Habari za Punde

Kamishna wa Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB) Amekutana na Washauri wa Kodi na Kuwakumbushwa kufanya kazi kwa weledi.

Kamishna wa Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB) Ndg.Yusuph Juma Mwenda amekutana na kuzungumza na washauri wa kodi Zanzibar, wakati wa mkutano wake uliofanyika katika ukumbi wa ZRB Mazizini Unguja Jijini Zanzibar. 
 

Na. Mwandishi Wetu

Kamishna wa Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB) Ndg. Yusuph Juma Mwenda amewaasa washauri wa kodi kutojihusisha na kuwasaidia walipakodi katika kukwepa kulipa kodi stahiki Serikalini akisisitiza kuwa kufanya hivyo ni kinyume na maadili ya taaluma yao na sheria za nchi.

Kauli hiyo ameitoa mara baada ya kukutana na washauri wa kodi katika mkutano wa siku moja uliofanyika katika ukumbi wa mkutano wa jengo la ZRB Mazizini Zanzibar.

Kamishna huyo amesisitiza kuwa ili washauri wa kodi wawe weledi katika ufanyaji wao wa kazi ni lazima wafanye kazi kwa mujibu wa taratibu na sheria zilizowekwa pamoja na kujipambanua baina ya Serikali na walipakodi ili kuhakikisha kuwa mapato ya Serikali yanapatikana ikizingatiwa kuwa kiwango cha ulipaji kodi wa hiyari bado hakiridhishi Zanzibar.

Alisema kuwa, taaluma ya Ushauri wa Kodi ni taaluma muhimu kwa maendeleo ya nchi na kwamba wanapaswa kuwa Daraja muhimu baina ya Serikali na Walipakodi ili kufanikisha maendeleo ya nchi.

Pamoja na kufurahia mkutano huo ambao ni wa mwanzo kwa Kamishna na washauri hao, Washauri wa kodi waliorodhesha changamoto kadhaa za kiutendaji ambazo walimshauri Kamishna na uongozi wake kuzifanyia kazi ili kuimarisha ukusanyaji wa mapato.

Ikiwa ni katika kuchapuza uweledi wa washauri hao, ndugu Mwenda ameahidi kuyapatia ufumbuzi ndani ya kipindi kifupi changamoto za ukusanyaji zilizopo ZRB kwa kufungua ofisi za Mikoa Pamoja na kuwaongezea ujuzi watendaji wa taasisi hiyo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.