Na Kassim Abdi, OMPR
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla amewaongoza waumini na wananchi katika maziko ya aliekuwa Kamishna wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar Makame Juma Pandu.
Mhe. Hemed amejumuika na wanafamilia pamoja na watendaji mbali mbali wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuustiri mwili wa marehemu Kamshna Makame Juma Pandu katika makaburi ya Mwanakwerekwe Wilaya ya Magharibi “B” Unguja.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alishiriki ibada ya Sala ya kumsalia maiti katika Masjid Jalyl uliopo mbuzini .
Mapema Asubuhi Mhe. Hemed alifika nyumbani kwao marehemu kwa ajili ya kuipa pole familia pamoja na kumuombea dua marehemu huyo.
Mhe. Hemed amewataka ndugu na jamaa kuwa wamoja,kusaidiana na kushirikiana katika kipindi hichi kigumu na kuendelea kumuombea safari ya kheri mzee wao ili apate radhi zake Allah (S.W).
Alisema marehemu Makame ameitumikia vyema Serikali kwa nafasi mbali mbali ambapo mchango wake umethaminiwa na atakumbukwa kwa mengi ikiwemo busara na hekima katika kuleta maendeleo nchini.
Marehemu Makame Juma Pandu katika uhai wake ametumikia Wizara ya Elimu, Mwanasheria wa Wizara ya Ardhi, Mfanyakazi wa Ofisi ya Mkurabita Jamhuri ya muungano wa Tanzania , hadi umauti unamkuta marehemu alikuwa kamishna wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar.
Marehemu amefariki akiwa na umri wa miaka 63 na amewacha vizuka wawili na watoto watano, watatu wa kike na wawili wa kiume
Mungu ailaze roho ya marehemu mahala pema peponi Aamin.
No comments:
Post a Comment