Habari za Punde

Wito watolewa kushirikiana na walemavu ili waweze kujikimu kimaisha

 

Na Mwashungi Tahir   Maelezo      27-10-2021.

Jamii imetakiwa  kuwa na mashirikiano na watu wenye ulemavu ili  kuwawezesha kupata haki zao za msingi  na kuweza kujikimu  maisha.

Hayo yameelezwa  na Afisa Miradi na Utetezi wa Haki za Binaadamu Ali Yussuf wakati alipokuwa  akifungua mkutano wa Jukwaa la wadau wa Taifa  kwa  watu wenye ulemavu huko katika Ukumbi wa hoteli ya Golden Tulip  uliopo Malindi katika ukusanyaji wa taarifa za jumuiya za watu wenye ulemavu 2020.

Amesema  jamii iwapo itakuwa karibu  na watu wenye ulemavu na kusaidia changamoto zinazowakabili wataweza kufanya kazi zao kwa  ufanisi zaidi na kupata huduma zote zinazostahiki.

Amesema watu wenye ulemavu ni sehemu ya jamii hivyo ni vyema kupatiwa huduma zote za muhimu za kijamii  ikiwemo afya, elimu, uwezeshaji ili kukabiliana na maisha. 

Ameeleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imekuwa ikuwajali watu wenye ulemavu kwa kuwawekea miundo mbinu ya uhakika  katika maeneo mbalimbali  kwa lengo kuwarahisishia  na kuwaletea maendeleo.

Aidha ameomba kuwekea huduma lugha za alama katika sehemu zinazotoa huduma za kijamii ili kupata mahitaji yao bila ya usumbufu na kuweza kufahamika.

“Tunaishukuru Serikali kwa kuwasogezea huduma muhimu karibu ila vifaa vizidi kusogezwa hasa katika mambo ya afya”, alisema Afisa huyo.

Nae Mratibu wa Mradi wa Maendeleo Jumuishi katika Jamii Saida Amour Abdullah  amesema iko haja ya kuboreshwa baadhi ya huduma kwa lengo la  kunufaika na mradi huo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Viziwi  CHAVIZA Asha Ali Haji amesema jamii iwe na mwamko wa kuhamasisha kuhusiana na kuwatia haki za msingi  watu wenye ulemavu na kuacha tabia ya  kuwafungia ndani bila ya kuwapa huduma.

Mradi huo ni wa miaka mitano katika kila wilaya za Unguja na Pemba ambao umeanza kwa lengo  la kuhakikisha kwamba  haki za binaadamu zinapatikana inavyotakiwa kwa watu wenye ulemavu na umefadhiliwa na Jumuiya ya Watu wenye Ulemavu Norway.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.