kwa ubora na kwa wakati kama ilivyopangwa kulingana na
bajeti waliyopewa.
Naye
Katibu wa Kuratibu Serikali Kuhamia Dodoma Bw. Meshaki Bandawe amesema mpango
wa Serikali kuhamia Dodoma umerahisisha wizara kuwa na majengo yao na zipo
katika eneo moja hatua inayorahisisha wananchi kupata huduma kwa wakati.
Bw.
Bandawe ameongeza kuwa majengo ya Wizara yanayojengwa katika awamu ya pili yapo
24 ambapo hadi sasa Wizara nane ikiwemo ya Sanaa, Utamaduni na Michezo
zimekamilisha taratibu za ujenzi huo, hivyo zimetekeleza agizo la Mhe. Waziri
Mkuu Kassim Majaliwa alilotoa Septemba 08, 2021 la Wizara zote zikamilishe
taratibu za ujenzi wa awamu ya pili ifikapo Septemba 30, 2021.
No comments:
Post a Comment