Habari za Punde

Dk. Mwinyi Amezipongeza Juhudi Zinazoendelea Kuchukuliwa na Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China Kuiunga Mkono Zanzibar Kuimarisha Sekta ya Afya.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na Madaktari Bingwa kutoka Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China wanaotoa huduma za Afya katika Hospitali za Unguja na Pemba, walipofika Ikulu Zanzibar kwa mazungumzo na kukabidhi Vifaa Tiba na Dawa mbalimbali kwa ajili ya Hospitli ya Kuu ya Rufaa ya Mnazi Mmoja Zanzibar,Kivunge Mkoa wa Kaskazini Unguja,Chakechake Pemba na Hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani Pemba, hafla hiyo iliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu Zanzibar leo 7-6-2022.
 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi amezipongeza juhudi zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China za kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta ya afya.

Rais Dk. Mwinyi aliyasema hayo leo Ikulu Zanzibar, katika mazungumzo kati yake na Timu ya Madaktari Bingwa kutoka Jimbo la Jiangsu nchini China ambao wanatoa huduma katika hospitali za hapa Zanzibar, mara baada ya kukabidhiwa na Timu hiyo dawa pamoja na vifaa tiba mbali mbali.

Katika mazungumzo hayo, Rais Dk. Mwinyi alisema kwamba kwa kipindi kirefu Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China imekuwa ikiisaidia Zanzibar katika kuimarisha sekta ya afya kwa kusaidia vifaa, dawa na hata Madaktari ambao wamekuwa wakija Zanzibar kutoka nchini China kila mwaka.

Rais Dk. Mwinyi alitoa shukurani kwa Timu ya Madaktari 21 kutoka China ambao wanatoa huduma za afya hapa nchini hivi sasa na kueleza kwamba misaada yao hiyo pamoja na huduma wanazozitoa zinasaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza uhaba wa Madaktari Bingwa, dawa pamoja na vifaa tiba katika hospitali za hapa Zanzibar.

Aidha, Rais Dk. Mwinyi alitoa pongezi kwa Timu hiyo ya Madaktari kwa kutoa huduma za afya zikiwemo zile za upasuaji wa kutumia teknolojia ya kisasa ambazo zimeweza kusaidia kuimarika kwa huduma za afya nchini.

Rais Dk. Mwinyi alieleza kufarajika na juhudi zinazochukuliwa na Timu hiyo ya kuwasomesha Madaktari wazalendo ambao wanatoa huduma za afya katika hospitali kadhaa za Unguja na Pemba.

Sambamba na hayo, alieleza hatua zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar za kuweka mazingira mazuri katika kuimarisha sekta ya afya ikiwa ni pamoja na ujenzi wa Hospitali za Wilaya unaoendelea hivi sasa, hali ambayo itaimarisha zaidi huduma za afya Unguja na Pemba.

Nae Waziri wa Afya, Nassor Ahmed Mazrui alieleza jinsi mashirikiano makubwa yaliopo kati ya Wizara yake pamoja na Timu hiyo Madaktari wanaotoa huduma zao katika hospitali za hapa Zanzibar huku akieleza kwamba dawa pamoja na vifaa tiba hivyo vina gharama ya zaidi ya TZS Milioni 300.

Mapema Kiongozi wa Timu hiyo ya Madaktari Bingwa kutoka China Dk. Qu Li Shuai alimueleza Rais Dk. Mwinyi juhudi zinazochukuliwa na timu hiyo yenye Madaktari 21 ambao kati ya hao 12 wanatoa huduma katika Hospitali ya Mnazi Mmoja na 9 wanatoa huduma katika hospitali ya Abdalla Mzee kisiwani Pemba.

Akitoa ufafanuzi juu ya misaada hiyo, Bwana Song Jianqing alimueleza Rais Dk. Mwinyi kwamba msaada huo ni muendelezo wa utamaduni wa uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati ya Zanzibar na China ambao umewekwa na waasisi wa nchi mbili hizo.

Bwana Jianqing alieleza kwamba Timu hiyo ya Madaktari ambayo iliwasili Zanzibar mnamo mwezi Septemba mwaka jana  imeanza kufanya kazi vizuri na tayari imeshatibu zaidi ya wananchi 50,000 na kuwafanyia upasuaji zaidi ya wagonjwa 6,000 katika hospitali  za Mnazi Mmoja, Abdalla Mzee na Kivunge.

Alieleza kuwa katika kuendeleza uhusiano na ushirikiano huo wa kihistoria uliopo Timu hiyo ya Madaktari Bingwa wameanzisha mafunzo kwa Madaktari wazalendo hatua ambayo itazidi kuimarisha sekta ya afya hapa Zanzibar.

Aidha, alieleza jinsi walivyofanya upasuaji kwa kutumia teknolojia ya kisasa hapa Zanzibar ambayo ni ya kwanza kufanyika katika hospitali za hapa Tanzania.

Aliongeza kuwa tayari wameshafanya pasuaji kadhaa zikiwemo za koo, masikio, macho, uchunguzi wa mfumo wa njia ya chakula na nyenginezo ambazo hapo mwanzo huduma hizo zilikuwa zikipatikana Tanzania Bara.  

Alivitaja miongoni mwa vifaa hivyo kuwa ni ECG defibrillator, potable echocardiography machines, probes, Trocar kwa ajili ya upasuaji wa laparoscopic, video ya laryngoscope, electric negative pressure suction devices, oxygen generators, multifunctional monitors, mesh, surgecal sutures na vyenginevyo.

Imetayarishwa na Idara ya Mawasiliano,

Ikulu Zanzibar.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.